Wednesday, September 28, 2016

HADITHI YAMENIKUTA SALAMA MIE SEHEMU YA 8

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI
 
YAMENIKUTA SALMA MIE 9 Inaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya Kampuni ya Usafirishaji abiria Tanga, Moshi, Arusha , Babati hadi Singida kila siku asubuhi, Freys wapo Tanga barabara ya 12 na kwa Singida wapo Kituo kikuu cha Mabasi yaendayo Mikoani, 0622 292990
 
ILIPOISHIA
 
Geti lilipokuwa wazi aliingia kwenye gari akaiingiza gari ndani. Tukashuka sote. Alikwenda kufunga geti. Alipomaliza tukaingia ndani ya nyumba yake.
 
“Shoga asante, acha niende nikatayarishe mambo” nikamuaga shoga yangu kabla ya kutoka kwenda kwangu.
 
Nilifungua mlango wa nyumba nikaingia ndani. Wakati nikiwa jikoni nikitafuta mahali pa kuficha vile vipakiti, nikasikia mlango ukigongwa. Nikaviacha vile vipakiti kwenye mkoba wangu, nikaenda kufungua mlango.
 
Nikashituka kuona alikuwa mgeni. Alikuwa mdogo wake Ibrahim aliyekuwa akikaa Dar. Alikuwa anaitwa Mashaka lakini mwenyewe alijiita meshack.
 
Alikuwa ni mdogo wake Ibrahi shangazi kwa mjomba.
 
“Oh shemeji, karibu sana” nikamkaribisha huku nikipokea begi alilokuwa amelipachika kwenye bega lake.
 
“Asante, habari ya hapa?”
 
“Nzuri, za safari”
 
Baada ya kulipokea begi niliingia nalo ndani.
 
“Nashukuru ni nzuri, sijui nyinyi hapa”
 
Meshack aliingia akafunga mlango.
 
Nikamkaribisha sebuleni lakini begi lake nilikwenda kuliweka kwenye chumba cha wageni.
 
Nilipotoka Meshack aliniuliza.
 
“Kaka yuko wapi?”
 
“Yuko kazini kwake, hapa anarudi jioni sana, si ana taarifa kuwa unakuja?”
 
“Anayo taarifa na leo asubuhi wakati najiandaa kuja huku nilimpigia simu kumjulisha kuwa ninakuja”
 
SASA ENDELEA
 
“Ngoja nimpigie nimjulishe kuwa umeshafika”
 
Nikachukua simu yangu na  kumpigia.
 
“Heloo!” Sauti ya Ibrahim ikasikika kwanye simu.
 
“Shemeji ameshafika” nikamwambia.
 
“Shemeji yupi?” akaniuliza.
 
“Shemeji Mashaka kutoka Dar”
 
“Oh alinipigia simu asubuhi kunijulisha kuwa anakuja lakini nilisahau kukuambia. Amefika sasa hivi”
 
“Ndiyo namkaribisha hapa”
 
“Mwambie ninakuja, tunafunga ofisi”
 
“Sawa”
 
Nikakata simu kisha nikamwambia shemeji.
 
“Anakuja”
 
Kutokana na ule muda aliofika shemeji nilikisia kuwa hakuwa amekula chakula cha mchana, nikaona angalau nikamtayarishie chai ya maziwa imchangamshe hadi usiku.
 
“Shemeji naenda jikoni” nikamuaga na kuondoka kwenda jikoni kumtayarishia chai.
 
Chai ilikuwamo kwenye chupa. Nilichukua slesi tatu za mikate, nilimpakia siagi na kumuandalia kwenye sahani pamoja na kikombe cha chai nikampelekea.
 
“Karibu shemeji” nikamwambia wakati nikimuwekea sahani.
 
“Asante shemeji”
 
Nikakaa kando yake kumzungumzisha huku akiendelea kunywa chai.
 
Alipomaliza kunywa chai alinishukuru. Nikaenda kuiondoa ile sahani na kuirudisha jikoni. Nikarudi tena pale sebuleni. Tuliendelea kuzungumza hadi mume wangu alipotokea. Niliwaacha wakisalimiana nikaingia chumbani.
 
Nilijilaza kitandani na kuanza kuwaza jinsi ya kuifanya ile dawa yangu wakati kulikuwa na mgeni ambaye angekula kile chakula. Isitoshe nisingeweza kufunga bomba na kusingizia maji yamekatika wakati kulikuwa na mgeni huyo.
 
Nilijimbia kama itagundulika kuwa maji yanatoka ispikuwa niliyafunga na kusingizia kuwa maji yamekatika, ningeeleweka vibaya mbele ya mgeni. Ningeonekana kama nimemfungia yeye na kwamba sikuvutiwa na ujio wake.
 
Nikaona nimpigie simu shoga yangu Rita.
 
“Tumepata mgeni” nikamwambia Rita alipopokea simu yangu.
 
“Ni nani?” Rita akaniuliza.
 
“Ni shemeji yangu, ndugu yake mume wangu. Sasa sijui itakuwaje?”
 
“Kwani yeye atakuzuia nini?”
 
