Sunday, May 21, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 29

NILIKIONA CHA MTO URITHI WA BABU 29
 
ILIPOISHIA
 
Akaja  kwenye  ushahidi  wa polisi wa  usalama  barabarani ulioonesha  jinsi ajali ilivyotokea. Akaeleza kuwa pia amekubaliana na  ushahidi huo uliokuwa na vipimo vya polisi ambao walipima  ajali hiyo.
 
Ushahidi wa afisa wa shirika la umeme uliotaja  tathmini ya hasara iliyotokea nao  ulichambuliwa na kukubaliwa.
 
Wakati wote niliokuwa nikisikiliza hukumu hiyo, moyo wangu ulikuwa ukienda  mbio  kama saa.  Na mara moja moja miguu yangu ilikuwa ikitetemeka.
 
Hakimu alipomaliza  kuuchambua ushahidi wa mashahidi  wote alisema  kuwa mashitaka yote matatu  niliyoshitakiwa yalikuwa yamethibitishwa bila  kuacha  shaka  yoyote.
 
“Kutokana na ushidi huo, mahakama hii inakutia  hatiani kwa makosa yote matatu.…”Hakimu aliniambia huku akinitazama.
 
SASA ENDELEA
 
Ingawa nilijua kuwa ningetiwa hatiani, nilishituka. Uso wangu ulionesha wazi kupigwa na butwaa.
 
Sasa hapo ilikuwa ni kutiwa hatiani tu, bado adhabu. sikujua ningekula miaka mingapi. Nikapatwa na kihoro kilichofanya nimkodolee macho hakimu.
 
“Adhabu” Hakimu alisema baada ya kuyageuza macho yake kutoka usoni kwangu na kulitazama jalada alilokuwa akilisoma.
 
“Baada ya kukutia hatiani ninakuhukumu adhabu ya kulipa faini ya shilingi laki tatu au kifungo cha miezi mitatu kwa kosa la kwanza ambalo ni la kuendesha kwa uzembe”
 
Hakimu alipenua ukurasa mwingine akaendelea kusoma.
 
“Pia ninakuhukumu kifungo cha miaka miwili kwa kosa la kugonga nguzo za umeme au ulipe faini ya shilingi milioni kumi”
 
Hakimu alisita akanitazama kabla ya kuendelea.
 
“Kwa kosa la tatu ambalo ni kulitia hasara ya shilingi milioni hamsini shirika la umeme, ninakuhukumu kifungo cha miaka mitatu jela au ulipe faini ya shilingi milioni kumi na tano pamoja na fidia ya shilingi milioni hamsini ambayo unatakiwa uwalipe shirika la umeme”  Hakimu alimaliza kupigilia msumari kwenye moyo wangu. Msumari huo ulikuwa umenimaliza kabisa.
 
Ilikuwa hukumu ambayo sikuitarajia kabisa. Nilijiuliza.
 
“Nitapata wapi pesa hizo za kulipia faini pamoja na fidia ya shilingi milioni hamsini?
 
Hapo ilikuwa ni kukubali tu kufungwa, hakukuwa na jingine.
 
“Kama utaweza kulipa faini na kulipa fidia utakuwa umeepukana na adhabu ya kifungo” Hakimu aliendelea kunifahamisha.
 
“Na kama utatumikia kifungo bado utalazimika kulipa fidia baada ya kifungo chako” hakimu  alimaliza hukumu yake.
 
Nilihisi kijasho chembamba kikinitiririka kwenye uti wa mgongo wangu. Yalikuwa ni matokeo ya joto lililofumka ghafla mwilini  mwangu.
 
Baada ya kusomewa  hukumu hiyo nilikuwa kama niliyepatwa na wazimu. Nilikuwa nikisema peke yangu huku nikiwalaumu polisi hususan Inspekta Amour..
 
“Mshitakiwa utalipa faini na fidia au utatumikia kifungo ambapo utakapomaliza kifungo chako utalazimika kulipa fidia ya shilingi milioni hamsini” Hakimu akaniuliza baada ya kimya kifupi.
 
Sikuwa  na jibu. Akili yangu ilikuwa imeruka. Pakapita  ukimya wa karibu sekunde tatu kabla  ya kuisikia sauti ya mwanamke ikisema.
 
“Mheshimiwa nitamlipia fainii pamoja na fidia ili asitumikie kifungo”
 
Maneno hayo yalinishitua, nikageuza uso wangu kuelekea upande sauti hiyo ilikotokea.
 
Ilitokea kwenye safu za watu waliokuwa wakisikiliza ile kesi. Kulikuwa na msichana mmoja aliyekuwa amesimama akimtazama hakimu. Nikahisi yeye ndiye aliyesema atanilipia faini  pamoja  na fidia.
 
“Hebu tokea hapa mbele” hakimu alimwambia.
 
Msichana huyo alitoka na kusimama karibu na meza ya mwendesha mashitaka. Nilipomtazama vizuri nilishituka nilipogundua kuwa alikuwa Ummy!
 
Alikuwa amevaa wigi lililompendeza na alipachika begani mkoba wa ngozi ya pindamilia uliokuwa umeendana na vazi allilokuwa amevaa.
 
“Hebu rudia ulichosema” hakimu akamwambia.
 
“Nimesema kwamba nitalipa faini na fidia aliyotozwa mshitakiwa”
 
“Umeisikiliza kesi vizuri?” hakimu akamuuliza.
 
“Ndiyo, nimeisikiliza”
 
“Umeisikia na hukumu niliyoitoa hapa?”
 
“Nimeisikia”
 
“Utamlipia faini ya kiasi gani na  fidia ya kiasi gani?”
 
“Kiasi chote kitakachohitajika”
 
“Fidia peke yake ni shilingi milioni hamsini!”
 
“Ninajua  mheshimiwa”
 
“Haya nenda kalipe”
 
Hakimu akamtaka polisi aliyekuwa akinilinda kufuatana na  Ummy pamoja na mimi kwenda kulipa faini na fidia.
 
Sikuamini na sikujua kama Ummy angeweza kulipa kiasi cha pesa kilichohitajika. Lakini katika hali ya kushangaza Ummy alitoa katika mkoba wake  maburungutu ya noti nyekundu ambayo aliyakabidhi kwa karani wa mahakama.
 
Taratibu za kulipa faini na fidia pamoja na kuachiwa huru zilichukua karibu saa moja. Wakati ule Ummy akinilipia pesa hizo  nilijikuta nikimheshimu na kumchukulia kama mkombozi wangu ingawa  ndiye yeye aliyekuwa ameniangamiza.
 
Nilipoachiwa huru na kutoka nje ya mahakama nikakutana na Imspekta Amour, akanipa mkono na kunisalimia.
 
“Pole sana na hongera” akaniambia kwa uso mkavu usio na aibu.
ITAENDELEA kesho hapahapa usikose

No comments:

Post a Comment