Thursday, May 18, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 28

ZULIA LA FAKI
 
NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 28
 
ILIPOISHIA
 
Kwa kweli nilishangaa kuona polisi wamenigeuka na kunifungulia mashitaka. Maelezo yalikuwa yamegeuzwa. Badala yake nimeshitakiwa kwa kuendesha kwa uzembe wakati  hapakuwa na uzembe wowote. Kilichotokea kilikuwa miujiza tu.
 
Kadhalika  nilikuwa nimemgonga Ummy na polisi wamekwenda kampuni ya simu na kuthibitisha kuwa Ummy alinipigia simu na alikuwa  mbele ya gari langu lakini hakutajwa kuwa nilimgonga.
 
Inspekata Amour sikumuona tena. Kweli polisi hana  rafiki.  Anakuwa rafiki yako pale anapotaka lake.
 
Baada ya kusomewa  mashitaka  hayo  na kuyakana, upande wa mashitaka ulisisitiza kuwa nisipewe dhamana kwa sababu ninaweza kuingilia na kuharibu uchunguzi wao kwani uchunguzi wa tukio hilo ulikuwa bado unaendelea.
 
Nikapelekwa rumande.
 
Ile  kesi iliendelea kuunguruma kwa miezi minne. Wakati wote  huo  nilikuwa nimewekwa  mahabusi.  Japokuwa uchunguzi wa polisi ulikuwa umekamilika, nilinyimwa dhamna kwa madai kuwa hasara niliyoisababisha ni kubwa na ningeweza kutoroka  kama  nitaachiwa kwa dhamana.
 
SASA ENDELEA
 
Inspekta Amour alikuwa ndiye shahidi wa kwanza aliyekuja kutoa ushahidi dhidi yangu. Aliieleza mahakama kuwa alinifahamu nilipokwenda katika kituo cha polisi anachofanyia kazi na kuripoti kuhusu msichana anayeitwa Ummy ambaye alikuwa ananisumbua.
 
Alieleza kuhusu uchunguzi wake na jinsi alivyogundua kuwa msichana huyo alikuwa ameshakufa lakini kulikuwa na vielelezo na ushahidi kuwa alikuwa hai.
 
“Kwa vile tulitaka  kumkamata tulimwambia mshitakiwa kuwa atakapopigiwa simu na msichana huyo apange naye mahali pa kukutana na atuarifu ili twende tukamkamate” Alieleza Inspekata Amour.
 
Huku akiongozwa na Mwendesha Mashitaka, Amour aliendelea kueleza jinsi nilivyowaarifu kuwa Ummy alinipigia simu na nilipanga kukutana naye katika goteli ya Lux saa nne asubuuhi ambapo Amour aliandaa mtego wa kumkamata msichana huyo.
 
Lakini wakati polisi wanajiandaa kwenda hukohoteli ya Lux ndipo walipopata taarifa ya ajali ya gari iliyogonga nguzo ya umeme na kusababisha moto mkubwa kuwaka.
 
“Tulipofika hapo hoteli tulikuta aliyesababisha ajali hiyo alikuwa mshitakiwa. Tulikuta gari lake likiwa pembeni mwa nguzo zilizokuwa zinawaka huku mwenyewe  akiwa amezirai. Tukafanya jitihada za kuokoa  maisha yake” Inspekta Amour alisema.
 
Aliendelea kueleza kuwa baada ya kufanikiwa  kunitoa kwenye gari na kunipakia kwenye gari la hospitali, kikosi cha zima moto kiliendelea na jitihada ya kuuzima moto  huku wafanyakazi wa shirika la umeme wakiwa wameingia kazini kuzima umeme katika  eneo hilo.
 
“Uchunguzi wetu umeonesha kuwa ajali ile ilitokana na uendeshaji wa kizembe wa mshitakiwa ambaye bila kuwa muangalifu na kujali sheria za usalama barabarani aligonga nguzo za umeme zilizokuwa zimebeba transfoma na kusababisha mlipuko wa moto” Inspekta Amour alimalizia hivyo maelezo yake.
 
Baada ya inspekta Amour, alikuja polisi wa usalama barabarani ambaye alionesha vipimo vya jinsi ajali ilivyotokea na kueleza kwamba niliacha njia sahihi na kwenda kugonga nguzo za umeme.
 
Shahidi mwingine alikuwa afisa mmoja wa shirika la umeme ambaye alieleza kuwa kugongwa kwa nguzo za umeme kulisababisha transfoma ya shirika hilo kulipuka  na  kuwaka moto.
 
