Wednesday, May 10, 2017

NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 25

ULIA LA FAKI
 
NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 24
 
ILIPOISHIA
 
Macho ya  watu wote  yakaelekea kwenye mwili huo. Polisi hao waliufungua uso wa marehemu huyo. Ingawa ngozi yake ilikuwa nyeusi kwa sababu ya kukaa ndani ya kaburi kwa muda mrefu haikuwa imeharibika.
 
Uso wake ulikuwa mwembamba na uliosinyaa lakini haukunizuia kugundua kuwa ulikuwa na sura ya Ummy.
 
“Hebu mtazameni, huyu ndiye maiti wenu?” Inapekta Amour akawauliza wazazi wa Ummy.
 
“Ndiye yeye”  Mzee  Nasri akajibu haraka.
 
Polisi mmoja  aliyekuwa na kamera ya kuchukua alama za vidole alipiga picha alama za viganja vya Ummy. Polisi mwingine aliupiga picha uso wake. Daktari naye aliuchunguza mwili huo  na kukata kipande cha ngozi yake ya mkono.
 
Baada ya uchunguzi huo kumalizika, mwili huo ulirudishwa kwenye kaburi na kufukiwa tena
 
Daktari akawambia watu kwamba atakuwa na matokeo kamili ya uchunguzi wake baada ya saa sita.  Polisi walioupiga picha  mwili huo wakasema watakamilisha uchunguzi  wao baada ya saa tatu.
 
Tukaondoka.
 
SASA ENDELEA
 
Inspekta Amour alinirudisha nyumbani kwangu akanitaka nifike kituo cha polisi asubuuhi ya kesho yake ili nionanne naye.
 
Baada ya kuagana naye, Inspekta huyo aliondoka. Niliridhika sana na hatua alizochukua. Alikuwa ni miongoni mwa makachero wa polisi niliowakubali sana. Alikuwa akitambua wajibu wake  kama polisi  mpelelezi.
 
Hata hivyo bado niliona kitu kama ukungu katika uchunguzi huo wa polisi. Dalili kwamba huenda tukajikuta tupo njia panda katika uchunguzi huo ni kule kukuta maiti ya iliyoonekana kuwa ni ya Ummy kwenye kaburi lililofukuliwa.
 
Nilijiambia kama itathibitika kuwa aliyezikwa ni Ummy Nasir, moja kwa moja yule msichana anayenipigia simu atakuwa ni mzuka wa Ummy na ndio uliokwenda kusajili namba ya simu kwa ajili ya kunipigia mimi.
 
Na kama itathibitika kwamba  yule si Ummy, basi Ummy atakuwa yupo hai  na ndiye  aliyeuawa watu waliokuwa wakidaiwa na babu yangu, na ndiye  huyo  huyo aliyekwenda kusajili namba ya simu.
 
Kwa vyovyote itakavyokuwa, niliendelea kujiambia, huenda Ummy huyo asiwe na nia njema na mimi. Kama amedai anaijua siri ya mali ya babu yangu huenda anataka kuniua ili aweze kumiliki mali hizo.
 
Shaka hii ilinijia baada ya kuona ameshaua watu waliokuwa wanadaiwa na babu yangu bila kueleweka dhamiri yake ilikuwa nini.
 
Lakini kama utakuwa ni mzuka, suala litakuwa zito  zaidi.
 
Usiku wa siku ile sikupata usingzi kwa kuwaza. Niliwaza mengi yaliyonikera moyo  wangu lakini  hatimae kulikucha salama.
 
Saa tatu asubuhi nikawasili kituo cha polisi cha Kinondoni na kuonana na Inspekta Amour.
 
Inspekta Amour alinikaribisha kwenye kiti akaniuliza.
 
“Yule msichana hajakupigia simu?”
 
“Hajanipigia”
 
“Tumeanza kupata utata kuhusu suala lake. Tumefanya uchunguzi wa kutosha jana na leo lakini matokeo yamekuwa ni ya kutia shaka”
 
“Kwanini?”
 
