Tuesday, April 11, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU, SEHEMU YA 9

ZULIA LA FAKI,0655 340572
 
NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 9
ILIPOISHIA
 
Ndege ilipaa hewani kwa takribani saa sita kabla ya kutua katika kiwanja cha ndege cha Dar es Salaam.
 
Ndege ilipotua, abiria walianza kushuka. Nilikuwa miongoni mwa abiria wa mwisho mwisho. Nilikuwa nimechoka na nilionesha wazi kukata tamaa.
 
Wakati namalizia kushuka ngazi ya ndege, macho yangu yalimuona mtu aliyenishitua akiwa mbele yangu.
 
Alikuwa ni yule msichana muuaji! Alikuwa miongoni mwa abiria waliokuwa wamepanda ile ndege wakitokea Afrika Kusini. Alikuwa amefuatana na mwanamme mmoja aliyekuwa amevaa suti nyeusi wakizungumza.
 
Kusema kweli sikutambua kama yule msichana alikuwemo ndani ya  ndege ile. Nilimgundua wakati ule wa kushuka. Yule mtu aliyekuwa amefuatana  naye sikuweza kumtambua.
 
Tulipotoka nje ya jengo la kiwanja cha ndege, msichana huyo pamoja na yule mtu aliyekuwa amefuatana naye walikodi teksi na kuondoka. Na mimi nikakodi teksi na kumwambia dereva awafuate.
 
SASA ENDELEA
 
“Una maana niifuate hii teksi ya mbele yangu?” Dereva wa teksi akaniuliza.
 
“Ndiyo ifuate hiyo hiyo”
 
“Inaelekea wapi?”
 
“Popote itakapoelekea”
 
“Ina maana wewe hujui inaeleka wapi?”
 
“Kwani tatizo lako ni nini, hapo tutakapofika utanitoza kiasi utakachotaka”
 
“Sawa. Nilitaka tupatane tu”
 
“Hatuwezi kupatana kwa sababu sijui wanakwenda wapi”
 
“ Nimekuelewa”
 
Dereva wa teksi akaanza kuiandama teksi iliyokuwa mbele yetu. Wakati mwingine gari lilitinga katikati yetu lakini dereva alijitahidi kuhakikisha teksi hiyo haitupotei.
 
Wakati tunaendelea kuiandama teksi hiyo, mawazo yangu yalikuwa kwa yule msichana. Bado nilikuwa nikijiuliza msichana yule ni nani na kwanini nakutana naye katika kila nchi ninayokwenda. Pia nilijiuliza yule mtu aliyenaye ni nani na anatoka wapi.
 
Nilihisi kwamba kwa vile msichana huyo alikuwa katika jiji ambalo nilikuwa nikilijua vyema, ningeweza kufanya uchunguzi na kumgundua.
 
Hata hivyo jambo moja nilikuwa na uhakika nalo moyoni mwangu kwamba msichana huyo alikuwa wa hatari na muuaji aliyeonekana kuwa na uzoevu wa kuua.
 
Mara moja niligundua kuwa teksi iliyowapakia ilikuwa ikielekea Mbezi. Tuliendelea kuifuata hadi iliposimama mbele ya jumba moja la kifahari. Dreva wa teksi niliyopanda alitaka kusimama nikamwambia apitilize moja kwa moja.
 
“Sitaki wagundue kuwa ninawafuata” nikamwambia dereva huyo na kuongeza.
 
“Utasimama kule mbele”
 
“Nimekuelewa”
 
Wakati teksi ikiendelea kwenda, mimi nilikuwa nikitazama nyuma kwenye kioo. Nilimuona yule msichana akishuka kwenye ile teksi pamoja na yule mwanaume aliyekuwa naye. Teksi iliondoka na wao wakafungua geti na kuingia ndani.
 
Kwa vile nilikuwa nimeshaikariri ile nyumba, nilimwambia dereva wa teksi ageuze anipeleke nyumbani kwangu.
 
“Umeshawaona?” akaniulia wakati akiigeuza teksi.
 
“Nimewaona. Nilitaka kujua wanaishi wapi?”
 
“Kwani ni kina nani wale?”
 
“Nilisafiri nao kutoka Afrika Kusini. Nilitaka kujua wanaishi wapi hapa dar”
 
Dereva alitaka kuendelea kuniuliza  lakini alibadili mawazo akanyamaza kimya.
 
Baada ya nusu saa tu alinifikisha katika mtaa ninaoishi. Aliisimamisha teksi mbele ya nyumba yangu nikamuuliza gharama yake ni kiasi gani.
 
Alinitajia kiasi alichotaka nikatoa pochi yangu na kumpa kiasi hicho bila kusita.
 
“Asante sana” nilimwambia huku nikifungua mlango wa teksi na kushuka.
 
Huku nikiwa na begi langu nilikwenda kufungua mlango wa nyumba yangu nikaingia ndani. Niliondoka kwenda nje ya nchi kwa matumaini ya utajiri lakini nimerudi kama masikini. Safari yangu haikuwa na mafanikio yoyote, nilijiambia kwa huzuni.
 
Mbali ya kutokuwa  na mafanikio, ilikuwa safari ya balaa na iliyonitia hofu kutokana na wale watu niliowafuata kuuawa mmoja baada ya mwingine, tena wameuawa na msichana huyo huyo ambaye aliwafuata Botswana, Zimbabwe na Afrika Kusini.
 
Msichana yule sasa amekuwa ni kitendawili ambacho nilihitaji kukitegeua kadiri itakavyowezekana. Kwa vile nilikuwa nimeikariri sura yake pamoja na nyumba aliyoingia, niliamini kwamba ningewea kumfuatilia na kumjua vizuri.
 
Siku ile ikapita. Asubuhi ya siku iliyofuata wakati nimeketi sebuleni nikitazama televisheni, niliona kitu kilichonishitua.
 
Kilikuwa ni kipinidi cha taarifa ya habari. Habari ya kwanza kutangazwa na kuoneshwa ilikuwa ya mauaji ya mkazi mmoja wa Mbezi aliyetajwa kwa jina la Abdul Baraka.
 
Hilo jina lilinishitua kwa sababu lilikuwa katika orodha ya wale wadaiwa wa marehemu babu yangu. Jina hilo lilikuwa la kwanza na mtu huyo ndiye niliyeanza kumpigia simu lakini simu yake haikupatikana nikaamua nimuache kiporo.
 
Yeye hasa ndiye aliyekuwa tegemeo langu baada ya wale watu niliowafuata nje ya nchi kuuawa na kusababisha nisipate kitu.
 
Taarifa hiyo ya televisheni ilieleza kwamba mwili wa Abdul Baraka ulikutwa mchana wa jana yake nyumbani kwake ukiwa umelazwa sebuleni.
 
 
ITAENDELEA

No comments:

Post a Comment