Tuesday, April 4, 2017

SIMULIZI, NILIKONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 5

SIMULIZI
 
NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 5
 
ILIPOISHIA
 
Ilipofika saa saba mchana wakati natazama taarifa ya habari kwenye televisheni, lile tukio la mauaji lililotokea pale hoteli lilitangazwa.
 
Kitu ambacho kilinishitua ni kuwa mtangazaji alimtaja marehemu kuwa ni Isaac Chusama mtu ambaye alikuwa hafahamiki alikuwa akifanya kazi gani. Alitaja mtaa aliokuwa akiishi na kueleza kuwa hakuwa na mke wala watoto.
 
Taarifa ilieleza kuwa Chusama alifika hapo hoteli majira ya mchana na kuzungumza na msichana mmoja aliyekuwa ameketi kwenye ukumbi wa hoteli hiyo kabla ya kukodi chumba na kuingia chumbani na msichana huyo.
 
Taarifa ya televisheni iliendelea kueleza kuwa asubuhi ya siku ile mhudumu wa usafi wa hoteli hiyo aliigundua maiti ya Chusama iliyokuwa imelazwa chini na kutoa taarifa kwa uongozi wa hoteli.
 
SASA ENDELEA
 
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, uchunguzi wa madaktari umeonesha kuwa marehemu alikabwa koo hadi mauti yakamkuta.  
 
Msemaji wa polisi akaeleza kuwa polisi wanamshuku msichana aliyekuwa naye kuhusika na mauaji hayo na wameanzisha msako wa kumtafuta.
 
Baada ya taarifa hiyo kutolewa kwenye televisheni, nilibaini kuwa mtu aliyefika hapo hoteli na hatimaye kuuawa alikuwa ni mwenyeji wangu Isaac Chusama!
 
Hapo niligundua sababu ni kwanini simu nilizokuwa nikipiga zilikuwa hazipokelewi. Zilikuwa haipokelewi kwa sababu Chusama mwenyewe alikuwa ameshauawa. Bila shaka alikuwa ameuawa siku iliyopita.
 
Sasa nikabaki na maswali kuhusiana na tukio hilo. Nilijiuliza  yule msichana alikuwa nani?
 
Je alikuwa akijuana na Chusama?
 
Na ni kwanini amemuua?
 
Pia nilijiuliza baada ya Chusama kuuawa, kulikuwa na uwezekano kweli wa kulipwa pesa zangu? Na ni nani atanilipa?
 
Baada ya kufikiri kwa kina niliona uwezekano wa kulipwa pesa zangu haukuwepo. Kwani licha ya kuwa ni pesa nyingi nilizokuwa nikimdai Chusama pia nilikuwa si mwenyeji wa hapo na pengine nisiaminike na huyo ambaye atapaswa kulipa deni hilo.
 
Lakini baya zaidi, nilijiambia kama nitajitia kuwatafuta ndugu na jamaa wa Chusama ili wanilipe deni hilo wanaweza kuniripoti polisi na nikakamatwa na kuhusishwa na mauaji ya Chusama. Hapo nikaingiwa na hofu.
 
Matumaini ya kupata pesa nilizozifuata huko Zimbabwe yakaanza kuota mbawa. Kule kukata tamaa na kuona safari niliyoifanya ilikuwa ya bure, nilijikuta nikimlaumu Chusama kwa uzembe. Licha ya kutojua kama yule msichana alikuwa na uhusiano naye au la, nilimlaumu Chusama kwa kuonesha kuwa na tamaa ya ngono iliyopitiliza.
 
Niliamini kuwa Chusama alipokuwa anakuja pale hoteli alikuwa akinifuata mimi lakini ghafla akili yake ilikwenda kwa yule msichana akasahahu kwamba nilikuwa na ahadi naye na hata nilipompigia simu hakupokea. Matokeo yake yalikuwa ni kuuawa.
 
