Tuesday, October 18, 2016

WANASAYANSI KUUNDA TAIFA ANGA ZA JUU

Wanasayansi kuunda taifa jipya anga za juu

Picha ya chombo cha anga za juu cha AsgardiaKundi la wanasayansi mjini Vienna, Austria wameanzisha mpango wa kuunda taifa la amani la aina yake ambalo litakuwa na jina Asgardia.
Taifa hilo litaundwa katika anga za juu, eneo.
Maelezo kwenye tovuti ya wanasayansi hao yanasema taifa hilo litakuwa nje ya udhibiti wa mataifa yoyote ya sasa na litakuwa katika mzingo wa dunia, eneo ambalo vyombo vya anga za juu huzunguka dunia.
Wanasayansi hao wanapanga kurusha satelaiti ya kwanza, ya kuanzisha taifa hilo, mwishoni mwa mwaka ujao.
Matumaini ya wataalamu hao ni kwamba siku moja hivi karibuni watatambuliwa na Umoja wa Mataifa.
Lakini baadhi ya wataalamu wanatilia shaka uwezekano wa mpango huo kufanikiwa ikizingatiwa kwamba sheria za kimataifa huzuia mataifa kudai umiliki wa maeneo anga za juu.
"Raia" wa Asgardia, ambao watachunguzwa kwa makini kabla ya kukubaliwa, mwishowe watapewa hata pasipoti, anasema Lena de Winne, mmoja wa maafisa wakuu wa mradi huo ambaye alifanya kazi kwa miaka 15 katika Shirika la Anga za Juu la Ulaya (EPA)
Mradi huo unaongozwa na shirika la Aerospace International Research Center, ambalo lilianzishwa na mwanasayansi Mrusi, ambaye pia ni mfanyabiashara, Dkt Igor Ashurbeiyli.
Mashindano yanaandaliwa kuamua bendera na wimbo wa taifa wa nchi hiyo mpya.
Profesa Sa'id Mosteshar, mkurugenzi wa Taasisi ya Sera na Sheria za Anga za Juu ya London, amesema itakuwa vigumu kwa Asgardia kutambuliwa kama taifa ikizingatiwa kwamba haitahusiana na taifa lolote linalojitawala duniani, na pia 'raia wake' wengi watakuwa ardhini.
Tayari zaidi ya watu 50,000 wamewasilisha maombi mtandaoni kutaka kuwa raia wa taifa hilo.

No comments:

Post a Comment