Tuesday, December 30, 2014

KISIWA HARISHI (22)


HADITHI
 
KISIWA CHA HARISHI (22)
 
ilipoishia toleo lililopita
 
“Sidhani kama hapa ni karibu na kwenu Comoro. Mimi nadhani kama tutapata msaada wa kuokolewa tutapelekwa kwanza Zanzibar” nikasema.
 
“Si vibaya Zanzibar pia ni nyumbani lakini baba akipata habari atatuma ndege siku hiyo hiyo ituchukue pamoja na nyinyi”
 
“Itakuwa raha sana tukienda Comoro na kupokewa na rais” nikasema.
 
Shazume alikuwa kimya akitusikiliza. Bila shaka alikuwa anaona tunajidanganya kujifariji. Kwa mawazo yake sisi tulikuwa ni wa kufa tu.
 
“Si unajua mzazi aliyekwishamkatia tamaa mwanawe halafu anaambiwa amepatikana, atafurahije?” Yasmin akaniuiza.
 
“Atafurahi sana”
 
Iliwezekana tulikuwa tulikuwa tunajidanganya kweli kama alivyowaza Shazume lakini tulifarijika. Saa zikapita.
 
Tulipomaliza kula Yasmin alileta storitofauti tofauti kutuondoa katika mawazo mabaya. Tukawa tunazungumza.
 
Aliondoka jioni sana. Tukamsindikizakwa pamoja hadi nusu ya njia, tukarudi. Tukakaa kwenye kile kisehemu chetu kusubiri usiku. Hatukujua nini kitatokea kati yetu usiku huo.
 
SASA ENDELEA
 
Usiku ule tulikesha macho kwa sababu ya hofu. Tulikuwa tumejilaza chini kila mmoja upande wake lakini hakukuwa na aliyelala usingizi. Mara kwa mara nilimuona Shazume akijigeuza kila upande.
 
Ilikuwa kati kati ya usiku Shazume aliposhika mguu wangu. Sikujua kama alikuwa anataka kuniamsha au alitaka kujua nilikuwa macho lakini aliponishika nilishituka nikarusha mguu wangu.
 
“Nini?” nikamuuliza nikiizuia sauti yangu isisikike sana.
 
“Nimebanwa na haja ndogo” akaniambia.
 
“Sasa?” nikamuuliza.
 
“Tunaweza kutoka nikajisaidie”
 
“Haya tutoke” nikamwambia.
 
Shazume akainuka na mimi nikainuka. Akatangulia kutoka kwenye mlango. Kulikuwa giza sana. Hatukuweza kuona kwa mbali.
 
“Twende nje au uani?” Shazume akaniuliza.
 
“Naona tutoke uani” nikamjibu.
 
Shazume akaelekea upande wa uani. Mimi nilikuwa nikimfuata nyuma. Alifungua mlango akachungulia uani. Mwezi ulikuwa unaangaza, ua ulikuwa mweupe. Baada ya kuchungulia kwa tahadhari Shazume alivuka kizingiti cha mlango akatoka uani na mimi nikatoka.
 
Yeye alikwenda upande wake na miminilikwenda upande wangu tukachutama na kujisaidia. Mimi sikuwa na haja ndogo lakini baada ya mwenzangu kuniambiana mimi nikaisikia.
 
Tulipomaliza haja zetu tulirudi ndani tukajilaza tena. Safari hii tulipojilaza tu usingizi ulitupitia tukalala.
 
Wakati nipo usingizini niliota Harishi anatufukuza baada ya kutufuma tukiwa na Yasmin kwenye lile jumba lake. Tukaingia katika chumba kimoja kujificha chini ya mvungu wa kitanda. Muda si muda Harishi akafungua mlango na kuingia mle chumbani kututafuta.
 
Akaona mguu wa Shazume umetokeza chini ya mvungu. Akaushika na kuuvuta. Shazume akawa anapiga kelele kuniita.
 
