Sunday, April 9, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 8

ZULIA LA FAKI 0655 340572
 
NILIKIONA CHA MTO URITHI WA BABU 8
 
ILIPOISHIA
 
Yule dereva wa Muhoza alipoondoka pale hoteli sikumuona tena. Nikalala pale hoteli hadi siku iliyofuata ambapo nililazimika kujilipia mwenyewe chumba.
 
Nikafanya mipango ya usafiri wa kwenda Afrika Kusini. Nikagundua kuwa ulikuwepo usafiri wa treni wa kutoka Zimbabwe hadi hadi Afrika Kusini.
 
Nikasafiri kwa treni hadi Cape Town. Nilipofika kwenye kituo cha treni cha Cape town, nikampigia simu Domesan Dube kumjulisha kuwa nilikuwa nimewasili kwa treni kutokea Zimbabwe.
 
Dube akaniambia kuwa anamtuma dereva wake anifuate. Baada ya kupita kama saa moja hivi, dereva huyo akawasili na gari. Alinipakia akanipeleka nyumbani kwa Dube.
 
Wakati anasimamisha gari mbele ya jumba lake la kifahari nilimuona yule msichana muuaji akitoka katika jumba hilo. Alipungia mkono teksi iliyokuwa inapita barabarani. Teksi iliposimama akajipakia na kuondoka.
 
Yule dereva hakushituka kumuona msichana huyo lakini mimi nilishituka sana.
 
SASA ENDELEA
 
Mimi nilishituka kwa sababu nilikuwa namfahamu na nilikuwa nafahamu visa alivyovitenda kule Botswana na Zimbabwe.
 
Lakini pia nilishituka vile nilivyomkuta Afrika Kusini wakati jana yake tu aliuaa mtu Zimbabwe.
 
Kitu kingine kilichonifanya nishituke ni kuona msichana huyo alikuwa akinifuatia kwa wale wadaiwa wangu ambapo kile nchi niliyokuwa ninakwenda nilikuwa namkuta akiwa na mtu niliyekuwa namfuata.
 
Baada ya gari kusimama, dereva alishuka na  mimi nikafungua mlango haraka  na kushuka. Tayari uso wangu ulikuwa umeshatahariki baada ya kumuona yule msichana.
 
Dereva alitangulia kuingia  ndani ya jumba  hilo akaniambia.
 
“Karibu ndani”
 
Nikaingia ndani. Tulitokea kwenye sebule pana iliyokuwa imepambwa vizuri.
 
Mimi na yule dereva tulishituka tulipomuona mtu aliyekuwa amelala chini akiwa ametoa macho karibu na mlango.
 
“Oh Bwana Dube!” Dereva alitoa sauti ya kimako kisha akachutama na kumtazama yule mtu.
 
“Bwana Dube…Bwana Dube…!” akamuita huku akijaribu kumtikisa.
 
Mtu huyo alikuwa kimya huku macho yake yakitazama dari bila kupepesa. Sikuwa daktari na sikuwa na uzoevu wa kutazama miili ya watu waliokufa lakini nilipotazama yale macho, niligundua mara moja kuwa mtu huyo alikuwa ameshakufa.
 
“Huyo ndiye Bwana Dumesan Dube?” nikamuuliza yule dereva.
 
“Ndiye yeye. Sijui amepatwa na nini!”
 
“Kuna msichana alitoka humu ndani wakati tunafika, ni nani?”
 
Dreva akatikisa kichwa.
 
“Sikumfahamu. Ngoja nimuite daktari wake, labda ni presha”
 
Dereva huyo aliyekuwa ametaharuki aliinuka akatoa simu yake na kutafuta namba ya daktari wa Dube kasha akampigia.
 
“Bwana Dube ameaguka chini, sijui amepatwa na nini?” alisema baada ya simu kupokelewa.
 
Niliisikia sauti ya upande wa pili ikiuliza.
 
“Ameanguka wapi?”
 
“Nyumbani kwake. Nilikuwa nimetoka kidogo niliporudi nilimkuta yuko chini lakini hasemi na inaonekana hana fahamu”
 
“Subiri, ninakuja”
 
Dereva akakata simu na kunitazama.
 
“Daktari wake anakuja. Tumsubiri”
 
“Kwani Bwana Dube ana tatizo la presha?” nikamuuliza.
 
“Presha ni tatizo linaloweza kutokea ghafla tu, si lazima uwe nalo siku za nyuma”
 
Huyo daktari alliyeitwa aliharakisha kufika. Baada ya dakika thelathini tu aliusukuma mlango na kuingia ndani.
 
Alipomuona Dube akiwa chini hakuuliza chochote, alichutama na kuanza kumpima. Alianza kumpima presha kwa kutumia kipimo cha kufunga kwenye mkono.
 
Alipomaliza aliinuka na kutuambia.
 
“Nasikitika kuwambia kuwa Bwana Dube ameshakufa. Apelekwe hospitali kwa uthibitisho zaidi”
 
“Ameshakufa!” Dereva wa Dube alimaka uso wake ukionesha kutoamini.
 
“Apelekwe hospitali” Daktari akasisitiza.
 
“Lakini ni jambo la kushangaza sana kwa sababu niliachana naye muda mchache tu uliopita”
 
“Umeniambia kwamba alianguka?” Daktari akamuuliza.
 
“Itakuwa alianguka kwani tulipokuja tulimkuta hapo chini”
 
“Ana dalili kama ya kukabwa kwenye shingo yake”
 
Dereva alizidi kupata taharuki.
 
“Amekabwa? Amekabwa na nani? Humu ndani hakuna mtu. Au aliingia mtu na kumkaba?’
 
“labda ni yule msichana tuliyemuona akitoka?” nikamwambia.
 
“Msichana anaweza kumkaba?”
 
“Anaweza”
 
“Mimi naondoka. Nimewambia mumpeleke hospitali. Huko atafanyiwa uchunguzi na sababu ya kifo chake itajulikana” Daktari akatuambia na kutoka.
 
Nikajiambia kwamba kwa vile suala hilo linahusu mauaji, ingebidi lifike polisi na likifika huko, mimi na dereva wa Dube tutakuwa ndio watuhumiwa wa kwanza.
 
Kwa sababu ya kuogopa ushahidi, sikueleza chochote kuhusu yule msichana, nikamuacha yule dereva akishughulikia suala hilo. Mimi nikatafuta hoteli nikapanga chumba.
 
Kwa kweli suala la yule msichana muuaji lilisumbua akili yangu. Nilishindwa kujua msichana huyo alitokea wapi na kwanini alikuwa akiwaua wale watu. Pia nilikuwa nikijiuliza alikuwa akiwaua kwa namna gani?
 
Kile kitendo cha kumuona  akitoka katika jumba la Dube kilitosha kunithibitishia kuwa ndiye aliyemuua Dube.
 
Nilikuwa nina pesa chache ilizobaki ambazo zilitosha kukata tikiti ya kurudi Dar. Asubuhi kulipokucha nikaenda kukata tikiti na kuondoka. Safari yangu haikuwa na mafanikio yoyote. Zaidi ilikuwa ni kupata hasara tu na kupotea muda.
 
 
ITAENDELEA kesho, nini kitatokea kabla ya kuondoka Afrika Kusini, ungana nami kesho.
 

No comments:

Post a Comment