Friday, May 5, 2017

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 22

ZULIA LA FAKI
 
NILIKIONA CHA MTO URITHI WA BABU 22
 
ILIPOISHIA
 
“Sasa ulitaka tukusaidieje?” Inspekta huyo akaniuliza baada ya kumaliza maelezo yangu.
 
“Ninaiomba polisi ichunguze kuhusu huyu msichana na ikiwezekana akamatwe ili ajieleze ni nani. Nimepatwa na wasiwasi sana hasa baada ya kuambiwa kuwa alishakufa”
 
“Kazi ya jeshi la polisi nni kulinda  usalama wa raia na mali zao. Vile vile tunashughulikia masuala ya jinai. Kwa vile suala hilo linahusu usalama wako  na linaweza kuingia pia katika  jinai, tutakusaidia  kufanya uchunguzi”
 
“Nitashukuru sana”
 
“Nipatie namba  ya huyo msichana”
 
Nikampatia kachero huyo namba ambayo Ummy amekuwa akinipigia simu.
 
Nilipompa namba ya Ummy aliipiga na kuitega simu sikioni. Baada ya kusubiri kwa sekunde kadhaa aliniambia.
 
“Namba inaita lakini  haipokelewi”
 
Akaiondoa simu sikioni na kuniambia.
 
“Twende huko nyumbani kwao”
 
SASA ENDELEA
 
Dakika chache baadaye, kachero huyo aliyeonekana kuipenda na kuithamini kazi yake alikuwa amenipakia kwenye gari la polisi tukielekea Mwananyamala.
 
Alilisimamisha gari mbele ya nyumba niliyomuonesha. Mzee Nasri alikuwa amekaa barazani kwenye kiti  cha  uvivu akisoma gazeti la lugha ya Kiingeza.
 
Tulishuka kwenye gari hilo tukamsalimia mzee huyo.
 
Baada ya salamu Inspeketab Amour alijitambulisha kwake kabla ya kumuuliza kama alikuwa anafahamu Ummy Nasri.
 
“Namfahamu. Ni mwanagu lakini alishakufa” Mzee akamjibu.
 
“Alikufa lini?”
 
“Alikufa miaka mitano iliyopita”
 
Inspekta Amour alinitazama kisha akayarudisha macho yake kwa yule mzee.
 
“Unamfahamu huyu kijana?” akamuuliza.
 
“Huyu kijana aliwahi kuja juzi akatuambia kuwa alionana na marehemu lakini hilo jambo tulilipinga sana  kwa sababu marehemu alishakufa”
 
“Ana  uhakika  kwamba alikutana na binti yako unayedai kuwa amekufa na amekuja kutoa ripoti  kituo cha polisi hii leo.  Amedai kuwa huyo msichana anamsumbua na kumsababishia hofu kwani kila mara anampigia simu. Hiyo ndiyo sababu tumekuja  kwako ili tupate ukweli”
 
“Ukweli ndio huo niliokueleza  kwamba huyo  binti alishakufa. Sasa sijui  huyo anayemsumbua yeye ni nani”
 
“Huyo msichana amemwambia kuwa yeye ni mzuka wa Ummy”
 
Mzee akatikisa kichwa.
 
“Hakuna kitu  kama hicho”
 
“Namba ya simu anayotumia huyo msichana umewahi kuiona?” Inspekta alimuuliza mzee huyo.
 
“Alituonesha juzi. Binti yangu alikubali kwamba ilikuwa namba ya marehemu lakini  tangu alipokufa hadi leo ni miaka mitano. Mtu mwingine anaweza kupewa namba hiyo”
 
“Una picha za huyo marehemu??”
 
“Picha zipo”
 
“Ningeomba  nizione”
 
Mzee akainuka na kuingia ndani.
 
Baada ya muda kidogo alitoka akiwa na mke wake pamoja na mdogo wake Ummy.
 
Mke wake na  mdogo  wa Ummy walitusalimia wakati yule  mzee akituonesha picha za Ummy.
 
“Ummy mwenyewe ndiye huyu?” Inspekta akauliza.
 
“Ndiye yeye. Picha  zote hizi ni yeye”
 
“Na mna uhakika kwamba alikufa??”
 
“Alikufa, naweza hata kwenda kukuonesha kaburi lake”
 
“Kwanza ningeomba unipatie picha mojawapo kwa ajili ya uchunguzi”
 
“Unahitaji ipi?”
 
Inspekata alichagua picha aliyoitaka. Mzee akaichomoa kwenye albamu na kumpa.
 
“Sasa nipeleke  nikalione hilo kaburi lake”
 
Mzee akatupeleka. Baada ya Inspekata Amour kuliuona kaburi la Ummy alimwambia mzee Nasri.
 
“Kaburi nimeshaliona,  sasa turudi nyumbani”
 
Tukarudi. Mke wa Mzee Nasri pamoja  na binti yao walikuwa wakitusubiri barazani.
 
“Baba kuna mazingara yanafanyika siku hizi.  Unaweza kuambiwa mtu  fulani amekufa kumbe yuko hai. Sisi tulikwenda kwa  mganga tukaambiwa Ummy yuko hai amechukuliwa msukule lakini baba yake amekataa jambo  hilo” Mke wa mzee Nasri akatuambia.
 
“Tukiingiza imani kama hizo tutaharibu uchunguzi. Lakini vyovyote vitakavyokuwa ukweli utabainika muda si mrefu kwamba Ummy amekufa au amechukuliwa msukule. Tutajua tu….”  Ispekta alimwambia.
 
“Huo uchunguzi utakuwa ni muhimu sana kwa sababu hilo jambo limeshaanza kututia wasiwasi” Mke wa mzee Nasri alisisitiza.
 
“Sawa. Hivi sasa tunakwenda  katika kampuni ya simu ili tujue ni nani anayetumia hii  namba ya Ummy”
 
“Naamini utampata mtu aliyezusha huu utata”  Mzee Nasri akatuambia kabla  ya kuagana naye.
 
Tuliondoka na Inspekta Amour hadi katika  ofisi ya kampuni ya simu inayomiliki namba ambayo Ummy amekuwa akinipigia.
 
Baada ya  Amour kujitambulisha aliomba aoneshwe usajili wa namba hiyo.
 
Sekunde chache tu kompyuta ya kampuni hiyo iliutoa usajili wa namba ya Ummy pamoja na picha yake. Kitu ambacho kiliniacha hoi na pengine kilimuacha hoi Inspekta Amour ni kuona kuwa usajili huo ulikuwa na jina la Ummy Nasri na picha ya kitambulisho pia ilikuwa ya Ummy.
 
Ndipo  maswali yalipoanza.
 
“Hii namba ilisajiliwa lini?”  Inspekta Amour akauliza.
 
“Kwa mara ya kwanza namba hii ilisajiliwa miaka sita iliyopita. Baada ya kutumika kwa mwaka mmoja iliacha kutumiwa kwa karibu miaka mitano, tukaifuta”
 
“Baada ya kuifuta nani alikuja kuirudisha?”
 
“Ni mhusika huyo huyo, alikuja mwezi uliopita akaitaka namba  yake. Kwa vile hatukuwa tumeiuza kwa mtu mwingine tukampatia  na hivyo alifanya usajili upya”
 
“Huyo huyo Ummy Nasir ndiye aliyefanya usajili upya?”
 
“Ndiye  huyo huyo kama ambavyo picha yake inaonekana”
 
ITAENDELEA kesho usikose uhondo huu mtamu na mwanana hapo kesho asubuhi na mapema
 
 
 
 

No comments:

Post a Comment