Sunday, August 23, 2015

HADITHI SEHEMU YA (14)

Hadithi hii inaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya kituo cha Tiba cha Mkombozi Sanitarium Clinic, Mkombozi ni mabingwa wa magonjwa sugu na yaliyoshindikana. Mkombozi wako na mashine za kisasa zenye uwezo wa kugundua magonjwa yaliyojificha. Wapo Chuda Tanga mkabala na Raha Leo, simu 0654 361333
 
NILIJUA NIMEUA(14)
 
ILIPOISHIA
  
Nilikumbuka kuna siku moja ambayo nilikwenda kwa mganga mmoja wa kienyeji akaniambia kama nataka kupata pesa kwa wingi nikubali kuzini na maiti. Aliponiambia hivyo niling’aka kisha niliondoka bila kumuaga.
 
Katika kipindi kile pia kulikuwa na taarifa nyingi kwenye duru za habari juu ya watu wanaokamatwa  na viungo vya maiti.
 
Kwa hiyo dhana ya ushirikina imetawala katika hisia za watu hivyo vitendo vya kuzini na maiti au kuwakata viungo maiti vilikuwa ya kawaida.
 
Nilijiambia kama maiti ya mke wangu hakupelekwa kuziniwa, imekwenda kukatwa viungo ili vitumike katika mambo ya kishirikina.
 
Nilimuhurumia sana Halima. Matukio mawili mabaya yamemkuta katika usiku mmoja. Kwanza nimemtoa roho yake kikatili kwa panga na pili mwili wake umechukuliwa kwenda kuziniwa au kukatwa viungo.
 
Viumbe hawa katili sana! Nilijiambia na kutikisa kichwa.
 
Sikuwa na jingine la kufanya zaidi ya kuondoka mahali hapo huku nikiendelea kusikitika kwa huzuni na majonzi.
 
SASA ENDELEA
 
Nilijipakia kwenye gari na kuondoka. Wakati naendesha ghafla nikamkumbuka yule msichana niliyemkuta jana usiku pale makaburini. Nilipata wasiwasi sana kwamba huenda akahusika na kuchukuliwa kwa maiti ya mke wangu.
 
Nikajiambia huenda jana nilipomuona alikuwa akinichunguza mimi. Alikuwa akingoja nimfukie marehemu ili awambie wenzake waje wamfukue.
 
Vile alivyoniambia kuwa alitumwa na mganga azike vitu ulikuwa ni uongo mtupu!
 
Bila shaka nilipomfikisha nyumbani aliwambia wenzake, ndio wakarudi tena kule makaburini na kuufukua mwili wa marehemu.
 
Baada ya kuwaza hivyo niliamua kumfuata ili nimuulize. Nyumba niliyomteremsha usiku uliopita nilikuwa naikumbuka vizuri. Nilipofika kwenye ule mtaa nilizitupia macho nyumba zilizokuwa mwanzo mwanzo. Nikaiona ile nyumba. Kulikuwa na msichana aliyekuwa anatoka nikamdhani alikuwa ni yeye. Hapo hapo nikasimamisha gari.
 
Nilifungua mlango wa gari na kushuka. Nilipomuangalia vizuri yule msichana nikaona hakuwa yule niliyemdhania. Na yeye alipoona teksi akasimama ingawa alionesha alikuwa anatoka.
 
“Habari ya saa hizi?” nikamsalimia.
 
“Nzuri” akanijibu huku akinitazama kwa udadisi. Bila shaka alinigundua kuwa nilikuwa nataka kumuuliza mtu.
 
“Samahani. Unaishi humu ndani?”
 
“Ndiyo naishi humu”
 
“Kuna msichana mmoja namuulizia”
 
“Anaitwa nani?”
 
Tatizo lilikuwa jina lake. Jina lake nilikuwa silijui. Nilipokuwa naye jana sikuwahi kumuuliza anaitwa nani. Lakini sikujilaumu kwa kutomuuliza jina lake kwani sikuwa na sababu ya kumuuliza jina na hata yeye hakuniuliza jina langu.
 
Kwanza sikufikiria kabisa kwamba nitahitaji kukutana naye tena. Nilichojua ni kwamba ile jana ungekuwa ndio mwisho wetu wa kukutana, labda tuje tukutane kwa bahati mbaya.
 
“Anaitwa nani?” Msichana huyo akaniuliza tena alipoona nimeduwaa.
 
“Kwa kweli jina lake silifahamu. Lakini jana usiku nilimleta hapa kwa teksi”
 
“Sasa nitamjuaje kama hufahamu jina lake, kwani mlikutana wapi?”
 
Sikuweza kumwambia kama tulikutana makaburini, badala yake nikamuuliza.
 
“Kwani hakuna msichana mwingine anayeishi humu ndani?”
 
“Tuko wasichana watatu lakini siwezi kujua ni yupi”
 
“Huyo ni mrefu na mweusi. Kama nilimtazama vizuri ana mwanya wa juu”
 
“Ni Mwajuma!”
 
“Nafikiri atakuwa ni huyo huyo. Ninamuhitaji”
 
“Mwajuma, muda huu huwezi kumpata. Yuko kazini kwake. Mpaka jioni ndio anarudi”
 
“Anafanya kazi wapi?”
 
“Barabara ya tisa”
 
Nilitaka kujua kama Mwajuma alikuwa na mume ili nitengeze hoja kwamba mmoja wa wale watu niliowaona jana usiku alikuwa ni mume wake. Nikamuuliza kwa hila.
 
“Naweza kumpata mume wake?’
 
“Hana mume” Msichana akanijibu.
 
“Hapa ni kwao au amepangisha?”
 
“Amepangisha chumba”
 
“Umesema anarudi jioni saa ngapi?”
 
“Saa kumi na mbili jioni”
 
Niliona kusubiri hadi saa kumi na mbili jioni ilikuwa mbali sana. Nikaamua nimfuate huko huko kazini kwake.
 
“Anafanya kazi gain huko barabara ya tisa?”
 
“Anauza duka la nguo”
 
“Tafadhali nielekeze hilo duka lilipo”
 
“Lipo barabara ya tisa kwa barabara ya Jamaa. Upande wa kulia kuna jengo la ghorofa mbili limeandikwa KHADIJA MANSION. Lina maduka mengi lakini duka la kwanza ndilo analouza yeye”
 
“Nimeshapaelewa. Acha nimfuate, nina shida naye muhimu sana. Asante”
Ungana nami hapo kesho hapa hapa tangakumekuchablog ujue nini kitajitokeza katika hadithi hii ya kusisimua .

No comments:

Post a Comment