Sunday, December 7, 2014

Watishia kususia uchaguzi, Pangani

Kumekucha blog

Pangani,WAKAZI Wilayani Pangani Mkoani Tanga, wamewataka wagombea nafasi za Serikali za mitaa kuikumbusha Serikali  kuanza mchakato wa ujenzi wa ukuta wa maji  Mto Pangani vyenginevyo wataususia uchaguzi mkuu mwakani 2015.

Wakizungumza mara baada ya kumalizika mkutano wa kampeni wa CCM kata ya Bushiri jana, wakazi hao wamesema kwa muda mrefu kumekuwa kukitolewa  ahadi lakini hadi kufikia sasa hakuna dalili zozote za kuanza mchakato huo.

 Walisema ukuta huo kwa muda mrefu umeanguka na kutishia maji kuingia katika makazi ya watu na viongozi wa wa juu wa Serikali na wa vyama wamekuwa wakitoa ahadi za matumaini kisha  wakipotea jambo ambalo limekuwa likiwatia hofu.

 “Kupitia uchaguzi wa Serikali za mitaa na uchaguzi mkuu mwakani tunataka wagombea kusimama kidete kuzungumzia ukuta wa mto Pangani----ambaye hatauzungumzia atakuwa hana uzalendo” alisema Bakar Saleh

“Kama hatutaona wagombea wakishikia kidedea ukuta tunasema tutaususia uchaguzi huu na wa mwakani---na hii itatupa ishara kuwa viongozi wetu hawana uzalendo na badala yake wako kwa  maslahi binafsi” alisema Saleh

Alisema viongozi wa Serikali Wilayani humo wamekuwa wakilifumbia macho tatizo hilo jambo ambalo limekuwa likizidisha  hofu kwa wananchi na hivyo kuwaeleza kuwa vipimo vyao ni kipindi hiki cha kampeni za Serikali za mitaa.

Kwa upande wake mkazi wa Mikoroshoni, Mrisho Khalfan, amewataka wagombea wa vyama vya siasa kuzungumzia sera za kufanya jamb gani wakati wakishinda katika uchaguzi huo na kuacha kutupiana vijembe ambavyo havijengi.

Alisema wananchi wa Pangani wako na kero nyingi zikiwemo za  masoko ya kuuzia mazao yao ambapo kwa sasa wamekuwa wakiuza kwa walanguzi na kpata hasara na hivyo badala ya kusonga mbele wanarudi nyuma.

Alisema kutokuwepo kwa masoko ya kuuzia bidhaa zao kumewafanya kuwa masikini wa kila siku na baadhi ya matajiri kuwatishia kuwa bidhaa hizo hazina masoko nje ya Wilaya hiyo.

“Kwa vile sisi ni walalahoi matajiri wamekuwa wakija kwetu na kututishia vitisho kibao vikiwemo vya kutokuwa na kleseni za biashara na kukamatwa na mamlaka ya mapatop---hili kwetu ni kitisho kikubwa na huwa tunaamini” alisema Khalfan

Alisema ili kuondosha kero hiyo na baadhi ya wakulima na wafanyabiashara kuuza mazao yao kwa uhakika ni vyema Serikali ikawajengea soko la kuuzia mazao yao na kuepuka kulanguliwa.

                                          Mwisho

No comments:

Post a Comment