Tuesday, May 2, 2017

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI , NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 20

ZULIA LA FAKI 0655 340572
 
NILIKIONA CHA MTO URITHI WA BABU 20
 
ILIPOISHIA
 
Niliendelea kujiambia kama msichana huyo amekiri kuwa ni mzuka, atakuwa ni muuaji tu. Pengine alikuwa na kisasi na  babu yangu ambaye niliambiwa alikuwa mwanamke wake.
 
Nitakutanaje na kuzungumza na mzuka? Nilijiuliza huku nikifikiria niende Mwananyamala nikamjulishe mzee Nasri kuhusu yale maelezo ya Ummy.
 
Hata hivyo upande mmoja wa akili yangu ulinikataza kwenda Mwananyamala kwa vile nilijua yule mzee atapuuza maelezo yangu kwa ile imani yake kuwa Ummy alishakufa na aliyekufa hawezi kurudi tena duniani.
 
Sasa nifanye nini, huyu msichana ataendelea kuniandama?”  nikajiuliza
 
Sikuweza kupata jibu la haraka kwa vile akili yangu ilikuwa imetaharuki. Nilijiambia nitakapotulia na kurudi katika hali ya kawaida, huenda nitajua nitafanya nini.
 
Wakati nazungumza na Ummy nilikuwa nimesimama kwa kutaharuki, nikakaa kwenye kochi na kuendelea kuwaza.
 
SASA ENDELEA
 
Hisia zangu tangu nianze kumfahamu Ummy sasa zilikuwa zimebadilika. Mwanzo nilikuwa nikihisi kuwa Ummy alikuwa binaadamu anayetumia miujiza kuua watu. Nilijua hivyo tangu nilipoanza kumuona kule Botswana.
 
Na hata pale nilipomkimbia katika chumba cha hoteli aliponiita, nilimkimbia kwa hofu  kuwa alitaka kuniua kama alivyowaua wale wadeni wa marehemu babu.
 
Lakini sasa mtazamo haukuwa huo. Hisia zangu zilikuwa upande mwingine kwamba Ummy hakuwa muuaji mwenye miujiza kama nilivyokuwa nikidhani bali alikuwa mzuka wa mtu aliyekwisha kufa  miaka mitano iliyopita.
 
Kama Ummy aliyekufa alikuwa binadamu, huyu Ummy wa sasa si binaadamu tena. Huu ni mzuka kama alivyoniambia wenyewe. Hauna akili ya kibinaadamu. Mara nyingi mzuka  unapotokea unakuja kuua watu halafu unapotea.
 
Niliwaza kwamba mimi pia  nilikuwa katika orodha ya kuuawa na mzuka huo kwani wale waliouawa kwanza walikuwa wako pamoja na mzuka huo kiurafiki wakidhani alikuwa binaadamu mwenzao. Na wote waliuawa katika mazingira ya kimapenzi.
 
Sasa kama mzuka huo wa Ummy umeanza kuniambia kuwa umenipenda, ndio unataka kunitia kamba ili uniue kirahisi.
 
Lakini wakati nawaza hivyo suala la mali za babu lilikuwa likitikisa kichwa changu. Kwanini mzuka huo aliniambia unazijua siri za mali ya babu yangu?.
 
Ilikuwa ni muhimu nikutane naye lakini niliogopa. Huenda hapo tutakapokutana ndio nikauawa hapo hapo.
 
Nikajiuliza niende nikaripoti polisi ili Ummy akamatwe na kuhojiwa? Au, niliendelea kujiuliza, niende kwa mganga ili anieleze ukweli kuhusu kiumbe huyu na nia yake kwangu?
 
Wazo la kwenda polisi sikuafikiana nalo. Nilijiambia polisi hawashughulikii masuala ya mizuka. Ningeweza kudai kuwa huyu msichana anadaiwa kuwa alikufa miaka mitano iliyopita lakini ninamuona na ananipigia simu kutaka nikutane naye.
 
