Monday, May 30, 2016

HADITHI MWANAMKE SEHEMU YA 6

SIMULIZI A FAKI A FAKI 0713

MWANAMKE 6

ILIPOISHIA

“Mzee samahani, naomba msaada wako” nikamwambia.

“Msaada gani?”

“Mimi sijui nilivyofika hapa, ninaomba unioneshe njia ya kutoka nje”

“Unasema hujui ulivyofika hapa?”

“Sijui, nimejiona tu nikitokea katika nyumba hii”

“Kwani unatoka wapi?”

“Ninatoka katika nyumba ya msichana mmoja ambaye nilimuazima kitabu changu, wakati ule natoka  nikaona nimetokea kwenye pango. Baadaye tena naona nimetokea kwenye nyumba hii”

“Wakati unatoka ulimuaga mwenyeji wako?”

“Sikumuaga”

“Kwanini hukumuaga?”

Hapo nikanyamaza kimya, sikuwa na jibu. Nilishindwa kumueleza niliyoyaona kwa sababu yule mzee naye sikujua alikuwa ni nani.

Pakapita kimya cha sekunde kadhaa. Yule mzee alikuwa akinitazama akisubiri jibu langu na mimi nilikuwa nikimtazama uso wangu ukiwa umenywea ukionesha sikuwa na jibu.

“Ulifanya kosa kutomuaga mwenyeji wako na ndio sababu unahangaika. Siku nyingine usirudie kosa kama hilo” Yule mzee akaniambia.

SASA ENDELEA

Akanyamaza kimya kisha akanimabia.

“Mlango huu hapa, nenda zako”

Alinionesha mlango uliokuwa ubavuni kwake.

“Asante sana, nashukuru” nikamwambia huku nikivuta hatua kuelekea kwenye mlango huo.

Mzee alikuwa akinitazama.

Niliufungua ule mlango nikatazama nje na kutoka. Nilipotoka nikajiona niko nje ya nyumba ya Zena! Jambo hilo lilinipa mshangao lakini nilishukuru nikaanza kutoka mbio nikiwa pekupeku. Sikukumbuka tena ile pikipiki yangu.

Nilikimbia kwa miguu nikiwa peke yangu usiku ule katika njia iliyokuwa na vichaka vinavyotisha. Vivuli  vya miti  iliyokuwa ikitikiswa na upepo vilizidi kunitisha lakini sikuwa na la kufanya, nilikuwa nimeshajitolea.

Baada ya nusu saa nikawa nimefika kwenye barabara ya lami nikakata kushoto na kuendelea kukimbia. Nilipokuwa ninakikaribia kituo cha polisi cha Mabawa nikaanza kuchoka. Nguvu zilikuwa zimeniishia kabisa.

Nilisimama huku nikitweta. Nikatazama nyuma. Kulikuwa kimya. Kile kituo cha polisi kilinipa matumaini nikaanza kutembea taratibu. Nilikipita kituo hicho nikaendelea kutembea hadi nikafika nyumbani kwangu.

Nilifungua mlango nikaingia nyumbani kwangu. Mwili wote ulikuwa unaniuma. Shati langu lilikuwa limeloa kwa jasho. Nilivua nguo nikaenda kuoga. Niliporudi chumbani kwangu nikasikia dirisha langu linagongwa.

Nilikuwa nimeshazima taa na kupanda kitandani. Nikatega masikio yangu kusikiliza. Dirisha liliendelea kugongwa.

“Amour! Amour!” Sauti ya kiume ikawa inaita jina langu.

Nilijaribu kuifikiria ilikuwa sauti ya nani lakini sikuweza kutambua ilikuwa sauti ya nani miongoni mwa watu niliokuwa nawafahamu. Nikaamua kunyamaza kimya.

Sauti ile ikaendela.

“Amour fungua mlango nimekuletea viatu vyako na funguo za pikipiki yako”

Nilishituka niliposikia maneno yale nikajua mtu aliyekuwa akiniita alitoka kule kwa Zena ambako niliacha pikipiki yangu na viatu vyangu.

Nikajiambia kwa vyovyote vile atakuwa si mtu bali ni jini. Hofu yangu ilianzaa tena upya. Moyo ukaanza kunienda mbio.

Dirisha liliendelea kugongwa na ile sauti ikaendelea kuniambia nifungue mlango nichukue viatu vyangu pamoja na funguo za pikipiki yangu niliyoiacha kwa Zena.

Sikujibu chochote, nikaendelea kubaki kimya.

Baada ya muda kidogo ile sauti ikapotea, kukawa kimya. Nikasubiri kuona kama kutatokea kitu chochote, sikuona kitu. Nikaendelea kuwa macho huku hofu ikiwa imenitawala hadi nikapitiwa na usingizi.

