Friday, April 28, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URUTHI WA BABU SEHEMU YA 15

ZULIA LA FAKI
 
NILIKIONA CHA MTO URITHI WA BABU 15
 
ILIPOISHIA
 
Nikajiambia kama  hatakuwa shetani atakuwa ni mzuka. Lakini sikuelewa ni kwanini mzuka huo uliwaua wale watu na kwanini  uliniambia kuwa unajua siri za mali za babu yangu.
 
Kwa vile suala la msichana huyo lilikuwa limenipa dukuduku, nilipofika  nyumbani nikapata wazo moja. Wazo hilo lilikuwa ni kufanya  utafiti ili kumjua huyo Ummy niliyemabiwa kuwa alikufa, alikuwa msichana wa aina  gani. Alikuwa  akifanya kazi  gani na pia nijue kama alikuwa na uhusiano na marehemu babu yangu.
 
Sikutaka tena kumpigia simu Ummy kwa sababu huenda angeipokea na kunieleza maneno ya kunitisha.
 
Ili kuanza upelelezi wangu niliona niende katika mtaa ule ule aliokuwa anaishi Ummy nitafute mtu aliyekuwa anamfahamu nifanye  naye  urafiki na kisha nianze kumhoji kuhusu maisha ya Ummy mpaka kufa kwake.
 
Ule mtaa nilikuwa mgeni nao, nilijua isingekuwa kitu rahisi kumpata rafiki wa kunipa habari za Ummy lakini  nilijiambia ni lazima nijitahidi kwa kadiri ya uwezo wangu nimpate mtu ambaye ataweza kunifumbulia kitendawili  cha Ummy Nasir.
 
SASA ENDELEA
 
Siku ile yule msichana hakunipigia simu na mimi sikumpigia. Mimi sikumpigia kwa hofu niliyoipata baada ya kuelezwa kuwa msichana huyo alishakufa. Na kama alishakufa na nimekuja kukutana naye, basi atakuwa ni mzuka.
 
Asubuhi ya siku ya pili yake  nikaenda katika ule mtaa niliyokwenda jana yake kumuulizia  Ummy.  Safari hii sikwenda na  gari langu. Nilipanda daladala.
 
Sikutaka kufika tena pale nyumbani kwa mzee Nasir. Nilizuga zuga katika nyumba zilizokaribiana na nyumba  yake nikitafuta mtu ambaye ningeweza kufanya naye urafiki  na kumuuuliza kuhusu marehemu Ummy.
 
Katika kutupatupa macho nikaona  sehemu iliyokuwa na meza ya  kahawa na kashata.  Kulikuwa na mabenchi matatu ya kukalia.  Muuza kahawa aliyekuwa amevaa kofia kubwa lililosukwa kwa minyaa kama la mvuvi  wa samaki, alikuwa amekaa upande wa pili wa meza yake akiwa na ndoo mbili, jiko na birika la kahawa lililokuwa likifuka  moshi jikoni.
 
Muda ule kulikuwa na mtu mmoja tu aliyekuwa amekaa akinywa kahawa. Nikaona  niende nikakae mahali hapo ili nifikirie la kufanya.
 
Mara tu nilipoketi akaja mtu mwingine. Tukawa watu watatu.
 
Muuza kahawa akatutilia kahawa bila hata kutuuliza. Ukishakaa kwenye benchi lake maana yake ni kuwa unataka kahawa.
 
Nilichomsikia  akiuliza ni.  “Nikutilie tangawizi?”
 
Alikuwa akimtazama yule mwenzangu aliyekuja baada ya mimi.
 
“Ndiyo tia” Mtu huyo  akamjibu.
 
“Na wewe?” akaniiuliza mimi.
 
Wakati  ananitazama, sura yake ikanijia akilini mwangu. Zilinichukua  kama nukta tatu hivi kumkumbuka  Selemeni Mzaramu.
 
Wakati  namkumbuka, yeye alishanikumbuka zamani.
 
