Friday, April 14, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 10

ZULIA LA FAKI, 0655 340572
 
NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 10
 
ILIPOKIONA
 
Uchunuzi wa madaktari wa hospitali ya Muhimbili ulionesha kuwa marehemu aliuawa kwa kukabwa koo na kukosehwa pumzi kwa zaidi ya dakika tano jambo lililosababisha moyo wake kusimama na hivyo kusababisha kifo chake.
 
Sasa mshituko mkubwa niliupata wakati picha ya Abdul Baraka ilipooneshwa. Alikuwa ni yule mtu niliyemuona amefuatana  na yule msichana muuaji jana yake.
 
Hapo hapo nikajua kwamba aliuawa na yule msichana ambaye alitoweka baada ya kufanya mauaji hayo.
 
Nikajiuliza ni kwanini hawa watu wanaodaiwa na marehemu babu yangu wanauawa na anayewaua ni mtu mmoja tena msichana, amezunguka nchi zote kuwafuata?
 
Jambo jingine la ajabu nililoliona ni kuwa mauaji hayo yanafanyika wakati ule ninafuatilia madeni hayo. Kulikoni!
 
Nilitamani kwenda polisi kueleza nilichokuwa ninakifahamu kuhusu yule msichana lakini niliogopa kwa sababu sikuwa nikijua yule msichana alikuwa nani. Angeweza kuwa gaidi au ni mtu aliyetumwa kufanya mauaji.
 
Nikajiambia kama nitajitia kimbele mbele cha kumripoti polisi ningeweza kuuawa. Nikaamua kuwa kimya.
 
Wiki moja ikapita. Siku hiyo nilikuwa nimekaa nyumbani kwangu nikiwaza, simu yangu ikaita.
 
SASA ENDELEA
 
 Namba iliyokuwa ikinipigia ilikuwa ngeni kwangu. Nikaipokea ile simu.
 
“Hello!”
 
“Hello, nazungumza na Kassim Fumbwe?’ Sauti ya mwanamke ikaniuliza.
 
“Ndiyo. Kassim Fumbwe. Nani mwenzangu”
 
“Naitwa Ummy. Nilikuwa na mazungumzo na wewe. Nilihitaji tukutane”
 
Moyo wangu ulishituka kidogo.
 
“Tukutane wapi?”
 
Mimi niko Suzy Hotel hapa Masaki. Niko chumaba namba 35. Ukifika utanikuta”
 
Nikasita kidogo kabla ya kumuuliza.
 
“Unanifahamu vipi?”
 
“Ninakufahamu. Kama unataka kujua zaidi nitakufahamisha utakapofika”
 
“Hayo mazungumzo yanahusu nini?”
 
“Yanahusu mali za marehemu babu yako”
 
Aliponiambia hivyo sikutaka kuendelea kumhoji, nikamwambia.
 
“Nisubiri ninakuja sasa hivi”
 
Simu ya upande wa pili ikakatwa. Nilikuwa nimeketi sebuleni nikainuka na kutoka. Gari langu ambao nililirithi kwa babu nilikuwa nimeliegesha nje. Nikajiapakia na kuliwasha.
 
Gari lilipowaka nilitia gea na kuelekea Masaki huku nikijiuliza huyo mwanamke aliyenipigia simu alikuwa nani na alitaka kunieleza nini kuhusu mali za marehemu babu yangu.
 
Kilichonifanya nikurupuke na kumfuata haraka haraka ni ule utata wa mali za marehemu babu. Babu alikuwa tajiri lakini baada ya kufa alionekana hakuwa na mali yoyote.
 
Nilitarajia kuwa mwanamke huyo alikuwa akijua siri ya mali za marehemu babu na angenifichulia.
 
Nilipofika Suzy Hotel iliyokuwa Masaki niliegesha gari katika eneo la kuegeshea kisha nikatoa simu na kumpgia yule mwanamke.
 
“Nimeshafika?” nikamwambia.
 
“Uko wapi?” Sauti ya mwanamke ikauliza kwenye simu.
 
“Niko  hapa mbele  ya hoteli”
 
“Njoo chumba namba 35 kipo ghorofa ya kwanza”
 
“Sawa”
 
Nikashuka  kwenye gari na kuingia hotelini humo. Nilipanda ngazi hadi ghorofa ya kwanza, nikakitafuta chumba namba 35. Nilipokiona nikakifuata na kubisha mlango.
 
Baada ya sekunde  chache tu mlango  ulifunguliwa na msichana.
 
“Karibu ndani” akaniambia huku akitabasamu.
 
Nilipomtazama vizuri, sura yake  ikanijia akilini mmwangu.
 
Alikuwa ni yule msichana muuaji niliyekutana naye Botswana,  Zimbabwe na kisha Afrika Kusini.
 
Nilipogundua kuwa alikuwa ni yeye nilishituka nikarudi nyuma hatua  moja  kisha nikageuka  na kutoka  mbio.
 
“Mbona  unakimbia?” Niliisikia sauti  yake ikiniuliza kwa nyuma.
 
Sikujibu wala  sikusimama. Nilishuka ngazi mbili mbili nikafika chini. Pale chini niliona nikikimbia nitawatia watu wasiwasi nikatembea taratibu na kutoka  nje ya hoteli. Nikajipakia kwenye gari langu na kuliondoa kwa kasi.
 
Bila shaka yule mwanamke alitaka kunimaliza na mimi, nilijiambia kimoyomoyo huku nikizidi kukanyaga mafuta.
 
Nilishindwa kujua aliipataje namba yangu na alijuaje kuwa ninaitwa Kassim Fumbwe kwani aliponipigia simu aliniuliza kama  mimi ni Kassim Fumbwe.
 
Aliponipigia simu sikutarajia kama alikuwa ni  yeye. Si kwa sababu ya kunitambua kuwa mimi ni Kassim Fumbwe bali vile alivyoniambia kuwa ana mazungumzo na mimi kuhusu mali ya babu yangu.
 
Nikahisi kwamba likuwa akijua mengi kuhusu mimi hasa vile ambavyo alihusika katika safari yangu nzima kutoka Botswana, Zimbabwe, Afrika Kusini hadi kurudi tena Tanzania.
 
Sasa nikapata wazo moja kwamba ni kweli alikuwa akiifahamu siri ya mali ya marehemu babu yangu kwa sababu yeye ndiye aliyeifanya safari yangu isiwe na mafanikio. Yeye ndiye aliyewaua watu wote waliokuwa wakidaiwa na babu yangu. Sababu za kuwaua alikuwa akizijua mwenyewe.
 
Nikaendelea kujiambia, kwangu mimi msichana huyo atabaki kuwa adui. Ingawa sikuweza kujua ni kwanini aliwaua wale watu lakini nilijenga hofu kwamba alitaka kuniua na mimi.
 
Hii ndio sababu nilimkimbia pale hoteli.
 
Nilipofika nyumbani nilikaa sebuleni na kuendelea kujiwazia kuhusu yule mwanamke. Ghafla simu yangu ikaita. Nilipotazama namba nikaona ni ile ya yule msichana. Nikaipokea.
 
ITAENDELEA kesho hapahapa tangakumekuchablog, Usikose
 
 

No comments:

Post a Comment