Monday, October 10, 2016

HADITHI, YAMENIKUTA SALMA MIE SEHEMU YA 17

HADITHI
 
YAMENIKUTA SALMA MIE 17
 
ILIPOISHIA
 
Alichukua kipande cha kioo kilichovunjika ambacho kilikuwa juu ya meza akakiweka mbele  ya macho yangu.
 
“Hebu jitazame mwenyewe ulivyopendeza” akaniambia  huku akitabasamu.
 
Baada ya kujitazama nikalivua.
 
“Walivulia nini, liache tu”
 
“Niliache la nini, si niko ndani? Hapo nitakapotoka ndio nitavaa” nikamwambia.
 
Nikalivua lile juba na kumpa Konda ambaye alilirudisha ndani ya sanduku.
 
“Sasa ngoja nikutoe nikutambulishe kwa wapangaji wangu. Nina wapangaji wawili humu ndani lakini mwenye mke ni mmoja tu”
 
Tukatoka ukumbini  na Konda. Akawaita ukumbbini wapangaji wake.  Aliyekuja alikuwa mpangaji mmojatu na alitokea uani.
 
“Nimekuita kukutambulisha mke wangu” akamwambia na kuongeza.
 
“Mke wangu mwenyewe ndiye huyu”
 
Yule jamaa alinitazama  kisha akasema.
 
“Nimefurahi kumfahamu” 
 
SASA ENDELEA
 
Nilipoingia ndani nilimkuta mume wangu amekaa sebuleni peke yake. Zacharia hakuwepo.
 
“Habari ya hapa?’ nikamsalimia.
 
“Nzuri, mbona umechelewa sana?”
 
“Nilikwenda huko kwa mama yangu. Kuna mtabibu pale mtaani kwetu amenipa dawa nije nikufanyie”
 
“Dawa gani?”
 
“Dawa ya majani. Ameniambia nikufikichie kwenye macho kwa siku tatu”
 
“Haya tujaribu”
 
“Ameniambia nikufanyie asubuhi na jioni. Asubuhi imeshapita tusubiri jioni tuanze”
 
“Unanifikichia vipi?”
 
Nikamueleza vile nilivyoagizwa na yule mganga.
 
“Haya utanifikichia tujaribu”
 
“Amenihakikishia kuwa itakusaidia”
 
“Lakini haiwashi machoni?”
 
“Hakuniambia lakini nafikiri haiwashi kama inawasha angeniambia”
 
Baada ya hapo niliingia jikoni na kuanza kupika. Ile dawa niliitunza mahali pazuri ambapo ingeweza kukaa bila kukauka.
 
Ilipofika jioni nilichomoa majani matatu ya dawa hiyo nikaenda sebuleni ambako mume wangu alikuwa amekaa nikamwambia alale chini kichalichali ili nimfikichie machoni.
 
Mume wangu aliondoka kwenye kochi alipokuwa ameketi akasogea mbele kidogo na kukaa chini kisha akajilaza kichalichali.
 
Nilichutama  na majani yangu nikayashika na kuyafikicha kabla ya kumkamulia machoni mwake.
 
Maji maji yaliyotoka kwenye  majani hayo yalipomuingia machoni alifumba macho.
 
“Usifumbe macho, yafumbue” nikamwambia. “Yafumbue dawa ikuingie vizuri”
 
Akayafumbua kiuoga.
 
“Fumbua bwana!”
 
“Nimeshayafubua”
 
“Bado, fumbua zaidi”
 
Macho yake yalikwishakuwa maoga. Alishindwa kuyamfumbua sawa sawa.
 
Nikamkamulia majani  hayo hivyo hivyo. Maji maji machache yalimuingia machoni, mengine yalichirizika kingoni mwa macho na kumwagika chini.
 
Nilirudia kumkamulia mara tatu.
 
“Umeshamaliza?” akaniuliza.
 
“Nadhani imetosha”
 
Alikuwa anataka kuinuka nikamzuia.
 
“Ngoja kwanza dawa ikuingie vizuri, una haraka ya nini?”
 
