Saturday, August 27, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU YA 64

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI
 
MWANAMKE
 
ILIPOISHIA
 
Nilitupa macho yangu kwenye ule msitu uliokuwa mbele yetu kisha nikamuuliza Zena.
 
“Tunaelekea upande gani?”
 
“Huko unakoona msitu”
 
“Huko ndiko kuna mji wenu?” nikamuuliza.
 
“Mji uko huko. Twende”
 
Kusema kweli wakati wote nilikuwa nimejikaza kiume lakini nilianza kupata hofu tangu Zena aliponiambia kuwa pale tulikuwa katika ufukwe wa ujinini.
 
Pengine ningemuuliza ujinini ipo upande gani katika ramani ya dunia. Katika kusoma kwangu Jeografia kuanzia shule ya Msingi hadi Sekondari sikuwahi kuiona ramani ya ujinini katika upande wowote wa dunia.
 
Lakini niliona swali hilo halikuwa na umuhimu wa kuliuliza wakati ule. Kama kulikuwa na umuhimu ulikuwa ni kumuuliza tulifika pale kwa usafiri wa aina gani? Kama usafiri wenyewe ulikuwa haueleweki hata hiyo ramani ya ujinini inaweza isieleweke.
 
“Tuanze kusonga, bado tuna kipande cha mwendo wa miguu” Zena aliendelea kuniambia huku akitangulia kwenda mbele kuelekea katika ule msitu uliokuwa unatisha.
 
Wakati nikimfuata nyuma nilimuuliza.
 
“Lakini Zena sitapatwa na madhara yoyote huku?”
 
“Madhara kama yapi?”
 
“Mimi najua kuwa majini wengine wanadhuru watu?”
 
“Ni kweli wapo majini wanaodhuru watu”
 
Kukiri kwake kwamba kuna majini wanaodhuru watu kukaniongezea ile hofu yangu.
 
SASA ENDELEA
 
“Sasa itakuwaje, si nitakatwa vipande vipande?”
 
Nilipomwambia hivyo Zena akacheka.
 
“Huwezi kukatwa vipande vipande, si uko na mimi. Mimi ndiye mwenyeji wako ambaye nitakulinda wewe”
 
“Utaweza kunilinda Zena?”’
 
“Bila shaka yoyote. Hakuna jini yoyote atakayeniuliza chochote kuhusu wewe. Kwanza ukoo wetu unaheshimiwa sana na mimi najulikana kwamba ni jeuri”
 
Tuliingia katika ule msitu. Tulikuta njia nyembemba tukaifuata. Macho yangu yalikuwa yakiangalia kwenye ile miti.
 
“Hivi hao majini nitawaona kwa macho yangu?” nikamuuliza Zena baada ya kimya kifupi.
 
“Utawaona. Ngoja tutokeze kwenye mji”
 
“Wakoje?”
 
“Wako kama watu tu. Kama utaona tofauti ni ndogo sana. Sisi tunakuwa na maumbo ya kiasili na ya kujigeuza kama binaadamu. Sasa ukimuona jini katika umbo lake la asili ndio atakutishia kidogo lakini baadaye utawazoea”
 
“Kwani tutarudi lini huko Tanga?”
 
“Labda kesho. Nataka nikuoneshe kwa wazazi wangu ili wajue mtoto wao anaishi na nani”
 
Baada ya muda kidogo tuliona tumetokea katika majabali marefu. Yalikuwa mengi na mengine yalikwenda juu yakaonekana kama minara.
 
“Ni kitu gani?” nikamuuliza Zena.
 
“Ndio tumetokea kwenye mji wenyewe”
 
“Mji ndio huu?”
 
“Ndio huo unaouona”
 
“Mnakaa kwenye majabali?”
 
“Hizo ndio nyumba zetu za ghorofa”
 
“Una maana kwamba mle ndani ya ile minara kuna watu?”
 
“Si watu ni majini ndio wanaoishi humo”
 
Nikawa naikodolea macho ile minara. Ilikuwa na matundu kama madirisha ya kuingiza hewa.
 