Afisa huyo aliendelea kueleza kuwa hasara waliyoipata kutoka na tukio hilo ilifikia shilling milioni hamsini.
 
Wakati mashahidi hao wakitoa ushahidi wao, kichwa kilikuwa kinaniuma na kilikuwa kizito  kwa mawazo yaliyochnaganyika  na fadhaa hasa nilipowaza kwamba  kesi  ile  ingenifunga  miaka  mingi.
 
Baada  ya mashahidi  hao  kutoa ushahidi wao, kesi iliahirishwa  na kupangiwa tarehe nyingine  ya usikilizaji.
 
Nilirudishwa mahabusi ambako  niliendelea kusota na  kuwazia  maisha yangu ambayo niliona  yalikuwa yameshafikia kikomo kwani nilijjua kuwa nitafia jela.
 
Tarehe ya kuendelea kwa kesi hiyo ilipowadia nilipelekwa mahakamani nikiwa  na hali mbaya ya kiafya kwani nilikuwa nimekonda. Kule  mahabusi nilikuwa sili chakula vizuri kutokana na fadhaa.
 
Vile vile nilikuwa nikimlaani Inspekta Amour aliyekuwa amenigeuka ili kulinda kazi yake. Amour alifahamu fika  kuwa ajali ile  ilitokea kimiujiza na si mimi niliyeisababisha lakini  alitoa maelezo ya kunitia  katika hatia.
 
Kesi iliendelea kwa mashahidi mbalimbali kuja kutoa ushaidi wao. Katika kipindi chote wakati  ushahidi unatolewa nilipewa nafasi ya kuuliza  maswali kama kulikuwa na kitu sikubaliani nacho. Lakini ukweli ni kwamba nilishindwa kuuliza chochote.
 
Nilishindwa kwa sababu ya kutojua sheria na pia kupatawa na hofu.
 
Pale nilielewa ni kwanini hata wanasheria wanapokabiliwa na kesi wanaweka mawakili wa kuwatetea. Ni kwa sababu wao wenyewe licha ya kujua sheria wasingeweza kujitetea vizuri kwa sababu ya hofu.
 
Baada ya upande wa mashitaka kumaliza kuleta mashahidi wake, hakimu alisoma muhutasari wa kesi na kueleza kuwa nina  kesi ya kujibu, kwa hiyo nilitakiwa nijitetee.
 
Niliulizwa  kama  nilikuwa na mashahidi, nikajibu kuwa sikuwa na shahidi yeyote.
 
Baada ya kujibu  hivyo nilitakiwa niandae utetezi wangu ili kesi itakapoitishwa tena  niweze kujitetea.
 
Baada ya hapo kesi ikaahirishwa na kupangiwa tarehe nyingine.
 
Siku hiyo ilipofika nilipelekwa tena mahakamani ambako nilijitetea kwa kuieleza  mahakama  kuwa tukio lile la ajali lilitokea kimiiujiza na kwamba ajali ile sikuisababisha mimi.
 
Hakimu aliandika maelezo yangu na kupanga  tarehe ya kutoa hukumu.
 
Usiku wa siku ile ya kutolewa hukumu niliota ndoto  mbaya sana. Niliota ninahukumiwa kifungo cha miaka thelathini jela na kutakiwa nililipe shirika la umeme shilingi milioni hamsini.
 
Nilikuwa sina pesa hizo nikajikuta nimetupwa jela. Baada ya kusota jela  kwa mika thelathini, eti nikaona ninatoka jela nikiwa mzeee ninayetembea kwa mkongojo!
 
Ndoto ile ilinishitua sana nikajua ndio  mambo yatakavyokuwa.
 
Asubuhi nilipelekwa mahakamani kwenda  kusikiliza hukumu yangu.
 
Jalada langu lilipoitishwa  nilipanda kizimbani na hakimu akanisomea hukumu aliyokuwa ameniandalia.
 
Alianza kuyataja mashitaka yaliyokuwa  yananikabili na akaeleza  kuwa niliyakana mashitaka yote niliyosomewa.
 
Baada ya hapo akaanza kuuchambua ushahidi uliokuwa umetolewa na upande wa mashitaka.  Alianza kuuchambua ushahidi  wa Inspekta Amour.
 
Akaeleza kuwa ushidi huo anaukubali kwa vile mimi kama mshitakiwa nilishindwa kumhoji shahdi huyo chochote ikimaanisha kuwa  nilikubaliana nao.
 
 ITAENDELEA kesho hapahapa Usikose

No comments:

Post a Comment