Monday, May 1, 2017

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 17

ZULIA LA FAKI 0655 340572
 
NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 19
 
ILIPOISHIA
 
“Hakunidanganya. Baba yako alinionesha picha  yake, ndiye yeye  niliyemuona na hata namba ya simu anayotumia ulisema ni yake”
 
“Namba ya simu ni yake kweli, niliikariri  kichwani mwangu”
 
“Basi ndiyo ujue niliyemuona alikuwa ni Ummy kweli”
 
“Sasa mbona hapokei simu?”
 
“Tena mwanzo alikuwa akinipigia yeye, ndiyo nikaipata hii  namba yake”
 
“Basi atakapokupigia tena utakuja kutuambia”
 
Nikaagana na yule msichana. Sikwenda kwao tena. Nikaenda kupanda daladala na kurudi nyumbani.
 
Vile nafika nyumbani tu, simu yangu ikapigwa. Nilipoangalia namba inayonipigia, nikaona  namba  ya Ummy.
 
Nilishituka halafu mwili ulinisisimka.
 
SASA ENDELEA
 
Nikajiuliza niipokee au nisiipokee? Kama nitaipokea msichana huyo atanieleza nini? Nikajiambia chochote ambacho ataniambia kitazidi kuniweka njia panda kwa vile nimeshathibitisha kuwa msichana huyo alikuwa ameshakufa.
 
Vile vile tayari nilikuwa na hofu ya kuzungumza na mtu ambaye kuna ushahidi kuwa alikuwa amekufa.
 
Lakini kwa upande mwingine nilikuwa na shauku ya kumsikia yeye mwenyewe atakachojibu kuhusu madai kuwa alikuwa ameshakufa miaka  mitano iliyopita.
 
Nikajiambia nisipopokea simu yake, bado nitabaki kuwa njia panda kwani sitapata mtu mwingine wa kunipa ufafanuzi kuhusu madai ya kufa kwake.
 
Mbali na hayo, bado nilitaka kujua ni siri gani ambayo alitaka  kunieleza kuhusu mali za babu yangu. Nikaamua kupokea ile simu.
 
“Hello!” Nikasema kwa sauti ya kujikaza ili nisioneshe hofu niliyokuwa nayo.
 
“Hello! Kassim unajua nimekupenda sana, ninataka uwe mume wangu!”
 
Maneno hayo yalinishitua. Niwe mume wa mtu aliyekwisha kufa!
 
“Natumaini kuwa naongea na Ummy?” nikamuuliza.
 
“Mimi ni Ummy Nasri”
 
“Uliniambia nifike nyumbani  kwenu Mwananyamala, nimefika jana na leo lakini sikukuona”
 
“Ulimkuta nani?”
 
“Nilimkuta baba yako mzee Nasri”
 
“Vizuri sana. Alikuambia nini?”
 
“Aliniambia maneno ya kunishitusha sana”
 
“Kama yapi”
 
“Aliniambia kwamba mwanawe anayeitwa Ummy alikwishakufa miaka mitano iliyopita”
 
“Na mimi ni nani?”
 
“Umeniambia kuwa wewe ni Ummy Nasri”
 
“Na uliyembiwa amekufa ni nani?”
 
“Ni Ummy Nasri”
 
“Sasa una shaka gani?”
 
“Kwanza nataka unieleze ni kwanini nimeambiwa kuwa umekufa?”
 
“Kuna umuhimu wa mimi na wewe kukutana”
 
“Kwanza nataka ujibu, kwanini nimeambiwa kuwa umekufa?”
 
“Ndiyo maana nikakwambia kuna umhimu tukutane ili tuzugumzie hilo pamoja na kukueleza kuhusu mali za babu yako”
 
Nikanyamaza kwa sekunde kadhaa nikifukiria la kumjibu.
 
“Lakini ni kweli kuwa ulikufa?” nikamuuliza baada ya kimya kifupi.
 
“Ni kweli?”
 
“Sasa wewe ni nani?”
 
“Ni Ummy”
 
“Umekubali kuwa ulishakufa, sasa mbona uko hai?”
 
“Mimi ni kivuli cha Ummy”
 
“Sijakuelewa. Kivuli maana yake nini?”
 
“Maana yake ni mzuka wa Ummy!”
 
Moyo wangu ulipiga kwa nguvu kisha ukaanza kunienda mbio. Nikahisi mkono ulioshika simu ulikuwa ukitetemeka.
 
“Kassim tutakapokutana kila kitu utakielewa vizuri”
 
“Unadhani nitakutanaje na mzuka?”
 
“Tutakutana tu  na tutazungumza, usijali”
 
“Mmmh…!”
 
Pakapita kimya kingine.
 
“Niambie nikiuone wapi na muda gani?” Sauti ya Ummy ikautanzua ukimya uliokuwepo.
 
“Acha nifikirie kwanza”
 
“Ufikirie nini Kassim?”
 
“Umenitisha. Umeniambia kwamba wewe ni mzuka”
 
“Sasa unataka ufikirie nini?”
 
Sikujibu.
 
“Kassim!” Sauti ya Ummy ikaita kwenye simu.
 
Sikujibu. Nilibaki nimeduwaa kama gogo.
 
“Nitakupa muda wa kufikiria lakini usizidi saa arobaini na nane”
 
“Sawa” nikamuitikia.
 
Ummy akakata simu.
 
Yale maneno ya kwanza ya Ummy kuwa ananipenda na anataka niwe mume wake, yalipita katika akili yangu.
 
Nikajiambia hata wale watu aliowaua kule Buswana. Zimbabwe , Afrika Kusini na hapa Dar, inaelekea walianzana kwenye mapenzi,
 
Kitendo cha kuniambia anataka niwe mume wake si tu kimebadili mada yake ya kwanza ya kutaka tukutane ili anieleze ziliko mali za babu yangu bali pia nilifikiri kwamba ilikuwa ni hatua  ya kutaka kuniua.
 
 
ITAENDELEA kesho hapa hapa usikose ni kitaendelea wa Kassim akiwa katika mtihani mzito wa kusuka au kunyoa
 
 
 
 

No comments:

Post a Comment