 Nilichelewa sana kuamka asubuhi. Nilishukuru kuwa ilikuwa ni jumapili siku ambayo ni ya mapumziko, vinginevyo ningechelewa kufika kazini.

Mara tu niliposhuka kitandani nilitazama saa. Ilikuwa saa mbili na robo. Nikatoka nje nikiwa nimejifunga taulo. Wakati nafungua mlango wa mbele nikaona viatu vyangu nilivyoviacha kwa yule msichana, vimewekwa mbele ya mlango wangu pamoja na funguo za pikipiki yangu. Nikashituka.

Wakati huo mpangaji mwenzangu wa upande wa pili alikuwa anatoa pikipiki yake. Nikamuita.

“Alphonce!”

Alphonce akanifuata na kunisalimia.

“Kuna tatizo limenitokea” nikamwambia.

“Tatizo gani?” akaniuliza.

“Unaviona hivi viatu?”

“Ninaviona”

“Sasa njoo ndani nikueleze mkasa ulionitokea jana usiku”

Alphone akiwa amepatwa na mshangao aliigesha pikipiki yake karibu na mlango wangu akaingia ndani. Nilimkaribisha sebuleni kwangu. Vile viatu na funguo za pikipiki yangu nilikuwa nimeviondoa pale mlangoni.

“Haya nieleze kuna nini?” Alphonce akaniuliza.

Nikamueleza ule mkasa ulionitokea usiku uliopita uliosababisha nirudi nyumbani kwangu usiku nikiwa pekupeku.

“Wakati nimerudi niko chumbani kwangu, nikasikia sauti ya mtu kwenye dirisha akiniambia ameniletea viatu vyngu na funguo za pikipiki. Kwa kweli sikumjibu. Nilinyamaza kimya”

Wakati ninamueleza Alphonce alikuwa ameshangaa kweli kweli.

“Halafu ikawaje?” akaniuliza.

“Baada ya kunyamaza kimya ile sauti sikuisikia tena, sasa hii leo asubuhi nafungua mlango nakuta viatu vyangu na funguo za pikipiki yangu vimewekwa mbele ya mlango wangu”

“Una maana yule mwanamke alikuwa ni jini?”

“Alikuwa jini”

“Na huyo aliyekuletea hivyo viatu na funguo ni nani?”

“Sijui, lakini watakuwa ni wamoja”

“Unajua mimi huwa nazisikia habari za majini lakini siamini kama kuna viumbe hao. Unaonaje kama tutakwenda mimi na wewe kwenye hiyo nyumba?’

“Mimi nilikuwa nimepanga kwenda polisi kwa sababu ya pikipiki yangu”

“Twende huko Mikanjuni kwanza, kama pikipiki yako hutaipata ndio utakwenda polisi kwa ajili ya kupata msaada zaidi”

“Sawa. Subiri nivae tutoke”

“Nitakusubiri”

Nikanyanyuka na kuingia chumbani kwangu. Baada ya nusu saa nikatoka nikiwa nimeshavaa.

“Twende” nikamwambia Alphonce.

Tukatoka. Alphonce alinipakia kwenye pikipiki yake tukaelekea Mikanjuni. Nilimuelekeza mahali ilikokuwa ile nyumba ya yule msichana, tukaenda hadi mahali hapo lakini jambo la ajabu lililotokea ni kuwa ile nyumba hatukuiona. Badala yake tuliona eneo lote lilikuwa makaburi matupu ya watu wa zamani.

Nikapatwa na mshangao. Wakati naangalia angalia nikaiona pikipiki yangu ikiwa kando ya mti. Mti huo ndio ule uliokuwa uani mwa nyumba ya Zena. Kando yake palikuwa na kisima ambacho yule msichana na mwenzake walikuwa wakioga.

Wakati ule kile kisima hakukuwepo tena, badala yake tuliona dimbwinl maji ya mvua.

“Pikipiki yangu ile pale!” nikamwambia Alphonce ambaye naye alikuwa ameshangaa.

“Sasa mbona iko kwenye makaburi na hapana nyumba?” akaniuliza.

“Na mimi ndio nashangaa. Ile pikipiki niliiweka uani mwa hiyo nyumba niliyokwambia. Ule mti unaouona ulikuwa uani na lile dimbwi la maji kilikuwa ni kisima”

“Hebu twende pale karibu”


JE WAKIFIKA HAPO KARIBU WATAONA NINI? HUU NI MKASA WA KUSISIMUA SANA AMBAO WEWE MSOMAJI WA BLOGY HII HUTAKIWI KUUKOSA. SASA ANZA KAWAIDA YA KUTEMBELEA BLOG HII KILA SIKU BILA KUKOSA NA MWAMBIE NA MWENZAKO USIFAIDI PEKE YAKO. Kila mnapokuwa wengi ndio mimi hufurahi.

No comments:

Post a Comment