Saturday, May 27, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 33

NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 32
 
ILIPOISHIA
 
Nikainamisha uso wangu na kuanza kuwaza kwamba kumbe yule mwanamke aliyekuwa akitusumbua alikuwa jinni na si mzuka wa Ummy.
 
“Nilikuelekeza uende nyumbani kwa kina Ummy uniulizie, lengo langu ni kutaka kukuonesha miujiza. Baada ya Miujiza ile  nilitaka  tukutane nikueleze ukweli lakini ulikuwa ukinikwepa hadi hii leo nilipofanya uamuzi wa kukufuata nyumbani kwako” Maimun aliniambia.
 
Akaendelea. “Najua kilichokutisha ni jinsi nilivyowaua wale  watu kule Botswana, Zimbabwe na Afrika kusini. Wale watu baada ya kugundua kuwa aliyewapa mali alikuwa amekufa walipanga njama za kukuua. Ndipo nilipochukua uamuzi wa kuwaua wao mmoja baada ya mwingine. Wewe hujui tu lakini mimi nipo na wewe tangu babu yako alipofariki”
 
Wakati wote huo nilikuwa kimya nikimsikiliza kwa makini mwanamke huyo.
 
“Nilikwambia kuwa  ninaijua siri ya mali ya babu yako, siri yake ndiyo  hiyo. Utajiri wa babu yako ninao mimi na ninakusudia kukupa wewe. Lakini nisingekupa mpaka nikutane na wewe kama tulivyokutana hii leo na unirithi mimi”
 
SASA ENDELEA
 
Nikainua uso wangu na kumtazama mwanamke huyo huku nikimfananisha na jini. Hakuonesha ishara yoyote ya kuwa jini zaidi ya ile miujiza yake alionionesha siku ile katika eneo la hoteli ya Lux. Ile miujiza pekee ilitosha kunipa  imani kuwa alikuwa jini kweli.
 
“Nikurithi kivipi?” nikamuuliza.
 
“Unirithi kama mke wa babu yako na uendelee kuishi na mimi kama mke wako”
 
“Mimi sijui mlikuwa mnaishi namna gani?”
 
“Tulikuwa tunaishi kama mke na mume. Tofauti ilikuwa mimi ni jini, yeye ni binaadamu”
 
Nilijaribu kuwaza kwamba ninaishi na mwanamke ambaye ni jini nikaona jambo hilo haliwezekani.
 
Nikatikisa kichwa.
 
“Naona kama haiwezekani kuishi na mwanamke ambaye ni jini”
 
“Inawezekana. Mbona babu yako aliweza”
 
“Sijui alikuwa akitumia mbinu gani kuishi na wewe”
 
“Haihitaji mbinu. Tunaishi tu kama mke na mume. Vile ambavyo utamtumia mke wako ndivyo ambavyo utanitumia mimi. Na vile ambavyo mimi nitamtumia mume wangu ndivyo ambavyo nitakutumia wewe”
 
“Unaweza kunipa muda wa kufikiria jambo hilo na kunipa  muda wa kujiandaa”
 
“Ninaweza. Niambie nikupe  muda wa siku ngapi?”
 
“Nipe muda wa wiki moja tu”
 
“Sawa. Nitakupa  muda wa wiki moja. Lakini nitakuwa na masharti yangu  ambayo ni lazima  uyafuate”
 
“Masharti gani?”
 
“Kwanza sitataka ujihusishe kimapenzi na mwanamke mwingine. Pili kila jambo ambalo utalifanya ni lazima utake ruhusa kutoka kwangu. Na mimi kila jambo ambalo nitalifanya ni lazima nitake ruhusa kutoka kwako”
 
“Sawa. Na kuhusu huo utajiri nitaupataje?”
 
“Utaupata wakati tutakapokuwa tumekubalina kuwa wanandoa”
 
“Sawa”
 
Pakapita ukimya wa karibu sekunde kumi. Maimun alikuwa akikikodolea macho chumaba changu.
 
“Sasa mimi nakwenda zangu” akaniambia baada ya sekunde hizo.
 
“Sawa, tutawasiliana”
 
Maimun akainuka kutoka kitandani na kuniambia.
 
“Kwaheri”
 
“Karibu sana”
 
Akageuka na kuelekea kwenye mlango. Alifungua mlango akatoka. Nikainuka na kumfuatia ukumbini. Sikumuona tena. Nilikwenda kwenye mlango wa mbele  nikaukuta umefungwa kwa ndani.  Sikuweza kujua alitoka vipi. Nikarudi chumbani mwangu na kufunga mlango.
 
Nilijitupa kitandani na kuanza kuwaza. Kile kitendawili cha Ummy alikuwa nani, kilikuwa kimeshateguka. Sasa nilikuwa nikifahamu kuwa Ummy ni jini na siye yule Ummy tuliyekuwa tukimdhania aliyekuwa amezikwa kaburini.
 
Kile kitendo cha kuvaa sura ya Ummy ndicho ambacho kilinichanganya na kumdhania alikuwa mzuka wa Ummy.
 
Sasa suala la Ummy ni nani lilikuwa limeshapata jibu. Ummy ni jini na jina lake ni Maimun binti Hashhash. Suala sasa ni la kufikiria kuishi na mwanamke huyo kama mke na mume.
 
Awali sikuwa nikijua kama babu yangu alikuwa  na mke wa kijini. Kwa vile nilikuwa nikiishi Morogoro sikuwahi kumuona  hata  siku moja  na babu yangu hakuwahi kuniambia. Jambo hilo alilifanya kuwa siri yake.
 
Sasa babu ameshakufa, nilijiambia, jini huyo amenifuata mimi na ametaka  nimrithi.
 
Amenipa siku saba  za kufikiria ama kumkubalia ama kumkatalia.
 
Nikajiuliza endapo nitakubali kumrithi Maimun na kuwa mke wangu faida yake itakuwa ni nini?
 
Jibu nililipata mara moja.  Faida yake  ni  moja tu, kupata utajiri ambao kila mwanaadamu katika ulimwengu huu anauwania.
 
Nikimrithi Maimun nitakuwa tajiri. Nitaishi katika  jumba la kifahari na nitakuwa na gari kama sio magari ya gharama. Vile vile nitaishi maisha ya hali ya juu.
 
Na je kama sitataka kumrihi athari yake itakuwa nini? Nilijiuliza.
 
Jibu hilo lilipaswa litolewe na Maimun mwenyewe lakini nililijibu mimi kwamba endapo sitamrithi Maimun sitapata utajiri. Nitendelea kuishi katika umasikini. Hilo  ndilo jibu la haraka haraka nililolipata.
 
Usiku ule nilikesha macho nikiwaza hadi asubuhi. Wazo ambalo niliamka nalo ni la kwenda kwa yule mganga wa marehemu babu aliyeko  Chanika ili anipe ushauri  wake.
 
Ilipofika saa nne nikaliwasha  gari na kwenda Chanika kwa yule mganga.
 
Nilipofika nyumbani kwake nilimkuta akikatakata vipande vya mzizi.
 
“Habari za siku nyingi?” akaniuliza.
 
“Nzuri. Habari za hapa?”
 
“Hapa ni kwema. Karibu sana”
 
“Asante. Niimekuja nina  tatizo moja. Nataka kupata ushauri wako”
 
“Tatizo gani hilo?”
 
Nikamueleza kuhusu yule jini aliyekuwa mke wa babu yangu.
 
Baada ya kumpa maelezo yangu mganga alishituka  na kushngaa. Akaacha kukatakata vipande vya mizizi.
 ITAENDELEA ksho usikose
 

No comments:

Post a Comment