Kelele hizo ndizo zilizoniamsha. Nikaamka na kuangaza macho. Nikasikia Shazume akiendelea kupiga kelele kuniita lakini sauti yake ilitokea kwa juu, sio pale chini tulipolala. Nikashituka sana kwa kujua kuwa haikuwa ndoto.
 
Nikatazama juu. Kwanza niliona kanzu nyeupe halafu nikaona upanga uking’aa. Nilipoona hivyo nilijisogeza zaidi ndani ya makorokoro na kuendelea kuchungulia.
 
Nilimuona Shazume ameinuliwa juu juu na Harishi. Nikajiambia kumbe ile ndoto ilikuwa ni kweli. Shazume alitolewa mle chumbani. Sikuweza kujua Harishi aliwasili muda gani na kumkamata Shazume.
 
Bila shaka kilichokuwa kimeninusuru mimi, ni kuwa nililala nyuma ya mlango. Harishi alipoingia alimuona Shazume na kumkamata yeye.
 
Ile ndoto niliyoota ilikuwa ya kweli. Harishi alikuwa ametuingilia!
 
Jitihada zetu za kujaribu kumkwepa zilikuwa za bure kwani Harishi alikuwa akitugundua kila tulipokwenda kujificha na sababu ni kuwa alikuwa akifuata harufu zetu kama vile m’bwa.
 
Harishi alipomtoa Shazume ukumbini, nilimsikia Shazume akipiga ukulele mmoja tu “Nakufa!”. Halafu sikusikia kitu tena.
 
Moyo ulikuwa ukinienda mbio na nilikuwa nikihema kwa nguvu kama niliyekuwa nafukuzwa. Tukio hilo lilikuwa la ghafla sana kiasi kwamba nililazimika kujiuliza, kama bado nilikuwa kwenye ile ndoto au kilichokuwa kinatokea kilikuwa kweli.
 
Hofu yangu sasa ilikuwa kwangu. Nilijiua Harishi akimaliza kumuua Shazume ataniingilia na mimi kwani alipoingia humo chumbani alituona tukiwa wawili.
 
Wazo hilo likanifanya nizidi kujisogeza kwenye makorokoro ili Harishi akiingia tena asinione. Lakini muda ulipita. Sikumuona tena Harishi.
 
Nikaendelea kukaa hapo hapo hadi nikaona kunakucha. Nikahisi kwa muda ule Harishi atakuwa ameshaondoka. Nikajiburuza kujitoa kwenye yale makorokoro nilikojiingiza.
 
Nilinyata hadi kwenye mlango nikaufungua na kuchungulia ukumbini. Nilichungulia upande wa mbele na upande wa uani. Niliiona maiti ya Shazume imelala chini kando ya mlango wa chumba tulichokuwemo. Harishi mwenyewe hakuwepo.
 
Nikatoka nje na kuangalia kila upande. Sikuona kitu. Kando ya ile nyumba palikuwa na mti. Nikapata wazo kuwa nipande juu ya ule mti kujificha. Nikaenda kwenye mti huo nikaupanda na kukaa kwenye tawi mahali ambapo nisingeweza kuonekana.
 
Wakati nipo juu ya ule mti nilimuona Yasmin kwa mbali akija. Nikajiambia tuliobaki katika kisiwa kile tulikuwa watu wawili tu, mimi na Yasmin.
 
Sikupenda kujisifu kuwa nilikuwa nina bahati kwa sababu nimenusurika. Nilijua kuwa wakati wangu ulikuwa haujafika. Pengine niliandikiwa niwe wa mwisho kufa.
 
Historia ya kisiwa hicho tangu tulipofika kila siku alikufa mtu. Leo nimeishuhudia maiti ya Shazume, huenda kesho Yasmin ataishuhudia maiti yangu.
 
Yasmin alipofika pale nilimuacha aingie mle ndani. Mara moja nikamuona ametoka akiwa amechanganyikiwa. Bila shaka alikuwa ameshitushwa na maiti ya Shazume.
 
ITAENDELEA KESHO, USIKOSE KESHO NINI KITAJIRI

No comments:

Post a Comment