Saturday, December 27, 2014

KISIWA HARISHI (20)

KISIWA CHA HARISHI (20)
 
ILIPOISHIA TOLEO LILILOPITA
 
Shazume akatikisa kichwa bila kusema lolote.
 
“Kakangu najua umepatwa na fadhaa lakini tumbo lako likipata riziki ndio akili itakuja” Yasmin akamwambia Shazume.
 
“Tulikuwa watu saba sasa tumebaki wawili tu bado nile? Sitakula!”
 
“Wewe ni mwanaume Shazume usiogope kula. Unatakiwa upambane mpaka dakika ya mwisho. Mnaweza kuokoka ndugu zangu. Msikate tama kiasi hicho. Twende ukanywe uji japo kidogo!” Yasmin alimwambia.
 
Shazume akakubali kwenda. Tukaondoka sote kwenda kwa Yasmin. Ile maiti ya Haji tuliiacha pale pale. Tangu wenzetu walivyoanza kuuawa hatukuzika maiti yoyote. Zote tuliziacha ziliwe na kunguru.
 
Kwa hisia zetu tulikuwa kama watu tuliokuwa vitani. Akifa mtu hakuna kuzika. Kuzika kuna utaratibu wake ambao kutokana na hali tuliyokuwa nayo tusingeuweza.
 
Tulipofika kwa Yasmin alituandalia uji tukanywa. Mimi nilikunywa vikombe viwili, Shazume alikunywa kikombe kimoja.
 
Wakati tumepumzika Shazume akawa anahimiza tuondoke.
 
“Tumeshakunywa uji sasa tunaweza kwenda”
 
“Tusubiri kidogo nifikirie pa kuwapeleka” Yasmin akamwambia.
 
SAS ENDELEA
 
Baada ya kusubiri kwa muda kidogo Yasmin akatuambia. “Haya twendeni tukatafute nyumba nyingine”
 
Tukatoka na Yasmin. Niliona wazi kuwa Yasmin alikuwa na wasiwasi. Alikuwa akitupeleka katika nyumba nyingine lakini hakuwa mtu aliyeonesha matumaini.
 
Tulizunguka sana kutafuta nyumba nyingine ambayo ingeweza kutufaa kumkwepa Harishi. Tulikuta nyumba moja iliyokuwa ufukweni mwa bahari iliyokuwa na hali nzuri kidogo.
 
“Mnaionaje nyumba hii?” Yasmin akatuuliza huku akituonesha nyumba hiyo.
 
“Hii inafaa” nikamwambia kisha nikamtazama Shazume ili nipate mawazo yake.
 
“Unaionaje Shazume?”
 
“Hapa pamejificha kidogo, panafaa” akaniambia ingawa sauti yake haikuwa na nguvu.
 
Tukaingia katika ile nyumba. Humo ndani ilikuwa kama stoo iliyosahauliwa. Vitu vilikuwa vimerundikwa ovyo. Ubuibui na vumbi vilikuwa vimetanda pande zote.
 
Binaadamu mwenye akili zake timamu asingeweza kukaa ndani ya nyumba ile labda waduu kama vile nyoka na matandu. Lakini sisi hatukuwa timamu. Tulikuwa tumetingwa. Tungeweza kukaa.
 
Kama tungehitaji kufanya usafi ili nyumba hiyo iweze kukalika tungelazimika kutoa nje vitu vyote vilivyokuwa ndani na kuanza kufagia, kupiga deki na kusafisha kuta. Ingekuwa kazi kubwa. Ingetuchukua hata kwa siku mbili.
 
Tuliingia katika chumba kimoja tukatenga vitu na kupata upenyu mdogo ambao tuliusafisha na kuamua kukaa hapo.
 
Kusema kweli siku ile sisi sote hatukuwa na furaha. Tulikaa chini pamoja na Yasmin. Tukawa kimya. Kila mtu akiwaza lake.
 
Mimi nilkuwa nikiomba usiku usifike kwani karibu wenzetu wote waliuawa usiku.
 
Sikujua Yasmin na Shazume walikuwa wakiwaza nini. Lakini kila nilivyomuangalia Shazume niliona mawazo yake yalikuwa mbali sana. Nilikisia kwamba alikuwa akikumbuka kwao Pemba, akiwakumbuka wazazi wake na ndugu zake. Pengine hakuwa na matumaini ya kuwaona tena.
 
Bila shaka  Yasmin alikuwa akiwaza kama tutauawa atakosa wenzake wa kuzungumza nao na ataendelea kuwa mkiwa.
 
Mimi licha ya kuwa na hofu nlishajitolea kufa kupona. Sikupenda kujipa tama moja kwa moja kuwa nitapona na sikutaka kujikatia tama.
 
Ghafla Shazume akaanza kuimba kwa sauti ya huzuni. Ulikuwa wimbo maarufu uliokuwa unaimbwa na vikundi vya ngoma za kiasili.
 
“We Yauledi we niletee mashua twende Unguja!. We Yauledi niletee mashua twende Unguja!”
 
Na mimi nikamuitikia. “Ukipamba mke nawe ujipambe ndio suna. Usipojipamba watu hukwambia umtumwa! We Yauledi niletee mashua twende Unguja!”
 
Shazume aliendelea kuimba ubeti wake kwa kughani huku na mimi nikimuitikia.
 
Sauti ya wimbo huo ilikuwa ya huzuni lakini ilituchangamsha. Yasmin alikuwa akitutazama. Wakati ninamuitikia Shazume, Yasmin alikuwa akinifuatisha ninavyoimba.
 
Pengine tulikuwa tunajifariji kwa siku yetu ya mwisho kwani tangu tufike katika kisiwa kile, kila siku mwenzetu mmoja aliuawa na Harishi. Hakukuwa na siku yoyote ambayo hakukutokea kifo.
 
Kwa hiyo hatukujua usiku wa siku ile atakufa nani kati yangu na Shazume.
 
Shazume aliendelea kuimba kwa huzuni. Mimi nilikuwa nimenyamaza. Yasmin akawa anamuitikia.
 
Shazume alipoona mimi nimenyamaza na yeye akaacha kuimba tukawa kimya. Baada ya muda kidogo nilipata wazo.
 
“Tuombeni dua” nikawambia wenzangu.
 
“Tulikuwa tumejisahau kidogo” Shazume akasema
 
Nikasoma dua ndefu. Shazume na Yasmin wakawa wanaitikia “Amin”
 
Nilipomaliza nilimwambia Shazume aombe na yeye. Shazume akaomba dua ndefu, sisi tukamuitikia “Amin”
 
Alipomaliza nikamwambia Yasmin. “Omba na wewe”
 
ITAENDELEA KESHO, NA NINI KITAJIRI, USIKOSE UHONDO HUU KESHO

No comments:

Post a Comment