Monday, December 8, 2014

HADITHI, KISIWA CHA HARISHI

SIMULIZI
 
KISIWA CHA HARISHI (5)
 
ILIPOISHIA TOLEO LILILOPITA
 
“Sasa unamuitaje?”
 
“Alinipa chupa. Mnaiona ile chupa iliyopo juu ya kabati? Chupa ile iko wazi. Kifiniko chake kipo pembeni. Ameniambia nisiifunge. Anapotaka kuja ile chupa inajaa moshi halafu inavuma. Ule moshi ukishajaa unatoka kwenye mdomo wa ile chupa na kuundaumbile la jinni halafu anakuwa jinni kabisa.
 
“Sasa nikitaka kumuita nachukua ile chupa naiweka naiweka karibu na mdomo wangu kisha nataja jina lake mara tatu, hazitapita dakika mbili chupa itajaa moshi. Moshi ule utatoka kwenye mdomo wa chupa na kugeuka Harishi”
 
“Sasa kama anakuja kila wiki tutapata muda wa kuishi na pengine tunaweza kupata msaada kwani tutakwenda kukaa fukweni kusubiri vyombo vinavyopita” nikamwambia Yasmin
 
“Jaribuni hahati yenu. Nawaombe Mungu awasalimishe” Yasmin alituambia kwa ungonge.
 
Nikawambia wenzangu. “Jamani maneno mmeyasikia. Hapa hapakaliki”
 
“Sasa tuondoke” Mtu mmoja akauliza.
 
“Inabidi tuondoke tusalimishe maisha yetu”
 
“Sasa tutakwenda wapi?” Mwingine akauliza.
 
“Twende ufukweni tuangalie vyombo vinavyopita, tunaweza kupata msaada”
 
“Sasa huyu msichana naye  tumchukue?” Mtu mwingine naye akauliza.
 
SASA ENDELEA
 
“Itakuwa ni jambo zuri tukimchukua kama mwenyewe atakubali” nikawambia wenzangu kish nikamtazama Yasmin.
 
“Bibie unaonaje kama tutakuchukua ili tukunusuru?” nikamuuliza yasmin.
 
“Kunichukua mimi hakutakuwa nusura kwangu wala kwenu kwa sababu mpaka sasa hamna uhakika wa usalama wenu hata kama mtakwenda ufukweni mwa bahari kusuiri vyombo vinavyopita” Yasmin akatuambia.
 
“Kwanini unatuambia hivyo?” nikamuuliza.
 
“Kwa sababu Harishi anaweza kututoke hapa hapa na kutuua sote kwa hasira’
 
Sote tukagunana kutazamana. Yasmin aliendelea kutuambia.
 
“kwanza akija hapa nyumbani hata kama mtakuwa mmeshaondoka atasema anasikia harufu ya binaadamu na atataka kujua ni nani aliyeingia humu na itakuwa ni balaa kubwa”
 
“Sasa unatushauri nini?”  nikamuuliza Yasmin katika hali ya kukata tama.
 
“Nawashauri muondoke ndani ya jumba hili. Mwende popote mtakapoona mtaweza kujiokoa. Mimi niacheni hapa hapa”
 
“Sawa. Basi sisi tunondoka”
 
Yule msichana kwa kuonesha wema na ukarimu alituambia tumpishe mle chumbani avae nguo. Tukatoka ukumbini. Yasmin alipovaa alitoka akaenda jikoni. Akachukua vyakula na kututilia ndani ya mfuko.
 
“Sasa nendeni, msikae karibu kabisa” akatuambia.
 
Tukamuaga na kutoka. Tukaanza kutembea haraka haraka kwa kufuata ile njia tuliokwendea.
 
Kisiwa kilikuwa kimya na kilichokuwa kinatisha. Kelele zilizosikika zilikuwa ni za kunguru waliokuwa wakilialia na kurukaruka kwenye miti kama waliokuwa wakiambizana “Hao! Hao! Hao!”
 
Tulikuwa tukiangalia huku na huku kwa hofu ya kutokewa na Harishi. Kuwa na silaha katika mazingira yale ilikuwa muhimu. Mimi  nilikuwa na sime niliyokuwa nimeichomeka kiunoni. Wenzangu wawili walikuwa na mapanga. Wenzetu wengine walikuwa mikono mitupu.
 
