Sunday, April 9, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 7

ZULIA LA FAKI, 0655 340572
 
NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 7
 
ILIPOISHIA
 
Walipoona uso wangu ulikuwa umeota alama ya kuuliza waliniambia.
 
“Tulitaka  kukuchangamsha tu mgeni wetu. Tunaona umekuwa kimya chumbani, huna mwenzako”
 
Hapo ndipo nilipoelewa kuwa wale walikuwa changu doa waliokuwa wakijiuza kwenye mahoteli.
 
Mawazo yangu yalikuwa tofauti na wao kwa upande mmoja na yalikuwa yanalingana na wao kwa upande mwingine.
 
Yalikuwa tofauti na wao kwa upande mmoja kwa sababu kilichonipeleka Botswana hakikuwa kufuata machangudoa na yalilingana na wao kwa upande mwingine kwa sababu wao walikuwa wakitafuta pesa kwa njia zao na mimi vile vile nilikuwa natafuta pesa.
 
Nilipowaza hivyo nilijikuta nikitabasamu.
 
“Karibuni” nikawambia huku nikijiambia mwenyewe kuwa si vibaya kuzungumza nao mawili matatu kupitisha wakati.
 
Wasichana hao wakaingia mle chumbani.
 
SASA ENDELEA
 
Wote wawili walikimbilia kukaa kitandani wakaniwekea nafasi nikae katikati yao. Nikakaa.
 
“Kwanini unataka kulala peke yako wakati sisi tupo?” Msichana mmoja aliyeonekana kuwa na macho ya juu aliniuliza.
 
“Nimekuja peke yangu, nitalala peke yangu. Mlitaka nilale na nani?” nikamjibu.
 
“Uchague mmojawapo kati yetu sisi” Msichana wa pili akaniambia.
 
Kusema kweli hawakuwa malaya wa kuweza kunishawishi. Mkorogo ulikuwa umewaharibu. Lakini nilitaka kuzungumza nao tu nichangamshe akili yangu.
 
“Je kama nitawachagua nyote itakuwaje?’ nikawauliza huku nikiwatazama kwa zamu.
 
“Utatuweza?” Mmojawapo akaniuliza.
 
“Nisiwaweze kwani nyie ni vyuma?”
 
“Sawa. Utatupa dola ngapi?”
 
“Tatizo litakuwa hapo kwenye dola”
\
“Utatupa dola ngapi?”
 
“Sina hata dola moja”
 
“Si kweli. Huoneshi kuwa huna pesa, usingekaa katika hoteli hii”
 
“Kwani unatokea wapi?” Msichana mwingine akaniuliza.
 
“Natokea Zimbabwe”
 
“Wewe ni Mzimbabwe?”
 
“Hapana. Mimi ni Mbongo”
 
Wasichana hao wakaonesha kushituka.
 
“Mbongo ni mtu wa nchi gani?”
 
“Mtanzania”
 
“Kumbe unatoka Tananzia?”
 
“Unakufahamu?”
 
“Sijafika lakini tumefundishwa shuleni kwamba Tanzani ilikuwa moja ya nchi zilizokuwa mstari wa mbele kupigania uhuru wa Afrika ikiwemo nchi yetu chini ya uongozi wa Mwalimu Nyerere”
 
“Sasa kama mnajua hivyo kwanini mnanitoza dola?”
 
“Ulitaka bure?”
 
“Ikiwezekana”
 
Wasichana hao walicheka kisha wakainuka na kusimama. Bila shaka waligundua kuwa nilikuwa nikiwapotezea wakati wao  bure.
 
“Mbona mnakwenda zenu?” nikawauliza.
 
“Sisi tuko kazini bwana. Hamna bure hapa. Wewe hutaki kutoa pesa yako. Kwaheri” Msichana mmoja akanniambia.
 
Walitoka na kuniacha. Na mimi niliinuka nikafunga mlango wangu kisha nikarudi kitandani.
 
Siku ile ikapita nikiwa hapo hoteli.
 
Asubuhi ya siku iliyofuata nikiwa kwenye mkahawa wa hoteli hiyo nikipata kifungua kinywa, nilimuona dereva wa mwenyeji wangu Muhoza akinifuata. Uso wake ulikuwa umetaharuki.
 
Akanisalimia kisha akaniambia.
 
“Bwana Muhoza ameuawa!”
 
Mshituko ulinifanya niinuke kwenye kiti na kusimama.
 
“Bwana muhoza ameeuawa?” nikamuuliza kwa mshangao.
 
“Jana alipoondoka hapa alikwenda katika hoteli nyingine ambako alilala na yule msichana aliyekuwa naye. Aliniambia nimfuate asubuhi. Asubuhi nilipomfuata nikakuta taarifa hiyo. Maiti yake ilikutwa chumbani hii asubuhi”
 
Nikajiambia, ni yale yale yaliyotokea Botswana.
 
“Kwani yule msichana aliyekuwa naye ni nani?” nikamuuliza yule dereva.
 
Dereva huyo akabetua mabega yake.
 
“Simfahamu na sijui walikutana wapi”
 
“Yule ndiye aliyehusika na mauaji hayo!”
 
“Inaaminika hivyo kwa sababu amekimbia”
 
“Hebu kaa nikueleze kitu” nikamwambia Yule mtu huku na mimi nikikaa.
 
“Unajua mimi natokea Botswana. Yule msichana nilimkuta katika hoteli niliyofikia pale Botswana. Baadaye nilimuona akiwa na mwenyeji wangu na wakachukua chumba pale pale hoteli. Asubuhi yake mwenyeji wangu akakutwa ameuawa katika chumba cha hoteli na yule msichana hakuonekana. Sasa nilipofika hapa Zimbabwe nilishangaa kumuona tena akiwa na Muhoza” nikamueleza yule mtu.
 
“Kwanini hukutuambia tangu jana?”
 
“Nilishindwa kuwambia, nilijua labda wanajuana”
 
“Sasa yule msichana atakuwa ni nani na anatokea wapi?”
 
Nikaguna na kushusha pumzi ndefu.
 
“Hicho ni kitendawili na sidhani kama atapatikana”
 
“Anaweza kupatikana”
 
“Nilikuwa namdai Muhoza pesa nyingi na tulikubaliana kwamba angenilipa hii asubuhi. Sasa sijui nitafanyaje?”
 
“Huyu jamaa kama ulikuwa na mipango naye ya pesa ni bora usamehe. Kwanza mimi siwajui ndugu zake na isitoshe alishatengana na mke wake miaka mingi iliyopita”
 
Nikatikisa kichwa change kusikitika.
 
“Mkosi gani huu jamani…!” nilijisemea kimoyomoyo.
 
ITAENDELEA kesho hapa hapa Usikose Uhondo huu nini kitatokea baada ya Mahoza nae kuuwawa na wasichana wale kuondoka, je watarudi na jamaa nini atafanya au kumkuta akiwa hotelini
 
 
 

No comments:

Post a Comment