Monday, April 3, 2017

SIMULIZI , NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 4

SIMULIZI na Faki A Faki, 0655 340572
 
NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 4
 
ILIPOISHIA
 
“Ninaongea na wewe nikiwa chumbani”
 
“Sawa. Kama utahitaji chakula au kinywaji chochote agiza tu, nimeweka oda kwa ajili yako”
 
“Sawa”
 
“Nitakuja kuonana na wewe baada ya dakika chache”
 
“Nakusubiri”
 
Baada ya hapo kukawa kimya. Nikaurudisha mkono wa simu kisha nikatoka humo chumbani. Nilifunga mlango kwa funguo nikashuka chini.
 
Unaposhuka chini unatokea pale mapokezi, nikaenda kukaa kwenye meza moja katika ule ukumbi. Yule msichana niliyemuona ameketi nilipoingia alikuwa bado ameketi akisoma gazeti.
 
Nilikuwa nimevutiwa na umbile lake la kupendeza na sura yake jamali.
 
Lakini laiti kama ningetambua tukio ambalo lingetokea hapo hoteli ningeahirisha mapema safari yangu!
 
SASA ENDELEA
 
Baada ya kuketi mhudumu alikuja kuniuliza kama nilikuwa nahitaji kitu, akanipa menyu.
 
Kwenye menyu niliona ugali kwa samaki. Nikatamani kula ugali wa Kizimbabwe. Nikamuagiza mhudumu huyo aniletee ugali kwa samaki.
 
Wakati nasubiri nilitewe ugali nilioagiza, nilimuona mtu mmoja aliyekuwa amevaa suti nyeusi akiingia hapo hoteli. Alipomuona yule msichana aliyekuwa amekaa karibu na mlango alisita kisha akavuta kiti na kuketi naye. Nikaona wanazunguma ingawa sikuweza kusikia walikuwa wanazungumza nini.
 
Mhudumu alimfuata yule mtu, nikaona anaagiza kitu. Baadaye kidogo waliletewa chupa mbili za bia na kuanza kunywa. Mimi nilikuwa nimeshaletewa chakula nilichoagiza.
 
Nilikuwa nikila ugali huku jicho langu likiwa kwa wale watu. Kama sijakosea walikunywa bia mbili mbili. Mimi nilikuwa nimeshamaliza ugali wangu wakati yule mtu alipoinuka na kwenda mapokezi. Alizungumza na mhudumu wa mapokeziki kabla ya kupewa funguo.
 
Baada ya kupewa funguo alirudi kwa yule msichana akazunguma naye akiwa amesimama. Baada ya muda kidogo msichana aliinuka wakaenda kupanda ngazi.
 
Nilihisi kama vile yule mtu alikuwa amechukua chumba na alikuwa akielekea chumbani na yule msichana. Huenda walikuwa wakijuana na kwamba yule msichana alikuwa akimsubiri yule jamaa pale.
 
Niliendelea kuketi pale pale nikiangalia televisheni iliyokuwa imepachikwa katika ukuta. Nilipoona muda unazidi kwenda niliondoka nikarudi chumbani kwangu na kumpigia simu mwenyeji wangu.
 
Nilitaka kumuuliza mbona hatokei kwani muda mrefu ulikuwa umepita tangu aliponiahidi kuwa anakuja. Simu ikaita kwa muda mrefu bila kupokelewa.
 
Simu ilipokata nikapiga tena lakini pia haikupokelewa. Nikaamua kusubiri kabla ya kupiga tena.
 
Kwa vile sikuwa na kingine cha kufanya, niliona nijilaze pale kitandani. Bila kujitambua usingizi ukanipitia hapo hapo.
 
Nilipozinduka ilikuwa usiku. Niliwasha taa kisha nikatazama saa. Ilikuwa saa mbili na robo usiku. Nikapiga tena simu lakini bado simu ilikuwa ikiita tu bila kupokelewa.
 
Nikawa nimechukia. Nilihisi huyo mtu aliyefanya niende Zimbabwe hakuwa na ahadi za kweli. Nikaenda kuoga. Niliporudi nilipiga simu tena. Nilipiga mara tatu bila kupokelewa. Simu ilikuwa inaita tu.
 
Nikashuka chini na kula chakula kisha nikarudi tena juu. Nikapiga tena simu lakini haikupokelewa. Ilikuwa kama vile simu ilikuwa peke yake au mwenye simu aliamua kunisusia.
 
Kusema kweli nilichanganyikiwa. Nilikuwa sijui la kufanya. Nikalala. Asubuhi nilipoamka kitu cha kwanza kilikuwa kupiga simu. Simu ya Chusama bado ilikuwa ikiendelea kuita tu. Sasa nikaanza kupatwa na wasiwasi.
 
Nikashuka chini na kupata kifungua kinywa. Wakati naendelea kunywa chai. Nilisikia nung’unung’u hapo hoteli kuwa kuna mtu aliyeuawa akiwa ndani ya chumba cha hoteli.
 
Tukio hilo liligunduliwa na mhudumu wa usafi ambaye aliingia katika chumba hicho na kukuta maiti ya mwanaume iliyokuwa imelazwa chini.
 
Baadaye polisi walifika hapo hoteli. Waliongozwa na baadhi ya wafanyakazi wa hoteli hiyo kuelekea katika chumba hicho kilichokuwa ghorofa ya kwanza. Na mimi kwa kutaka kupata ukweli niliinuka nilipokuwa nimeketi nikaelekea huko huko.
 
Kilikuwa chumba kilichopakana na chumba nilicholala mimi. Mlango ulikuwa umeachwa wazi na polisi pamoja na baadhi ya wafanyakazi walikuwa wameingia ndani.
 
Sikuweza kumuona  vizuri mtu huyo mpaka mwili wake ulipokuwa unatolewa ukiwa kwenye machela. Nilipomuona tu nikamtambua. Alikuwa ni yule mtu ambaye alifika jana yake pale hoteli na kuzungumza na yule msichana na kisha wakaondoka pamoja kuelekea chumbani.
 
Hata hivyo yule msichana aliyekuwa naye hakuwepo. Ilisemekana kwamba alitoroka kabla ya tukio hilo kugundulika.
 
Mpaka mwili wa mtu huyo unatolewa, polisi hawakuwa wamegundua mtu huyo alikuwa ameuawa kwa kitu gani. Kwenye pua yake na kwenye pembe moja ya midomo yake kulikuwa na michirizi ya damu iliyoganda.
 
Kulikuwa na baadhi ya wafanyakazi ambao walichukuliwa na polisi kwenda kutoa maelezo.
 
Nikajiuliza kama yule mwanamke alikuwa muuaji kweli. Hakuonekana kuwa katili. Niseme ukweli kama ndiye aliyemuua yule mtu, tukio lile lingenikuta mimi kwani jana yake ilibaki kidogo niende nikakae naye.
 
Nikashukuru kwamba Mungu alikuwa ameninusuru.
 
Ingawa tukio hilo lilichnaganya akili yangu lakini kitendo cha mwenyeji wangu kutopokea simu kilinichanganya zaidi. Niliingia chumbani na kutafakari nifanye nini. Kwa kweli sikupata jibu.
 
ITAENDELEA kesho Usikose Uhondo huu nini kitatokea  ni hapahapa tangakumekuchablog
 

No comments:

Post a Comment