Kwa sababu ya hofu iliyosababishwa na kelele za wale kunguru nilitoa sime yangu na kuishika mkononi. Sasa nikawa tayari kukabiliana na chochote kitakachotokea.
 
Mpaka tunatokea kule ufukweni mwa bahari tulizungukazunguka sana kwani tulikuwa tunapotea njia mara kwa mara. Kulikuwa na mti mkubwa ulioota kando ya bahari. Tukakaa chini ya ule mti.
 
Tulitoa vyakula tulivyopewa na Yasmin na kuanza kula. Vilikuwa vhyakula vizuri vikiwa mchanganyiko wa mikate ya mayai, keki, sambusa na biriani.
 
Wakati tunakula mawazo yangu yalikuwa kwa yule msichana. Kwa kweli nilimuhurumia sana kwa kuishi maisha ya peke yake katika kisiwa kile cha kutisha. Laiti ningekuwa na uwezo wa kumuokoa ningemuokoa lakini ndio hivyo hatukuwa na uwezo na bado sisi wenyewe pia hatukuwa na uhakika wa maisha yetu.
 
Hata hivyo nilimsifu kwa kuwa na moyo wa kijasiri na wa kiume kwani asingeweza kuishi na kuendelea kuwa hai hadi leo wakati yuko kwenye jinamizi la mauti. Kuishi na jini anayeua watu peke yake lilikuwa ni jinamizi la mauti mbali ya kule kuishi peke yake katika kisiwa kile kinachotisha!.
 
Nikajiambia kama chombo chetu kingekuwa kizima tungeondoka naye hata kama angekataa.
 
Baada ya kula kile chakula tulipata akili tukaanza kujadiliana.
 
“Sasa tufanye nini jamani?” Mwenzetu mmoja akauliza.
 
“Tuijaribu tena ile boti, inaweza kukubali” nikatoa wazo ambalo lilikubaliwa na wenzangu.
 
Tukaenda kwenye chombo chetu tukajaribu kukiwasha lakini chombo hakikuwaka. Kila mmoja wetu alijaribu kukiwasha kwa mkono wake. Hakukuwa na yeyote aliyefanikiwa.
 
Tukaamua kujitia ufundi kuanza kuichokoresha mashine ya boti. Kila mmoja alitia ufundi wake lakini pia hatukufanikiwa. Mimi nilijitupa chini kwenye mchanga nikawaacha wenzangu wakiendelea kushindana nayo.
 
Yalipita karibu masaa mawili. Hatimaye niliona wenzangu mmoja mmoja akiondoka kwenye boti na kutafuta mahali pa kukaa. Wote walikuwa wamekata tama kama nilivyokata mimi.
 
Mawazo yangu yakarudi kwa Harishi. Kama alivyotwambia Yasmin Harishi anaweza kutokea na kutumaliza kama alivyowamaliza watu wa kisiwa hicho.
 
Kwa muda sote tulikuwa kimya. Kila mmoja alikuwa akiwaza lake. Tulipokitokea kisiwa kile tuliona tuliona tumeokoka tukafurahi. Kumbe tumeepuka kufa maji, tumekwenda kwa muuaji mwingine anayefyonza damu.
 
Tuliendelea kukaa pale tukiangalia baharini hadi jua likaanza kuchwa. Hatukuona chombo chochote kilichopita karibu. Tulichokiona ni mawingu yaliyoonekana kama yanazama upeoni mwa macho yetu.
 
Wakati giza linaingia hatukujua tungejisitiri mahali gani usiku huo kwani kwa vyovyote vile tusingeweza kuupitisha usiku mahali hapo kutokana na baridi. Pia usalama wetu ulikuwa mdogo. Lolote lingeweza kutokea wakati wa usiku. Kuna vitu kama majoka na wanyama wakali ambao hujificha wakati wa mchana na kujitokeza wakati wa usiku.
 
Baada ya kuufikiria usalama wetu tulishauriana turudi tena katika lile jumba la yule msichana. Kuna waliopinga wakataka tupande juu ya mti ule tuupitishe usiku.
 
Lakini upepo mkali ulioanza kuvuma pamoja na ngurumo za radi ndio uliofanya tukubaliane kwa pamoja kurudi katika lile jumba kwani tulijua muda si mrefu mvua kali ingenyesha na kututosa.
 
ITAENDELEA KESHO.
 
Usipitwe na hadithi hii ya kusisimua hapo kesho na Kumekucha blog

No comments:

Post a Comment