Thursday, April 27, 2017

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMUA 14

ZULIA LA FAKI, 0655 340572
 
NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 14
 
ILIPOISHIA
 
“Sasa  mwanangu, huyu msichana uliyekuja kutueleza kwamba ulikutana naye na kuzungumza naye alishakufa na mdogo  wake amethibitisha kwamba namba ya simu uliyopigiwa ni ya marehemu kweli, je mpaka sasa una wazo gani?” Yule mama akaniuliza lakini swali lake lilikuwa ni gumu kulijibu.
 
“Sijui nikujibu nini mama yangu. Hiyo taarifa kwamba huyu msichna alikufa  miaka mitano iliyopita imenichanganya akili yangu” nikamjibu.
 
“Kwani alipokupigia simu alikueleza alikuwa na uhusiano gani na babu yako?” Yule mzee naye akaniuliza.
 
“Hakuniambia kama alikuwa na  uuhusiano wowote na babu yangu isipokuwa aliniambia alitaka anipe taarifa za mali ya babu yangu”
 
“Na mimi nina  wazo langu” Yule msichana  naye akasema na kuongeza.
 
“Hebu mpigie simu hapa hapa tumsikie”
 
“Hilo ni wazo zuri” nikasema na kuitazama simu yangu ambayo nilikuwa nayo mkononi.
 
Nikampigia Ummy Sharif Nasri.
 
SASA ENDELEA
 
Simu ilikuwa inaita lakini ilikuwa haipokelewi.
 
“Simu inaita lakini haipokelewi” nikawambia.
 
Niliiondoa simu sikioni mwangu na kuielekeza kwa yule msichana.
 
“Sikiliza simu inaita” nikamwambia.
 
Msichana aliishika  ile simu  akaiweka kwenye sikio lake na kusikiliza.
 
“Ndiyo simu inaita kweli” akasema.
 
Aliendelea kuiweka sikioni kwake hadi simu ikakata yenyewe. Akaiondoa sikioni  na kunipa.
 
“Simu inaita  lakini hapokei” akasema tena.
 
“Una  maana kwamba Ummy yuko hai?” Mama yake akamuuuliza.
 
Msichana akabetua mabega.
 
“Tunachojua sisi ni kuwa amekufa, sasa hii habari kuwa dada yuko hai hatuijui. Kama angekuwa hai si angekuja  nyumbani”
 
“Ni miujiza hii!” Mzee akasema huku uso wake ukiwa umefadhaika.
 
“Hebu piga  tena” Yule mama akaniambia.
 
Nikapiga  tena ile  namba.
 
Safari hii simu  haikupatikana.
 
“Inaita” Mama akaniuliza.
 
“Simu  haipatikani tena” nikawambia.
 
“Mara moja hii!” Mama akashangaa.
 
“Inawezekana ameizima” nikawambia.
 
“Huyo Ummy ndiyo ameizima?”
 
“Ndiyo  yeye. Mnaponiambia kuwa amekufa niinashangaa kwa sababu nimemuona  na nimezungumza naye”
 
“Huyu huyu ambaye umemuona  kwenye picha?”
 
“Ndiye huyo  huyo”
 
“Sasa ili uamini kuwa amekufa twende nikakuoneshe  kaburi lake. Makaburi hayako mbali” Mzee akaniambia.
 
Mzee huyo alinichukua hadi katika  eneo la makaburi ambalo halikuwa mbali sana. Akanionesha kaburi la Ummy Nasri. Lilikuwa na kibao kilichoandikwa jina lake, tarehe aliyokufa na aliyozikwa.
 
“Kaburi lake ni hili hapa”
 
Sikuwa hata na la kusema. Nilibaki kushangaa tu.
 
Mzee aliendelea kuniambia.
 
“Marehemu amelala ndani”
 
“Sasa mzee huyu atakuwa nani?” nikamuuliza.
 
“Sisi hatumjui. Sisi tunachojua ni kuwa binti yetu alishakufa na aliyekufa hafufuki”
 
“Lakini mzee fikiria kwamba alinielekeza yeye mwenyewe kuwa nije pale nyumbani nimuulizie”
 
“Mtu yeyote hawezi kukubaliana  na maelezo yako” Mzee akaniambia huku akiondoka.
 
“Nimekuja kukuonesha hili kaburi ili uthibitishe kuwa Ummy alikwishakufa” akaongeza.
 
“Na mimi nathibitisha kuwa nilimuona”
 
“Basi itakuwa ni miujiza mikubwa”
 
Tukarudi pale nyumbani.
 
“Ni vizuri kama utakutana naye tena uje naye hapa mguu kwa mguu” Mzee akaniambia wakati akiketi kwenye kiti chake  cha uvivu.
 
Wakati narudi na gari langu nilianza kuzikumbuka  zile safari za kimiujiza za yule msichana amabaye kwanza nilimkuta Botswana. Halafu nikaenda kumuona Zimbabwe. Nilipokwenda  Afrika Kusini nikakutana naye tena. Bado wakati narudi Tanzania nikashuka  naye kwenye ndege moja ingawa wakati wa kupanda ndege sikumuona.
 
Na huko kote alikuwa akiwaua watu niliokuwa nimewafuata. Mtu wa mwisho alikuwa mkazi wa hapa hapa Dar ambaye alishuka naye kwenye ndege.
 
Watu  wote aliowaua walikuwa wakidaiwa na marehemu babu yangu na mauaji yalifanyika wakati ule nafanya ziara yakufuatilia madeni.
 
Mwisho wa siku msichana huyo alinipigia simu na kuniambia kuwa ana mazungumzo na mimi kuhusu mali za babu yangu.
 
Aliniona Botswana. Aliniona Zimbabwe. Aliniona  Afrika Kusini lakini hakuniambia kuwa ana mazungumzo na mimi.
 
Katika nyumba aliyonielekeza niende nimeambiwa kwamba msichana huyo wanamfahamu lakini alikwisha  kufa miaka mitano iliyopita.
 
Sasa napata picha  kwamba msichana huyu hakuwa wa kawaida. Zile  safari alizozifanya kule Botswana, Zimbabwe na Afrika  Kusini pia hazikuwa za kawaida. Niliona  kama alikuwa akiibuka tu katika zile nchi nilizomkuta. Hakuwa akisafiri. Hakukuwa na hadi leo hakuna  usafiri wa haraka kiasi kile.
 
Pia yale mauaji aliyokuwa akiyafanya hayakuwa ya kawaida. Kwa mwanamke kuwaua wanaume kirahisi  rahisi namna ile haikuwa kawaida.
 
Baada ya kuwaza hayo nikajiuliza, yule msichana alikuwa shetani au mzuka wa Ummy niliyeelezwa kuwa alikwishakufa?
 
 
ITAENDELEA kesho hapahapa Usikose
 

No comments:

Post a Comment