Thursday, January 7, 2016

SOMA MAKUBWA YALIYOJIRI MAGAZETINI LEO JAN, 07 TZ

Uchambuzi huu wa magazeti unaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya kituo cha Elimu Cha Candle Education Centre Tanga, kituo kinaongoza kufaulisha wanafunzi kidato cha pili hadi cha sita na wanaojiendeleza kielimu, kituo kiko na walimu wenye sifa, Candle wapo Tanga mkabala na Bank ya CRDB simu 0715 772746
MWANANCHI
Mwanasheria wa kujitegemea nchini, Fatma Karume amemshauri Rais wa Zanzibar, Ali Mohamed Shein kuachia madaraka.
“Dk Shein lazima aondoke kwa sababu kuendelea kubaki madarakani ni kuwanyang’anya Wazanzibari haki yao ya msingi,” alisema Fatma ambaye ni mtoto wa aliyekuwa Rais wa Zanzibar, Amani Abeid Karume.
Fatma alisema kuwa mzozo wa Zanzibar umesababishwa na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC), Jecha Salum Jecha kutangaza kufutwa matokeo yote ya Uchaguzi Mkuu visiwani humo wakati hana mamlaka kisheria kufanya hivyo.
Fatma alisema Jecha hana mamlaka kikatiba na kisheria kufuta matokeo hayo kwa kuwa maamuzi kama hayo yanatakiwa kufanywa na ZEC yenye mwenyekiti, makamu mwenyekiti na wajumbe watano; watatu kutoka CCM na wengine wawili kutoka CUF. “Akidi ya vikao vya ZEC ni mwenyekiti na wajumbe wanne.
Kama kikao kilifanyika, akidi ilitimia na jambo hilo likakubaliwa na tume hiyo, basi waonyeshe ni wapi walipokubali wajumbe wengine.
Hata makamu mwenyekiti hajashiriki kwenye maamuzi hayo kwa sababu kisheria uchaguzi hauwezi kufutwa bila kupata akidi hiyo,” alifafanua Fatma.
Mwanasheria huyo alisema kuwa amekuwa akiwasikia baadhi ya wana CCM Zanzibar wakisema kuwa Jecha ndiyo tume na tume ndiyo Jecha, hivyo ana haki ya kufuta uchaguzi. Lakini Fatma alisema Jecha hana mamlaka kusema jambo ambalo halijakubaliwa na tume.
Alipoulizwa ikiwa hatua ya aliyekuwa mgombea urais kupitia CUF, Seif Sharrif Hamad ya kutangaza matokeo aliyodai yalimpa ushindi si kosa, Fatma alisema, “Sikumuona Maalim Seif alipokuwa anatangaza matokeo hayo hivyo sijui kama alijitangaza kuwa mshindi au alitangaza matokeo kama yalivyobandikwa kwenye vituo.
“Katika nchi zilizokomaa kidemokrasia mgombea anaweza kuona mwelekeo wa matokeo na akampigia mwenzake kumpongeza. Nadhani Maalim Seif alisoma jumla ya matokeo ya uchaguzi kama yalivyobandikwa kwenye vituo, hivyo hilo si kosa ati,” alisema na kuongeza: “Ninasikitishwa na tabia hii.
Sikutegemea kama CCM watatumia nguvu kutaka kubaki madarakani kwa njia hii. Sikutegemea kama watavuruga katiba…ndiyo maana nina huzuni.” Jambo jingine alilosema litazua mgogoro Zanzibar ni mamlaka yenye haki ya kuidhinisha fedha za uchaguzi wa marudio ikiwa watalazimisha ufanyike.
“Kisheria fedha hizo ni lazima zikubaliwe na Baraza la Wawakilishi. Baraza lipo wapi? Ili mtu awe waziri lazima awe mjumbe wa Baraza la Wawakilishi.
Rais alivunja Baraza Agosti na kwa hiyo hadi ilipofika siku ya kuapishwa rais mpya, Zanzibar hakuna Baraza wala Waziri. Ina maana fedha za wananchi zinatumiwa bila idhini ya Baraza, ” alisema.