“Ah! Kasim Fumbwe… kumbe  ni wewe?” akaniuliza  kwa mshangao.
 
“Mzaramu!  Bado upo Dar hii!” nikamuuliza.
 
“Twende wapi ndugu yangu. Tunabangaiza humu humu. Makamba alituambia tutabanana hapa hapa”
 
Tukacheka.
 
“Nikuwekee tangawizi?’  akaniiuliza tena.
 
“Ndiyo niwekee”
 
Selemani Mzaramu alikuwa rafiki yangu wa miaka mingi. Nilisoma naye shule ya msingi hadi darasa la saba. Wakati  mimi  naendelea na masomo ya sekondari, mwenzangu hakuchaguliwa. Na baada ya hapo sikuwahi kukutana  naye tena hadi siku ile nilipomuona  amevaa kofia la minyaa akiuza kahawa.
 
Mzaramu alinisogezea kikombe cha  kahawa akaniuliza.
 
“Uko wapi Kasim?”
 
“Mimi niko hapa hapa  Dar. Nilikuwa Morogoro , maisha yakanishinda, nikarudi hapa  Dar”
 
“Unafanya kazi  wapi,  nije  unipe kibarua?”
 
“Bado nipo  nipo tu, sifanyi kazi popote. Nilikuwa na duka Morogoro, duka likafa, nikarudi Dar baada ya babu yangu kufariki. Na ndiyo nimeamua niendelee kuwa hapa”
 
“Mimi baada ya masomo nilihangaika na malori mpaka yamenitia kilema. Sasa  nipo  hapa?”
 
“Alah! Umepata ulemavu?”
 
“Mguu wangu ulivunjika  mara tatu. Mfupa ulisagika vibaya. Nimeokolewa na vyuma…”
 
Mzaramu alinionesha mguu  wake wa kushoto  baada  ya kuisega suruali yake. Mguu huo ulikuwa hautazamiki kwa mishono!
 
“Nje unaouna ni mguu lakini  ndani  ni vyuma vitupu, yaani ulikuwa ukatwe lakini kaka  yangu alijitahidi sana kunipeleka hospitali za pesa ambako niliwekewa vyuma. Nikasema sasa malori basi”
 
“Loh! Pole sana rafiki yangu. Ulikuwa dereva?”
 
“Nilikuwa taniboi. Basi nilikaa hospitali karibu mwaka  mzima”
 
Nikatikisa kichwa changu kumsikitikia.
 
“Pole sana rafiki yangu lakini kama unapata riziki yako na maisha yanakwenda, shukuru Mungu”
 
“Nashukuru.  Nimeoa na nina watoto  wawili lakini mke wangu alinikimbia aliposikia nitakatwa mguu. Kaniachia watoto lakini nimewalea mwenyewe na hivi  sasa wanasoma”
 
“Kumbe  ulipata  mkasa mkubwa rafiki yangu….”
 
“Kula kashata” Mzaramu akaniambia.
 
Nikaokota kashata moja na kuing’ata.
 
“Unazitengeza  mwenywe?” nikamuuliza.
 
“Nazitengeza mwenyewe usiku.  Asubuhi nakuja  nazo”
 
“Kwani unaishi wapi??’
 
“Naishi hapa  hapa  Mwananyamala”
 
“Mtaa huu?”
 
“Ndiyo  naishi mtaa huu huu lakini ni kule mwisho”
 
“Umeishi mtaa  huu kwa miaka mingapi?’
 
“Nina miaka  kumi na mitano  sasa”
 
Nikajiambia kimoyomoyo kuwa atakuwa anamjua Ummy ambaye alikufa  miaka mitano tu iliyopita.
 
“Katika mtaa huu alikuwa akiishi msichana mmoja  aliyekuwa akiitwa Ummy Nasri…”
 
“Nyumba  yao ile paleee lakini huyo msichana alikwisha  kufa  zamani ila namfahamu sana”
 
ITAENDELEA kesho Usikose
 

No comments:

Post a Comment