Tuesday, May 16, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 27

HADITHI
 
NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 27
 
ILIPOISHIA
 
Mara nikamuona Inspekta Amour akiingia katika  chumba hicho.
 
Alipoona namtazama alimuuliza daktari kama  angeweza kuongea na mimi.
 
“Mnaweza kuzungumza” alipata jibu kutoka  kwa daktari.
 
“Pole sana”  Inspekta akaniambia.
 
“Asante”
 
“Nini kimetokea pale”
 
“Kwa kweli palitokea kitu kama miujiza….”
 
SASA ENDELEA
 
Nilimueleza  inspekta huyo hali iliyotokea pale. Inspekata Amour akashangaa.
 
“Una uhakika  kwamba aliyekupigia simu ni Ummy na alikwambia kwamba utaona?”
 
“Nina  hakika”
 
“Na una uhakika kwamba ulimuona amesimama mbele yako wakati unafika pale hoteli?”
 
“Nina uhakika”
 
“Tangu tulipooanza uchunguzi wa Ummy, namba ya Ummy imetegwa na  kila anapopiga au kupigiwa simu inarekodiwa. Tutakwenda kampuni ya simu ili tuhakikishe kwamba ni namba  ya Ummy iliyokupigia na pia tuhakikishe wakati alipokuwa anakupigia alikuwa karibu na wewe”
 
 
“Nilimuona mbele ya gari akiwa ameshika simu. Nikafunga breki ili nisimgonge. Kumbe nilikanyaga pedeli ya mafuta, nikamgonga. Nilipomgonga alitoweka pale pale, nikaona nimegonga nguzo ya umeme” nikamwambia Inspekta Amour kwa mkazo.
 
“Ni kitu kisochoeleweka lakini nitakwenda kwenye kampuni  ya simu kufanya utafiti. Laiti tungeuona mwili wake uliogongwa tusingepata utata lakini mwili wa Ummy haukuwepo!”
 
“Alitoweka kimiujiza. Yule kweli si binaadamu, ule ni mzuka. Ulitaka  kuniua!” nikasema kwa jazba.
 
“Tulia upate matibabu. Tukio lililotokea ni kubwa”
 
“Nimekuelewa Inspekta”
 
Inspekta huyo  akaniaga na kutoka.
 
Yule daktari pamoja na wauguzi wake nao waliondoka. Akabaki yule polisi aliyekuwa na bunduki ambaye sikujua alikuwa akisubiri nini.
 
Baadaye kidogo  muuguzi mmoja alikuja na chano cha dawa. Akanipa tembe za kumeza kisha akanipiga sindano na kuondoka.
 
Tukio lile lililotokea lilikuwa limeushitua moyo wangu na kuniacha katika hali mbaya. Kila wakati ile picha ya kumuona Ummy akiwa amesimama mbele ya gari huku akiniambia.
 
“Utaona leo...utaona leo!” ilinijia akilini ikifuatiwa na ile picha ya kumgonga kisha ghfla akanipotea na kuona nimegonga nguzo ya umeme.
 
Zilikuwa picha zilizonisisimua na kunitia hofu ya kufa. Kama  nilinusurika kufa pale, nilijua si muda mrefu Ummy ataniua kama alivyowaua  wadaiwa wa babu yangu.
 
Nilijua kikubwa kilichompa hasira ni kugundua kuwa nilishirikiana na polisi kumuwekea mtego wa kumkamata. Bila shaka Ummy aligundua kuwa polisi walitaka  kumkamata ndipo akaona  anikomoe.
 
Sikuweza kujua  gari langu liliharibika kiasi gani na lilikuwa wapi.  Na pia sikuweza kujua ule moto uliendelea kuwaka hadi muda gani  na ulisababisha hasara ya kiasi gani.
 
Laiti ningejua kuwa tukio lile lingetokea, katu nisingekwenda kule  Lux Hotel wala nisingekubali kumuwekea mtego Ummy wakati nikijua fika kuwa alikuwa mzuka.
 
Lakini nikajiuliza,  Mzuka  huo ulikuwa  una lengo gani na mimi?
 
Sikuweza kupata jibu mara moja.
 
Baada ya muda kidogo niliona polisi watatu wa usalama  barabarani ambao walikuja kuchukua maelezo yangu.
 
Walitaka kujua  jinsi ile ajali ilivyotokea, nikawaelezo lakini niliona wazi kuwa polisi hao hawakuamini maelezo yangu yote. Nusu waliyamini lakini nusu hawakuyaamini.
 
Kwamba yule msichana ambaye nilipanga na Inspekta  Amour tumuwekee mtego alitokea mbele ya gari langu na  kisha nikafunga breki na yakatokea yaliyotokea, polisi hao hawakuamini.
 
Lakini walitimiza jukumu lao la kuandikisha maelezo yangu  kama  nilivyoyatoa  wakaniambia niweke saini,  nikaweka  saini.
 
Walipokuwa wanataka kuondoka niliwauliza hali ilivyokuwa baada ya ajali hiyo. Polisi hao walinieleza kwamba ajali hiyo ilikuwa kubwa na kwamba transfoma iliyokuwa katiika nguzo za umeme ililipuka moto na kusababisha nyaya za umeme kutoa cheche za moto na moto kusambaa katika eneo kubwa.
 
Walinieleza kuwa baadhi ya nyaya zilikatika kwa mlipuko na kuanguka chini.
 
Patashika iliyotokea ilisababisha shughuli kusimama kwa  muda katika hotelli ya Lux ambapo wateja walikimbia ovyo kwa hofu.
 
Ile habari nayo ikazidi  kunifadhaisha.  Nikajiambia huo  mpango ulipangwa na polisi, mimi nilifuatisha tu maelekezo ya polisi.
 
Baada ya kupita kama saa nne hivi, Inspekta Amour akarudi tena pale hospitali.
 
“Ni kweli ulivyosema” akaniambia  na kuongeza.
 
“Sauti ya Ummy imenaswa na amesikika akisema “Utaona leo!” Alikuwa akipiga simu kwenye namba yako. Vile  vile mionzi ya simu yake ilionesha kuwa ilirushwa katika mnara mmoja na mionzi ya simu yako. Watu wa kampuni ya simu wameniambia hii inaonesha kuwa  ni kweli mlikuwa karibu au mllikuwa katika  eneo lile lile”
 
Inspekta huyo aliponiambia hivyo nikamuuliza kwa pupa.
 
“Umeamini sasa…umeamini sasa….? Yule msichana ni mzuka! Kama  alikuwa pale, sasa yuko wapi?  Mbona hakuonekana  tena?”
 
Inspekta Amour akanyamza kimya.
 
Nilikaa pale hospitali kwa siku tatu. Polisi aliyekuwa na bunduki alikuwa akibadilishana zamu na mwenzake kila baada ya  saa nane. Baadaye niligundua kuwa polisi hao walikuwa wakinilinda  mimi kwani nilikuwa  chini ya ulinzi.
 
Asubuhi ya siku ya tano nilitolewa hapo hospitali. Nikapelekwa mahakamani moja kwa  moja. Huko nilifunguliwa mashitaka ya kuendesha gari kwa uzembe, kugonga nguzo ya umeme na kusababisha hasara ya karibu shilingi milioni hamsini.
ITAENDELEA kesho hapahapa usikose
 
 
 

No comments:

Post a Comment