Lakini ni kwanini auawe? Nikajiuliza na  kuendelea kujiuliza, yule msichana alikuwa nani? Ana kisa naye gani na baada ya kumuua Chusama, alipotelea wapi?
 
Sikuweza kupata jibu hata la kukisia. Nilikuwa nimeketi pale ukumbini nikainuka na kurudi chumbani.
 
Wakati ninapanda ngazi nilijiambia ni vizuri niondoke haraka hapo Zimbabwe kwani licha ya kuwa nisingepata faida yoyote kwa kuendelea kukaa hapo bali pia nilitaka kuepuka uchunguzi wa polisi.
 
Nilihisi kwamba katika uchunguzi wao polisi wanaweza kugundua kwamba Chusama alikuwa amenipangia chumba pale hoteli na ninaweza kukamatwa na kuulizwa nilikuwa na mpango naye gani.
 
Baada ya kuingia chumbani nilichukua begi langu nikatoka kimya kimya. Nilikodi teksi na kurudi kiwanja cha ndege. Kwa bahati njema nilikuta kulikuwa na ndege inayokwenda Botswana ambayo bado ilikuwa na nafasi.
 
Nikakata tikiti ya ndege ya kwenda Botswana. Ndege iliondoka maasaa matatu baada ya mimi kufika kiwanja cha ndege. Nilipofika Gaborone, nilimpigia simu Benjamin Muhoza na kumjulisha kuwa nilikuwa katika kiwanja cha ndege cha Gaborone.
 
“Subiri ninatuma gari ikufuate” Sauti ya Muhoza ikasikika kwenye simu.
 
“Dereva wako atanitambuaje” nikamuuliza.
 
“Umevaa mavazi gani?”
 
“Kwanza mimi ni mrefu wa wastani na mweupe. Nimevaa tisheti ya rangi ya samli, suruali aina ya jinzi ya rangi ya samawati. Nimevaa miwani ya jua”
 
“Atakutambua. Nitakupa namba ya usajili ya gari atakalokuja nalo”
 
“Sawa”
 
Muhoza alinitajia namba ya usajili ya gari hilo, aina yake na rangi yake. Nikamwambia nitalitambua litakapofika.
 
Saa moja baadaye nikiwa hapo nje ya jengo la uwanja wa ndege nikaliona gari hilo likiwasili. Sikutaka kumpa dereva wa gari hilo taabu ya kunitafuta. Nikamfuata.
 
Baada ya kujitambulisha kwake kuwa mimi ndiye mgeni wa Chusama aliniambia nijipakie kwenye gari.
 
Nilijipakia katika siti ya mbele iliyokuwa kando ya dereva. Gari hilo lilinipeleka katika hoteli moja ambapo mwenyeji wangu tayari alikuwa amenichukulia chumba.
 
“Sasa acha nimfuate mheshimiwa” Dereva akaniambia baada ya kunifikisha hapo hoteli. Akaongeza.
 
“Aliniambia nikishakufikisha hapa hoteli nimfuate”
 
“Sawa” nikamjibu. Wakati huo nilikuwa nimekaa katika bustani iliyokuwa mbele ya hoteli ambayo iliwekewa viti na meza.
 
“Unaweza kuagiza kinywaji unachotaka au chakula”
 
“Labda kinywaji tu, sitapenda kula kitu chochote kwa sasa” nikamwambia.
 
Dereva huyo alipoondoka muhudumu alinifuata na kuniuliza kama nilikuwa ninahitaji huduma yoyote.
 
“Nipatie soda tu” nikamwambia.
 
“Soda gani?”
 
“Fanta”
 
Mhudumu akaondoka. Baada ya muda mfupi alirudi na kuniletea soda niliyomuagiza.
 
ITAENDELEA kesho usikose uhondo huu jamaa amewasili Gaborone, je  nako nini kitatokea je, atafanikiwa nako huko. ungana nami kesho.
 
 
 
 

No comments:

Post a Comment