Saturday, December 27, 2014

WAHAMIAJI HARAMU SITA WANASWA, MUHEZA TANGA



Kumekucha blog
Muheza, POLISI Wilayani Muheza Mkoani Tanga, imewakamata wahamiaji haramu sita kwa tuhuma za kuingia nchini bila kibali wakiwa wamefichwa katika nyumba ya mtu anaesadikiwa kuwa ni wakala wa kusafisrisha wahamiaji haramu.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, kamanda wa polisi Mkoani hapa, Freisser Kashai, alisema polisi ilipata taarifa kutoka kwa wakazi kijiji cha Kicheba kuwepo kwa watu wanaokatisha mitaa  ambao hawafahamu.
Alisema alituma askari wa upelelezi kuchunguza kuwepo kwa watu hao na kubaini kama ni wahamiaji haramu na baada ya kujiridhisha kwao waliweza kuvamia usiku wa saa 8 na kuwakamta watu wote na mwenyeji wao kufanikiwa kutoroka.
“Jambo la kufurahisha ni kuona jamii inashirikiana na polisi kwa kila jambo ambalo wanahisi kwao  linaweza kuwaletea matatizo ----hili linaleta faraja na tunawaomba wananchi kushirikiana na polisi kwa kila jambo” alisema Kashai
Kamanda aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni,Gesemu Abato(30), Hash Negash(20), Tsegaye Aliso(21), Jamal Godso(25), Alemayo Ataro(22) na Erigudo Elitiro(25) wote walikamatwa wakiwa wamelala na kushindwa kutoroka.
Alisema watuhumiwa watafikishwa mahakamani mara baada ya uchunguzi kukamilika na kwa sasa wanaendelea kumtafuta wakala wao ili kuweza kumfikisha katika vyombo vya sheria na kuwa fundisho kwa wengine.
Katika tukio jengine, kamanda Kashai alilitaja kuwa ni mkazi wa Kinondoni, Enerst Joseph, amefariki baada ya gari lake alilokuwa akiendesha kuacha njia na kutumbukia katika mto na watu wawili waliokuwa ndani kupata majereha.
Alisema tukio hilo lilitokea juzi saa 7 mchana eneo la Kitumbi kata ya Mkata Wilayani Handeni barabara kuu ielekeayo Chalinze Mkoani Pwani na kuwajeruhi watu wawili ambao hadi muda huo hawajatambuliwa majina yao.
“Uchunguzi wa kipolisi umeonyesha kuwa dereva wa gari hilo alikuwa amelewa chakari na pombe zake kumfanya kwenda mwendo kasi bila kujitambua----alipofika mlima wa Kitumbi na kuteremsha alishindwa kuimudu kona ya daraja na kutumbukia” alisema Kashai
“Taarifa za dereva huyo ni kuwa hata katika kituo cha ukaguzi kilichopo kilometa moja tu kutoka eneo la ajali aliposimamishwa hakusimama---pombe zake bila kikomo zimemiondoa duniani” alisema Kashai
Akitoa wito kwa jamii inayoishi katika mipaka ya nchi jirani na misitu inayotumiwa na wasafirishaji wa magendo na wapitishaji wahamiaji haramu, Kashai alisema mtu yoyote ambaye atabainika kushirikiana na watu hao atafikishwa katika vyombo vya sheria.
                                                           Mwisho

No comments:

Post a Comment