Saturday, May 27, 2017

MKUU WA MKOA WA TANGA AWAPA RUNGU TANESCO



Tanga, MKUU wa Mkoa wa Tanga, Martin Shighella, ameliagiza Shirika la Umeme Tanzania Tanesco Tanga, kuzikatia umeme taasisi zote na mashirika ambayo yamelimbikiza madeni ya umeme.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Shighela alisema agizo la Rais Magufuli la kuzikatia umeme mashirika na Taasisi za Serikali linapaswa kuheshimiwa hivyo kulitaka Shirika hilo kuanza mchakato wa ukataji kwa wadaiwa sugu.
Alisema kuna baadhi ya Mashirika na Taasisi zimekuwa zikilimbikiza madeni ya umeme ilhali zimekuwa na bajeti ya umeme hivyo ili kujua umuhimu wa nishati hivyo ni kuzikatia.
“Natoa agizo kwa taasisi za Serikali na Mashirika ya umma kuhakikisha wanalipa umeme kwa wakati na  kuepuka aibu ya  kukatiwa, agizo la Rais linapaswa kuheshimiwa” alisema Shighella na kuongeza
“Rais ametoa agizo la kila mtumiaji wa nishati ya umeme kulipa kwa wakati na yoyote ambaye analimbikiza madeni kukatiwa, sisi ni watendaji kuhakikisha maagizo yake yatekelezwe” alisema
Kwa upande wake Kaimu Meneja wa Tanesco Tanga, Cesilia Msangi, amewataka watumiaji wa umeme Tanga kuhakikisha wanalipa Ankara zao kwa wakati ili kuepuka kukatiwa umeme.
Alisema kwa sasa Shirika hilo linafanya msako wa nyumba moja baada ya nyengine ikiwemo kuwabaini watu waliojiunganishia umeme kwa njia za udanganyifu.
Alisema watu ambao watabainika kujipatia umeme kwa njia za hila watafikishwa mahakamani wakiwemo mafundi vishoka ambao wamekuwa wakilihujumu shirika hilo.
“Kuna baadhi ya watu wamekuwa wakirubuniwa na wafundi vishoka kwa kuwaunganishia umeme, kwa hili hatutakuwa na msamaha zaidi ya kuwafikisha mahakamani” alisema
Aliwataka watumiaji wa umeme kuwa na ada ya kulipa kwa wakati bili zao ili kuepuka malimbikizi ambayo unafika wakati hushindwa kulipa na mwisho wake ni kukatiwa.
Kwa upande wake Meneja Mkuu wa kiwanda cha Maziwa (Tanga Fresh) Michael Karata, amelitaka Shirika hilo kuwapunguzia gharama za umeme kwa watu wenye viwanda.
Alisema gharama ya umeme ni kubwa hivyo kulitaka kuwaangalia wawekezaji na wenye viwanda jambo ambalo litaweza kuongeza ufanisi na uzalishaji wa bidhaa.       
                                                Mwisho     




No comments:

Post a Comment