Saturday, August 20, 2016

MUHONGO ATAKA MIGODI IREJESHWE KWA WANANCHI





Tangakumekuchablog
Korogwe, WAZIRI wa Nishati na Madini, Sospeter Muhongo, amemuagiza Afisa Madini Mkoa wa Tanga, Zephania Maduhu kuirejesha  migodi ambayo wawekezaji wameshindwa kuiendeleza.
Pia amewaagiza vijana kuunda vikundi kuweza kupata mikopo kwenye taasisi za fedha  na kuweza kuendeleza uchimbaji wa madini kutoka wadogowado hadi kuwa wakubwa  na kuweza kutoa ajira kwa wengine.
Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara juzi kijiji cha Dindira Tarafa ya Bungu, Muhongo alisema kama kuna migodi ambayo wawekezaji wameshindwa kuiendeleza   hakuna sababu ya kuachwa na ni lazima  kurejeshwa kwa wananchi.
Alisema vijana wengi wanakosa ajira ilhali rasilimali zipo pamoja na fursa mbalimbali za kujiletea kipato hivyo kumuagiza afisa madini kupitia upya leseni na mikataba ya wawekezaji wa migodi hiyo.
“Nimesikia kuwa kuna migodi mitano hapa ambayo wawekezaji wameshindwa kuhuisha leseni zao, hii ina maana kuwa wameshindwa na kutuambia kuwa irudi kwa wananchi” alisema Muhongo na kuongeza
“Kama fursa za maendeleo zipo lakini zimekaliwa na watu wachache sisi kama Serikali hatukubaliani nazo na nakuomba wewe afisa madini mwenye dhamana kupitia upya leseni zao” alisema
Alisema Serikali inataka kuona kila mmoja anafanya kazi za kujiletea maendeleo na haitaki kuona mtu anashinda kwenye vijiwe ambavyo havina tija zaidi kuukumbatia umasikini wa kujitakia.
Kwenye mkutano huo wa wananchi, Waziri Muhongo alitoa nafasi za watu kumi kuuliza ama kuhoji kuhusiana na sekta ya Nishati na Madini ambapo wengi walisema migodi iliyopo imefungwa na wao kukosa ajira.
Walisema awali ambapo migodi hiyo ikifanya kazi vijana wengi walikuwa wakipata ajira ambayo  kumuona kijana mitaani akizurura lilikuwa jambo la nadra kijijini hapo.
“Mheshimiwa tumefurahi kukuona na kuja kwetu hasa ukiwa wewe ndio mtibabu  mkuu wa changamoto zetu za nishati na  madini, hapa tumerudi katika umasikini ambao tunajitakia ilhali tumezungukwa na madini” alisema Rajab Mbwana
Alisema migodi toka kufungwa vijana wengi wamejikalia vijiweni na hawana kazi hivyo kumtaka ujio wake kutafuta mwekezaji mwengine ama migodi hiyo kukabidhi wananchi.
                                            Mwisho

No comments:

Post a Comment