“Uchuguzi wa madaktari wa Muhimbili kwa kutumia chembechembe za mwili wa marehemu na vielelezo vingine umebaini kuwa ule ulikuwa mwili wa Ummy…”
 
Nilikuwa niimemkodolea macho Inspekta huyo kumsikiliza. Akaendelea.
 
“Sasa utata unakuja kwa sababuni  hata uchunguzi tuliofanya sisi unaonesha kuwa mtu anayekupigia simu ni Ummy huyo huyo ambaye ameshakufa. Alama zake za vidole zilizoko katika usajili wake  na alama tulizozichukua jana katika  viganja vyake zinafanana. Hii inaonesha kuwa ni Ummy huyo huyo!”
 
“Una maana kwamba alama za vidole za watu hazifanani?”
 
Inspekta Amour akatikisa  kichwa.
 
“Alama za vidole za binaadamu hazifanani kabisa. Kila mtu ana alama zake”
 
“Hata kama  watachunguzwa watu milioni moja, watakutwa na alama za vidole tofauti?”
 
“Hata watu milioni kumi, wanaweza kufanana sura tu lakini alama  zao za vidole hazifanani. Kila binaadamu anakuwa na alama zake mwenyewe”
 
“Hicho ni kitu cha ajabu sana”
 
“Ndiyo  maumbile yetu binaadamu. Na wataalamu waligundua hilo. Ndiyo maana alama za  vidole zimekuwa kielelezo muhimu cha kumkamatisha mhalifu”
 
“Mungu ni muweza sana”
 
“Unaiona ile  mistari ya pundamilia?”
 
“Ndiyo,  niimeshawahi kuiona”
 
“Unaweza kuiona kama inafanana lakini ile pia  haifanani. Kila  punda milia ana  aina yake ya mistari, hata wawepo pundamilia milioni kumi, watakuwa na mistari tofauti”
 
“Hilo sijawahi kulisikia”
 
“Ndiyo  nakueleza mimi ili uone maajabu ya Mungu, si katika alama za vidole za binaadamu tu bali tofauti zipo hata katika alama za wanyama”
 
“Nimekuelewa Inspekta. Sasa hili suala la Ummy unalifikiriaje?’
 
“Ndiyo nilikuwa nataka kukueleza kwamba limekuwa suala  lenye utata. Mtu ambaye imethibitika kuwa amekufa na kuzikwa miaka mitano iliyopita lakini kunakuwepo na ushahidi kuwa yuko hai. Hili jambo ni la ajabu sana”
 
“Niliwahi kukwambia kwamba inawezekana kuwa ni mzuka wa Ummy”
 
“Suala hilo la kiimani hatuwezi kuliingiza  katika uchunguzi. Kazi yetu haiamini kuwepo kwa mizuka”
 
“Sasa atakuwa ni nani yule?’
 
“Siwezi kusema ni nani kwa sababu hatujamthibitisha ila wewe utakuwa ni nguzo muhimu katika  uchunguzi wetu  wa awamu ya pili.  Nisikilize kwa makini”
 
“Ndiyo”
 
“Wakati wowote atakapokupigia simu, kubali kukutana naye halafu tupigie simu ili tufike  mahali hapo. Pale mtakapokutana tu tunamkamata hapo hapo”
 
“Nafikiri hilo litakuwa wazo zuri. Hapo mwanzo nilikuwa sitaki kukutana naye kwa sababu ya hofu lakini kama polisi mtakuja nitaweza kukutana naye”
 
“Tutakuja.  Muulize angependa mkutane wapi”
 
“Mara nyingi anapenda tukutane mahotelini”
 
“Basi muache ataje yeye hoteli ambayo angependa mkutane”
 
ITAENDELEA kesho hapa hapa tangakumekuchablog usikose uhondo huu mwanana

No comments:

Post a Comment