Madai hayo yanaweza kuwavutia polisi wamuandalie mtego  na kumkamata. Lakini nikajiuliza kama Ummy ni mzuka kweli, anaweza kukamatika au ninajidanganya?
 
Wazo zuri, niliendelea kujiambia, ni la kwenda kwa  mganga.  Mganga anaweza  kunitegulia kitendawili hiki.
 
Baadaya kuwaza hivyo nikaamua niende kwa mganga mmoja wakati ule alikuwa akikaa Chanika. Alikuwa mzigua wa Handeni. Alikuwa akifahamiana  na babu na kuna siku niliwahi kwenda kwake nikiwa na babu.  Babu yangu licha ya utajiri aliokuwa  nae alikuwa mshirikina sana.
 
Siku ambayo nilikwenda naye kwa mganga huyo alikwenda kumroga mfanyabiashara mwenzake ambaye naye alikuwa na vituo vya mafuta. Walikuwa wakishindana kibiashara na babu akaamua kuingiza na uchawi.
 
Siku hiyo nakumbuka, mganga alizika mbuzi watatu wakiwa hai kwenye kaburi la mwanamke aliyekufa zamani. Juu ya kaburi pakamwagwa mchanga wa alama za viatu za mfanyabiashara aliyekuwa akishindana na babu yangu.
 
Babu alikuwa ametuma watu kuzitafuta alama za viatu  za mfanyabiashara huyo kwa dau la  shilingi milioni tatu kwa mtu atakayefanikisha kuzipata. Watu hao wakawa wanamuandama mfanyabiashara huyo usiku na mchana mpaka wakafanikiwa kupata alama zake.
 
Alama hizo walizipata aliposhuka kwenye gari na kukanyaga mchanga kabla ya kwenda kulikagua eneo ambalo alitaka kulinunua pale Ubungo.
 
Baada ya mchanga huo kumwagwa juu ya kaburi hilo palikutwa kibao kilichokuwa na jina lake. Baada ya siku saba mfanyabiashara huyo aliaga dunia baada ya gari lake kugongwa na lori la mafuta! Babu akafurahi.
 
Mganga huyo alikuwa mzigua aliyetoka Handeni. Wenyeji wa Chanika walimpa jina la “mashine ya kuua”
 
Tangu kipindi hicho miaka mingi ilikuwa imepita na sikuwahi kwenda kwake tena kwa vile sikuwa na tabia za kwenda kwa waganga wa kienyeji. Hiyo tabia alikuwa nayo  babu yangu.
 
Nikaona niende nikamueleze matatizo yangu nikiamiini kuwa anaweza kunipatia ufumbuzi.
 
Nikaenda  kwa gari langu
  
Nilipofika niliikuta ile nyumba yake ambayo wakati ule ilikuwa ikiendelea kujengwa, ilikuwa imeshakamilika. Lakini nilikuta msururu wa watu.
 
Ikabidi  na mimi nipange msitari. Hadi nafanikiwa kuingia katika chumba chake cha uganga ilikuwa karibu saa kumi na moja jioni. Nilikuwa na matumaini madogo sana kama angelishughulikia suala langu kwa vile  muda ulikuwa umekwenda sana.
 
Mganga mwenyewe alikuwa amenisahau, nikamkumbusha. Mara moja akamkumbuka babu yangu lakini mimi hakunikumbuka.
 
“Wewe ni mjukuu wa yule mzee?” akaniuliza.
 
“Ni mimi lakini babu mwenyewe alishakufa”
 
Mganga akashituka.
 
“Kumbe mzee Limbunga alikufa?”
 
“Alikufa”
 
“Alikufa mwaka gani?”
 
“Alikufa mwaka huu”
 
“Kwa hiyo wewe ndiye umesimamia shughuli zake?”
 
“Ni mimi lakini kuna matatizo yamejitokeza”
 
“Matatizo gani?”
 
“Wewe unajua kuwa mzee Limbunga alikuwa tajiri lakini alipokufa mali zake hazikuonekana”
 
“Kwanini?”
 
“Sijui”
 
ITAENDELEA kesho usikose uhundo huu

No comments:

Post a Comment