“Si ile dawa nilitakiwa niitie kwenye chakula”
 
“Kama nakumbuka vizuri yule mzee alikwambia hata wewe mwenyewe unaweza kula hicho chakula, kwani si kuna huyo mdogo wake mwingine mnayeishi naye. Si pia atakula hicho chakula?”
 
“Sasa kama hilo si tatizo, kuna tatizo jingine. Nikiyafunga yale maji, si nitaonekana nimemfungia mgeni? Si unakumbuka tulikubaliana nisingizie kuwa maji yamekatika ili huyu bwana aoge kwenye ndoo?”
 
“Kwani huyo mgeni atakaa kwa siku ngapi?”
 
“Sijajua bado”
 
“Unaweza kusubiri hadi atakapoondoka”
 
“Naona nachelewa”
 
“Sasa utafanya nini?”
 
“Sina la kufanya, itabidi nisubiri hadi atakapoondoka lakini ndio hivyo moyo waumia”
 
“Subira huvuta heri msichana, acha pupa” Rita akaniambia kwa mzaha. Tukacheka.
 
“Najua kuwa subira huvuta heri lakini ngoja ngoja nayo huumiza matumbo”
 
Wakati nasema hivyo mume wangu akafungua mlango ghafla na kuingia ndani. Nikazuga hapo hapo.
 
“Basi shoga tutaongea baadaye, ngoja nimuhudumie mume wangu ndio amerudi sasa hivi kutoka kazini”
 
Sikungoja jibu lake nikakata simu.
 
“Unazungumza na nani?” Ibrahim aliposikia namsema akaniuliza.
 
“Nazungumza na jirani yangu Rita” nikamwambia huku nikinyanyuka kitandani.
 
“Umempa chakula mgeni?”
 
“Nilimpatia chai tu na slesi tatu, hakukuwa na chakula”
 
“Jioni utapika nini?”
 
“Mh! Sijajua bado. Ulitaka njipike nini?”
 
“Labda ukaange chipsi, viazi si vipo?”
 
“Viazi vipo”
 
“Kaanga chipsi na mayai”
 
Baada ya kuzungumza hivyo na Ibrahim nilitoka mle chumbanni nikaingia jikoni na kuanza kumenya viazi. Mpaka inafika saa mbili usiku, chipsi kwa mayai ya kukaanga zikawa tayari. Ndani ya friji kulikuwa na jagi la juisi ya matunda. Nikaenda nalo mezani.
 
Baada ya kuyayarisha mlo huo nikaenda sebuleni kumuita mume wangu na shemeji zangu.
 
Tulikula pamoja. Baada  ya kula wenzangu waliondoka na kuruidi sebuleni, wakaniacha nikiondoa vyombo.
 
Muda wa kulala ulipowadia nilimuuliza Ibrahim kama mdogo wake aliyekuja kutoka Dar alikuwa amepata likizo kazini kwake.
 
“Sijamuuliza kama alipata likizo” Ibrahim akanijibu.
 
Nikataka nimuulize ataondoka lini lakini niliona swali hilo halikuwa la msingi kumuuliza mume wangu hasa kwa kuzingatia kuwa yule alikuwa ndugu yake.
 
Asubuhi ya siku iliyofuata nilifurahi Ibrahim alipoondoka na mgeni wake. Walikwenda kunywa chai huko huko.
 
Walipoondoka tu nikaenda kwa Rita.
 
Baada ya kusalimiana naye aliniuliza “Vipi?”
 
“Mpango wangu umekwama” nikamwambia huku nikiketi kwenye kochi.
 
“Kwa sababu ya huyo mgeni?”
 
“Na sijui ataondoka lini!”
 
Rita alipoona nimechukia akanicheka na mimi nikajidai kucheka.
 
“Huyo mgeni siku zote haji, anangoja nina mipango yangu ndio anakuja. Si balaa hili!”
 
“Pengine hatakaa sana, ni wasiwasi wako tu”
 
“Kama hatakaa sana ndivyo ninavyotaka”
 
Mgeni huyo alikaa kwetu kwa siku nne. Usiku wa siku hiyo ya nne akaniambia kuwa kesho yake ataondoka kurudi Dar kwani alikuja kutujulia hali tu. Nilifurahi sana aliponiambia hivyo.
 
Asubuhi ya siku iliyofuata Mashaka akaondoka kurudi Dar. Nikaona sasa nitumie ile nafasi kufanya ile dawa yangu. Ilipofika jioni nilijaza maji kwenye ndoo zote na kwenye mabeseni kisha nikaenda kufunga mita ya maji.
 
Mume wangu alipokuja nikatangulia kumwambia kuwa maji yalikuwa yamekatika.
 
“Yamekatika saa ngapi?” akaniuliza.
 
“Hivi jioni”
 
“Sasa tutaoga nini?”
 
“Niliwahi kuchota. Nimejaza ndoo zote”
 
“Oh! Umefanya vizuri sana”
 
Ilipofika usiku yeye alikuwa wa kwanza kwenda kuoga. Aliponiambia nimtayarishie maji, nikaenda kukichukua kipakiti kimoja kati ya vile viwili nilivyopewa na mganga, nikachota ile dawa na kuitia mara tatu kwenye ndoo kama alivyoniagiza yule mganga.
 
ITAENDELEA kesho usikose uhondo huu

No comments:

Post a Comment