Hata hivyo ilionesha kama ilikuwa ni kazi ya kale ya kisanaa. Niligundua kuwa yale majabali na ile minara ilikuwa imechongwa na kuwezeha kuwa nyumba za majini.
 
Karibu minara yote ilikuwa na rangi nyeupe kama iloiyopakwa chokaa.
 
Baada ya mwendo mfupi tulitokea katika eneo la wazi ambalo lilionekana kama uwanja mpana. Tulikuta viumbe wengi kama watu wakiwa katika harakati mbali kwenye uwanja huo.
 
Nilimuuliza Zena pale palikuwa ni wapi na wale tuliokuwa tukiwaona walikuwa kina nani.
 
“Hapa ni kwenye gulio. Wale ni majini, wengine wanauza bidhaa zao na wengine wananunua” Zena akaniambia.
 
“Sasa ni bidhaa gani zinazouzwa pale?”
 
“Bidhaa mbali mbali. Bidhaa za vyakula na bidhaa nyinginezo”
 
“Hizo bidhaa wanazipata wapi?”
 
“Zinapatikana humu humu. Bidhaa nyingine zinatoka Bara Arabu, India na hata China”
 
“Hizo bidhaa zinafikaje huku?”
 
“Kuna majini wanaokwenda kununua na kuzileta huku”
 
“Mnatumia pesa gani?”
 
“Kwa huku kwetu pesa si muhimu. Mara nyingi biashara inayofanyika ni ya mali kwa mali. Unatoa kibaba cha mchele, mwenzako anakupa kibaba cha ngano. Lakini wako majini wanaouza na kununua vitu kwa pesa. Pesa zinazotumika ni rupia, real ya uarabuni na pesa za Kichina”
 
“Pesa za Kitanzania hazitumiki”
 
“Hazitumiki”
 
“Kwanini?”
 
“Majini hawaendi kununua vitu kule”
 
Tulikiuwa tumeshalipita lile eneo lakini mimi bado nilikuwa nikishangaa shangaa.
 
Tulikuwa tukipishana na watu mbalimbali ambao Zena aliniambia kuwa walikuwa ni majini.
 
Kulikuwa na wengine waliokuwa wakinitazama kwa macho makali lakini Zena aliniambia nisiwajali.
 
“Labda wananishangaa kuona nimekuja katika mji wenu?” nikamwambia.
 
“Wanakushangaa kwani hawawajui binaadamu? Wewe si binaadamu wa kwanza kufika huku”
 
“Na hao binaadamu wengine wanafikaje huku?”
 
“Wanaletwa na majini wao kufundishwa uganga au kutembea tu. Tena wanakaa muda mrefu hadi wanajua lugha yetu”
 
“Na mimi naweza kuwaona hao binaadamu wenzangu?”
 
“Huku kila mmoja ana lake. Siwezi kujua wako wapi na hao waliowaleta sihusiani nao”
 
Tukafika katika jabali moja lililokuwa na mnara mrefu. Zainush akaniambia kuwa pale ndio kwao.
 
Wakati tunataka kuingia kwenye mlango wa jabali hilo wakaja majini watatu kutupokea. Walikuwa wanawake watupu tena wasichana wadogo. Lugha ya Zena ikabadilika, akawa anaongea kikwao.
 
Walitupokea yale mabegi wakatangulia nayo ndani na sisi tukafuata nyuma. Zena akaniambia kuwa wale walikuwa wadogo zake.
 
“Sisi tuko thelathini, wanawake tuko kumi na saba, waliobaki ni wanaume”
 
“Mko wengi sana. Nyote ni baba mmoja na mama mmoja?”
 
“Baba mmoja na mama mmoja”
 
“Wewe ni wa ngapi kuzaliwa?”
 
“Ni wa saba lakini kwa wanawake mimi ni wa pili”
 
“Hao ndugu zako wengine wako humu?”
 
“Wale wakubwa wana masikani zao zingine. Walioko hapa ni wale wadogo tu”
 
Tukafika mahali ambapo tulikuta pazia zito la rangi nyeupe.
 
ITAENDELEA

2 comments: