Monday, April 17, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 11

ZULIA LA FAKI, 0655 340572
 
NILIKIONA CHA MTO  URITHI  WA BABU 11
 
ILIPOISHIA
 
“Mbona umekimbia?” Sauti ya msichana ikaniuliza.
 
“Hebu niambie ukweli wewe ni nani?” nikamuuliza.
 
“Kama ulikuwa hunijui kwanini umenikimbia?”
 
“Nimekukimbia kwa sababu”
 
“Sababu gani?”
 
“Wewe si nilikukuta Botswana siku chache ziliopita halafu nikakuona tena Zimbabwe na jana ulikuwa Afrika Kusini?”
 
“Kumbe umenikariri vizuri”
 
“Nimekukariri kwa sababu nimeona kila nchi niliyokwenda nilikuwa nakuona”
 
“Ndiyo sababu nilitaka kukutana na wewe”
 
“Kwani wewe ni nani? Unamjuaje marehemu babu yangu na umenijuaje mimi?”
 
SASA ENDELEA
 
“Sasa hayo ndiyo mambo ambayo tutazungumza tutakapokutana
 
Nikatikisa kichwa changu ingawa niliyekuwa nikizungumza naye hakuwa karibu yangu.
 
“Hilo la kukutana na wewe litakuwa gumu kidogo”
 
“Hutaki kujua zilipo mali  za marehemu babu yako”
 
“Ninataka sana lakini kuna mambo  ambayo yamenishitua”
 
“Niambie ni mambo gani?”
 
“Kuna watu ambao ulikuwa karibu nao.  Hao watu  waliuawa katika mazingira ya kutatanisha” nikamwambia.
 
“Wapi huko?”
 
“Botswana, Zimbambwe na Afrika Kusini”
 
“Umetaja lakini bado mmoja”
 
“Abdul Baraka  wa Mbezi hapa Dar aliuawa pia”
 
“Waliuawa na  nani?”
 
“Nilikuona wewe na Abdul Baraka mkishuka kwenye ndege kutoka  Afrika  Kusini”
 
“Swali nililokuuliza,  wameuawa na nani?”
 
Hapo niligwaya kujibu. Niliona  kama  nitamwambia aliwaua yeye anaweza kukasirika na akajua  kuwa nina ushahidi kuwa yeye nndiye  muuaji. Akipata uhakika huo  nilihofia kuwa anaweza kunisaka kwa udi na uvumba ili aniue.
 
Nikamuuliza. “Uliponiambia  bado mmoja ulikuwa na  maana  gani?”
 
“Nilikuwa nina maana unayoijua wewe”
 
“Mimi sijui  kitu”
 
“Haiwezekani kuwa hujui kitu. Usingeniambia kuwa kuna watu walikuwa karibu na mimi na wameuawa. Ulikuwa na maana gani?”
 
“Usinielewe vibaya. Nilimaanisha hao watu walikuwa na  wewe kabla ya kuuawa”
 
“Hao watu wanakuhusu?”
 
“Walikuwa wakidaiwa  na marehemu babu yangu”
 
“Tunarudi pale pale katika mali ya marehemu babu yako. Bado hutaki kujua kile  kilicho nyuma ya pazia”
 
“Ninataka”
 
“Sasa naomba kukutana na wewe kwa mara nyingine”
 
Nikafikiri kidogo kisha nikamwambia.
 
“Kwanini tusizungumze kwenye simu?”
 
“Hatuwezi kuzungumza kwenye simu kila  kitu.  Kuna  maongezi mengine ni lazima tukutane mimi na wewe”
 
“Ungejitambulisha kwanza ili niweze kukujua vizuri, wewe ni nani  na  unamjuaje babu yangu?”
 
“Sasa ili unijue vizuri mimi, nitakuelekeza mahali ambapo utapata habari  zangu kikamilifu na tutaweza kuonana mimi  na wewe”
 
“Nielekeze ni mahli gani??”
 
Msichana akanielekeza mtaa mmoja ulioko eneo la Mwananyamala. Pia akanitajia namba ya nyumba.
 
“Ukifika uliza Sharif Nasri” akaniambia.
 
“Huyo Sharif  Nasri  ni nani?”
 
“Ni  baba yangu”
 
“Umeniambia  wewe unaitwa nani?”
 
“Naitwa Ummy Sharif  Nasri”
 
“Wewe ni sharifu?”
 
“Hilo  ni jina tu”
 
“Kwa hiyo kama nitampata huyo mzee nimuulize kuhusu wewe?”
 
“Ndiyo muulize na mimi utanipata hapo hapo”
 
“Sawa. Nitafanya hivyo”
 
“Basi nakutakia mchana mwema”
 
Msichana akakata simu.
 
Aliniacha na mawazo yaliyochanganyika na fadhaa. Nilijiuliza maswali mengi sana yaliyokosa majibu.
 
Imani niliyokuwa nayo ni kuwa huyu  msichana  ndiye aliyewaua wale watu niliowafuata kule Botswana, Zimbbabwe na Afrika Kusini. Na ndiye pia aliyemuua Baraka Abdul aliyeuawa nyumbani kwake Mbezi.
 
Kama kweli ndiye aliyewaua, ilikuwa ni lazima niwe na hofu naye na ni lazima nishuku kuwa pengine alitaka  kuniua na  mimi ingawa sababu za kufanya mauaji hayo nilikuwa sizijui.
 
Sasa kwa kunielekeza kwa mtu mwingine ambaye aliniambia ni baba yake, alizidi kunichanganya. Nilijiuliza huyo mtu atanieleza nini kuhusu msichana huyu aliyeonesha kila dalili ya kupata mafunzo ya uuaji.
 
Nikaendelea kujiuliza, huyo mzee anajua nini kuhusu watu  hao waliouawa na mwanawe na anajua sababu za mauaji hayo?
 
Au  mzee huyo anamjua babu yangu au ananijua mimi?
 
 
ITAENDELEA kesho Usikose Uhondo huu nini kitatokea,
 
 
 

No comments:

Post a Comment