Akatulia.
 
Baada ya dakika tatu hivi nikamwambia ainuke. Akainuka na kukaa kwenye kochi.
 
“Yanawasha?” nikamuuliza.
 
“Yanawasha kwa mbali”
 
Nilichukua kitambaa nikamfuta futa yale maji maji yaliyokuwa yamemchirizikia pembeni mwa macho kisha nikaondoka.
 
Asubuhi nilimfanyia tena,  nikarudia tena jioni.
 
“Vipi, hujaanza kuona ona” nikamuuliza.
 
“Bado. Naona kiza tu”
 
“Mganga mwenyewe ameniambia nikufanyie kwa siku tatu”
 
“Labda mpaka kesho kutwa”
 
Niliendelea kumfanyia Ibrahim dawa hiyo kwa siku tatu lakini macho ya Ibrahim hayakuona chochote. Siku ya nne yake nikarudi tena kwa yule mganga.
 
Nilipomueleza nilimuona akikunja uso.
 
“Bado hajaweza kuona?” akaniuliza.
 
“Hajaona bado”
 
Mganga akafikiri kisha akaniambia.
 
“Njoo kesho nitakupa dawa nyingine”
 
Nikaondoka. Kwa vile hata zile dawa alizopewa  hospitalini hazikuweza kumsaidia, kesho yake nilirudi tena kwa yule mganga. Kwa kweli aliniweka sana. Alipomaliza kuhudumia wateja wake akaniita na kuniambia niende tena kesho kwani hakupata nafasi ya kwenda kunichumia dawa nyingine.
 
Nikaondoka. Siku iliyofuata Ibrahim alipelekwa hospitali na mdogo wake na mimi nikatoka kwenda kwa mganga.
 
Nilipofika alinipa dawa ya ungaunga mweusi, akanimbia nichote kidogo niroweke kwenye maji ya vugu vugu kwa dakika moja kisha nimpe mume wangu anawe uso.
 
“Niroweke kwenye maji ya kiasi gani?” nikamuuliza kwa matumaini.
 
“Kama nusu lita hivi”
 
“Anawe uso yote?”
 
“Ndiyo anawe yote. Unamtilia asubuhi na jioni kidogo kidogo”
 
“Kwa siku ngapi?”
 
“Kwa siku tatu”
 
Baada ya mazungumzo hayo nikaondoka. Nilikuta mume wangu alikuwa amesharudi kutoka hospitali. Alikuwa amepewa dawa nyingine za kutumia kwa siku tatu.
 
“Na mimi nimekwenda kwa mtaalamu mwingine” nikamwambia.
 
“Amekwambiaje?”
 
“Baada ya kumueleza matatizo yako amenipa hii dawa”
 
“Ni dawa ya aina gani?”
 
“Ni ya unga unga. Ameniambia nitie kwenye maji ya vugu vugu kisha uoshe uso asubuhi na  jioni”
 
“Kwa sababu tuna shida tutafanya” Mume wangu aliponiambia hivyo niliona huzuni sana.
 
Tulifanya ile dawa kwa siku tatu bila mafanikio. Zile dawa za hospitali nazo hazikuleta matumaini yoyote.
 
Kwa vile niliona lile tatizo lilitokea kwa yule mganga nikarudi tena bila kuchoka. Mganga akanibadilishia dawa nyingine. Nazo pia hazikufaa.
 
Kwa upande wa hospitalini tulimaliza hospitali kadhaa za macho. Mume wangu aliambiwa hawezi kuona tena!
 
Sasa maisha yetu yalianza kuwa magumu. Mume wangu alikuwa hawezi tena kufanya kazi. Tulikuwa tunakula mtaji. Kusema kweli pesa nyingi zilimalizika kwa uchunguzi na matibabu yake.
 
Mwisho wake akanimabia anafikiria kuuza ile gari yake ili apate pesa za kuendelea kujitibu. Kulikuwa na watu ambao walikuwa wakimpa moyo kwamba asikate tamaa.
 
ITAENDELEA kesho hapahapa usikose





  

No comments:

Post a Comment