Thursday, December 18, 2014

WALALAMIKIA UGUMU WA MAISHA

Kumekucha blog

Tanga,WAZAZI na walezi Tanga wamelalamikia hali ngumu ya maisha baada ya bidhaa nyingi kuwa bei juu vikiwemo vifaa vya shule kwa wanafunzi na hivyo kuitaka Serikali kupunguza wingi wa kodi ili kupata unafuu kwa baadhi ya mambo.

Wakizungumza wakati wa soko la Jumanne uwanja wa Tangamano, baadhi ya wazazi hao walisema kukithiri wingi wa kodi imekuwa chanzo cha maisha kuwa magumu na kuwapa kichwa wafanyabiashara kupandisha  bidhaa zao.

Walisema kipindi hiki cha kuelekea shule kufunguliwa wamedai vitu vingi viko bei  juu jambo ambalo kwa wazazi wenye vipato vya chini kushindwa kumudu mahitaji ya watoto wao ikiwemo vifaa vya shule na ada.

“Kipindi hiki ni cha heka heka kuelekea sikukuu ya krismass na kufunguliwa shule---hapa kila ukionacho hakinunuliki na hii ni sababu ya kuwepo kwa utitiri wa kodi” alisema Abdalla Zubeir

“Ukizihesabu kodi za nchi yetu utachoka nijuavyo kuna kodi moja tu ndio iliyoondolewa ambayo ilikuwa ikijulikana kama kodi ya kichwa---mfanyabiashara analipa kodi hadi nyengine anazisahau” alisema

Alishauri Serikali kuwapatia maisha bora Watanzania kwa kupunguza wingi wa kodi hizo kwa kuamini kuwa kupanda kwa bidhaa madukani na masokoni na maisha kuwa magumu inatokana na kodi kuwaelemea wafanyabiashara.

Kwa upande wake mzazi mkazi wa Mikanjuni, Fatma Athuman, ameishauri Serikali kudhibiti mfumo wa bei madukani kwani kitu kinachofanyika kwa sasa ni ulanguzi na hivyo kutaka kuweko kwa utaratibu wa bei moja.

Alisema kutokuwepo udhibiti wa bei imekuwa chanzo cha kila mfanyabiashara kuwa na bei yake jambo ambalo limekuwa likiwaumiza wananchi hasa masikini na kushindwa kukamilisha kwa baadhi ya mambo.

Alisema uhuru walionao wafanyabiashara umekuwa ukiwaumiza wananchi masikini hasa vipindi vya sikukuu na kuelekea kufunguliwa kwa shule na hivyo kuitaka Serikali kuchukua hatua madhubuti.

“Kila mfanyabiashara yuko na bei yake kitu ni kilekile iweje huyu yuko na bei hii na  yule yuko na bei ile-----huku ni ukandamizaji na kudidimizana katika dimbwi la umasikini jamani” alisema Fatma

Kuelekea vipindi vya sikukuu na ufunguaji wa shule, mzazi huyo amewataka wafanyabiashara kuacha kupandisha bidhaa zao kwa tamaa ya kujipatia pesa kwa njia za kiulanguzi jambo ambalo ni kosa na dhambi.

                                                        Mwisho

No comments:

Post a Comment