Thursday, August 25, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU AY 63

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI 63
 
MWANAMKE
 
ILIPOISHIA
 
Aliniambia kwamba siku zote nilikuwa nikiishi naye nikimdhani kuwa ni Shamsa kumbe siye.
 
Hadithi ile ilinishitua sana. Nikamwambia Shamsa.
 
“Nitaaminije kuwa wewe ni Zena na si Shamsa?”
 
“Subiri” Shamsa akanimabia na kuufinika uso wake kwa kanga.
 
“Sasa nifunue hii kanga” Sauti yake ikaniambia.
 
Nikaifunua ile kanga. Nilipomtazama. Nikaona alikuwa ameshabadilika na kuwa Zena. Wakati mimi nimepatwa na mshangao, yeye alikuwa anatabasamu.
 
“Kumbe ni kweli!” nikajisemea.
 
“Je utaendelea kuniogopa tena wakati umeshanizoea?” Zena akaniuliza huku akiendelea kutabasamu.
 
Unadhani ningemjibu nini wakati polisi wameshafika pale hoteli?”
 
“Sitakuogopa tena”
 
“Nimefurahi kusikia kauli yako hiyo”
 
Mara tukasikia mlango unagongwa kwa kishindo. Nikajua walikuwa ni wale polisi. Walikuwa wameshaelekezwa chumba tulichokuwemo.
 
“Sasa Zena tutafanyaje?” nikamuuliza Zena.
 
SASA ENDELEA
 
“Kwanza nataka tukubaliane kitu kimoja”
 
“Kitu gani?”
 
“Utakikubali?”
 
“Nitakikubali, niambie ni kitu gani?”
 
“Nikupeleke kwetu ujinini tukaithibitishe ndoa yetu kabla ya kurudi Tanga”
 
“Sasa tutakwendaje huko Ujinini wakati tutakapotoka  tu ninakamatwa na polisi?”
 
“Mimi ndiye ninayejua, wewe kubali tu ninachokwambia”
 
“Mimi nimeshakubali”
 
Mlango uliendelea kugongwa.
 
“Hawa wako ndani wanatusikia lakini wanaleta jeuri” Tukaisikia sauti ya polisi mmoja akiwambia wenzake nje ya mlango.
 
“Basi acha tuvunje mlango” Tukasikia sauti nyingine ikisema.
 
“Zena mlango unavunjwa!” nikamwambia Zena kwa hofu.
 
Zena akanyanyuka na kuniambia.
 
“Na wewe nyanyuka ushike hayo mabegi yako”
 
Nikayachukua yale mabegi mawili, moja nililipachika begani kwangu na moja nililishika mkononi.
 
Zena naye akalipachika begani begi lake.
 
 
Sasa mlango ulikuwa unavunjwa!
 
“Njoo usimame sambamba na mimi”
 
Nikajisogeza kwake na kuwa naye bega kwa bega.
 
Zena akachora msitari kwenye sakafu kutoka kulia kwenda kushoto. Ulianza kwenye usawa wake ukafika hadi kwenye usawa wangu.
 
Baada ya hapo alinishika mkono akaniambia.
 
“Fumba macho yako”
 
Nikafumba macho.
 
Sasa mlango ulikuwa umeshavunjwa na kufunguka.
 
Nikaona polisi wakiingia kwa vishindo.
 
“Piga hatua haraka uvuke huo mstari niliouchora hapo chini” Zena akaniambia.
 
Nikainua mguu wangu wa kulia kwa haraka na kupiga hatua kuuvuka  mstari huo kabla ya wale polisi kutufikia.
 
“Sasa fumbua macho yako” nikasikia sauti tulivu ya Zena ikiniambia.
 
Nikafumbua macho yangu. Kama ni mshangao, mshangao nilioupata hapo haukuwa na mfano!
 
Hatukuwa tena kwenye kile chumba cha hoteli. Tulikuwa ufukweni mwa bahari! Sikuweza kujua mara moja tulikuwa kwenye ufukwe wa bahari gani.
 
Ulikuwa ufukwe wenye mchanga mweupe na mbele yetu kulikuwa na msitu ulioshiba. Nyuma yetu ndio kulikuwa na bahari.
 
Jua lilikuwa limekuchwa likitoa mionzi ya rangi ya kimanjano iliyokuwa ikimemeta baharini nyuma yetu.
 
Sikuweza kutambua mara moja tulikuwa katika ufukwe wa nchi gani uliokuwa ukipendeza kiasi kile. Ufukwe huo ulikuwa kimya na hakukuwa na chombo chochote kilichokuwa kikionekana baharini.
 
“Tuko wapi hapa?” nikamuuliza Zena.
 
“Ufukweni mwa bahari”
 
“Bahari ya wapi?”
 
“Bahari ya kwetu ujinini”
 
“Mbona tumefika mara moja”
 
“Kawaida. Lakini nilikukimbiza wewe usikamatwe na wale polisi”
 
“Itakuwa bado wako mle chumbani?”
 
“Wapo wanashangaa shangaa lakini wameambilia matupu”
 
Mabegi tuliyokuwa tumechukua tulikuwa nayo vile vile. Begi langu moja lilikuwa begani na jingine lilikuwa mkononi. Na begi alilokuwa amelishika Zena alikuwa bado analo.
 
Nilitupa macho yangu kwenye ule msitu uliokuwa mbele yetu kisha nikamuuliza Zena.
 
“Tunaelekea upande gani?”
 
“Huko unakoona msitu”
 
“Huko ndiko kuna mji wenu?” nikamuuliza.
 
“Mji uko huko. Twende”
 
Kusema kweli wakati wote nilikuwa nimejikaza kiume lakini nilianza kupata hofu tangu Zena aliponiambia kuwa pale tulikuwa katika ufukwe wa ujinini.
 
Pengine ningemuuliza ujinini ipo upande gani katika ramani ya dunia. Katika kusoma kwangu Jeografia kuanzia shule ya Msingi hadi Sekondari sikuwahi kuiona ramani ya ujinini katika upande wowote wa dunia.
 
Lakini niliona swali hilo halikuwa na umuhimu wa kuliuliza wakati ule. Kama kulikuwa na umuhimu ulikuwa ni kumuuliza tulifika pale kwa usafiri wa aina gani? Kama usafiri wenyewe ulikuwa haueleweki hata hiyo ramani ya ujinini inaweza isieleweke.
 
“Tuanze kusonga, bado tuna kipande cha mwendo wa miguu” Zena aliendelea kuniambia huku akitangulia kwenda mbele kuelekea katika ule msitu uliokuwa unatisha.
 
Wakati nikimfuata nyuma nilimuuliza.
 
“Lakini Zena sitapatwa na madhara yoyote huku?”
 
“Madhara kama yapi?”
 
“Mimi najua kuwa majini wengine wanadhuru watu?”
 
“Ni kweli wapo majini wanaodhuru watu”
 
Kukiri kwake kwamba kuna majini wanaodhuru watu kukaniongezea ile hofu yangu.
 
ITAENDELEA kesho usikose hapahapa tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment