Saturday, October 8, 2016

KOLO TOURE ATOA YA MOYONI

Wenger alinitoa mbali na kunijenga

Kolo Toure, Emmanuel Eboue na Arsene Wenger
Kipindi hiki meneja wa Arsenal Arsene Wenger anapoendelea kusherehekea kutimiza miaka 20 kwenye usukani, mmoja wa wachezaji wake Kolo Toure amezungumza kumhusu.
Toure, kutoka Ivory Coast anasimulia alivyopata fursa ya kujiunga na Arsenal na jinsi nusura mkosi umkoseshe nafasi hiyo alipomwangusha Wenger mazoezini.
"Mara yangu ya kwanza kukutana naye, alikuwa Ivory Coast. Alifika tulipokuwa tukicheza. Kwangu kumuona mara ya kwanza, ulikuwa wakati wa furaha sana.
"Niliamua nilitaka kuchezea Arsenal.
"Sote tulikuwa tunamuona kwenye runinga.
"Nilipojiunga na timu kufanyiwa majaribio, alinivutia sana alivyokuwa anasimamia timu.
Toure alifanyiwa majaribio ya kucheza Arsenal 2002.
"Kwangu kufanya mazoezi na wachezaji nyota kama vile Thierry Henri, Patrick Vieira, Dennis Bergkamp na wengine, nilihisi kama nilikuwa paradiso.
Sikufikiri ningewaona, sasa kuwaona na kufanya mazoezi nao na kuwakaba. Nilikuwa kama mbwa mwenye kichaa. Nilikuwa nakimbiza kila kitu hadi kwenye goli, ghafla nilijipata namkabili meneja, ambaye alikuwa Bw Wenger. Nilidhani alikuwa anacheza. Lakini hakuwa anacheza, alikuwa nje.
"Nilikuwa na hamu ya kuonyesha kwamba ningeweza kuchezea klabu hii kubwa Arsenal.
"Nadhani alishangaa sana, najua hakutarajia kwani maishani mwake labda ilikuwa wakati wake wa kwanza kuangushwa na mchezaji.
"Lakini alijua sikuwa nimekamilisha kutia saini mkataba. Alienda chumbani na alikuwa anacheka, kila mtu alikuwa anacheka, anamcheka.
"Nilipoingia chumbani, nilipata amewekewa barafu mguuni, nikajua mambo kwisha. Nitarejea kwetu nyumbani kwani hatanichukua.
"Kwangu, yeye (Wenger) ni mmoja wa mameneja wanaowachukua wachezaji wenye vipaji na kuwafanya kuwa wachezaji nyota.
Kuna mifano mingi, Vieira kutoka AC Milan, Anelka kutoka PSG, George Weah kutoka Monaco.
"Alitoa mbali, na akanifanya kuwa mchezaji niliye sasa. Alimchukua pia Adebayor (wa Togo) na kumjenga."

Kikosi hatari

Beki huyo, ambaye amechezea taifa lake mechi 118 alijiunga na Arsenal 2002 na akawa sehemu ya kikosi maarufu cha "Invincibles" ambacho hakikushindwa hata mechi moja Ligi ya Premia msimu wa 2003-04.
Alijiunga na Manchester City kwa £14m mwaka 2009, na kushinda taji jingine la Ligi ya Premia mwaka 2012.
Alihamia Liverpool mwaka 2013. Alijiunga na Celtic ya Scotland mwaka huu.

No comments:

Post a Comment