Alisema kinachofanyika Zanzibar ni ‘ukoloni’ wa watu weusi dhidi ya watu weusi ambao unawakosesha Wazanzibari haki yao msingi ya kumchagua kiongozi wanayemtaka.
“Hali si shwari Zanzibar. Watu wamekata tamaa kwa sababu unapokuwa na Serikali ambayo inanyang’anya haki ya wananchi ya kupiga kura, kuandamana, watu wanakosa imani na Serikali hiyo,” alisema.
Kurudia uchaguzi Kuhusu kurudiwa uchaguzi nchi nzima, Fatma alisema ulipofanyika uchaguzi mwaka 2000 ambao Amani Karume aligombea kwa mara ya kwanza, zilitokea dosari katika majimbo 10 ya Unguja.
CUF walipotaka uchaguzi urudiwe nchi nzima, CCM chini ya Benjamin Mkapa waligoma wakasema ni katika majimbo yenye dosari tu. “Nini kimetokea mwaka huu? Kama dosari zilijitokeza Pemba kama wanavyodai kwa nini urudiwe Unguja? Kwa nini hawataki kutumia uamuzi wa mwaka 2000 wa kurudia maeneo yenye dosari tu?” alihoji.
“Mkapa alisema wazi kwenye kipindi cha Hard Talk cha BBC akihojiwa na mtangazaji Tim Sebastian uchaguzi hauwezi kufutwa ila utarudiwa tu katika baadhi ya majimbo.
Kwa nini leo mambo yamebadilika na CCM inataka uchaguzi mpya?” alihoji. Fatma ambaye alikataa kueleza msimamo wake kisiasa, alisema iwapo uchaguzi huru na wa haki utafanyika leo Zanzibar, CCM haiwezi kushinda kwa sababu Wazanzibari wanajionea yale ambayo wanafanyiwa na chama hicho.
“CCM imeshindwa Zanzibar kwa sababu ilishindwa kuwashawishi watu wake na badala inawakemea, ikawanyima haki zao. Kisaikolojia wapiga kura wanataka haki zao na wasibaguliwe lakini ukiwapelekea jeshi na vifaru, unazidi kuwapoteza,” alisema.
Sherehe za Mapinduzi Wakati zikiwa zimesalia siku nne kufikia kilele cha maadhimisho ya miaka 52 ya Sikukuu ya Mapinduzi ya Zanzibar, Fatma alisema kwa hali ilivyo haina maana kutokana na CCM kung’ang’ania kukaa madarakani kwa nguvu. “Ninajisikia kusalitiwa.
Madhumuni ya Mapinduzi haikuwa kuiweka CCM madarakani milele bali kurejesha madaraka kwa wananchi,” alisema.
Alisema aliambiwa kuwa waliofanya mapinduzi (wakiongozwa na Abeid Amani Karume) walitabiri kuwa ipo siku Zanzibar itakuwa na uchaguzi au Serikali ya Umoja wa Kitaifa lakini CCM hawataki. “Wakati hao waliofanya mapinduzi wakisema hivyo, CCM haikuwepo, ilikuwepo ASP.
Hao ASP hawakuwa wakijiaminisha kuwa watakaa madarakani milele,” alisema. “Wakati tunaadhimisha mapinduzi ya Zanzibar, ni vyema Watanzania wakafahamu kuwa malengo ya mapinduzi hayo yalikuwa ni kuondoa ubaguzi wa aina yoyote na kuweka misingi ya kidemokrasia lakini CCM wamevuruga,” alisema Fatma.
MWANANCHI
Operesheni ya bomoabomoa inayoendelea kwa waliojenga nyumba mabondeni jijini Dar es Salaam itawaacha zaidi ya watu 200,000 wakiwa hawana makazi.
Ubomoaji huo ulioanza katikati ya Desemba mwaka jana, umezikumba nyumba takriban 600 katika mitaa ya Hananasif na Suna, Manispaa ya Kinondoni.
Wakazi hao ni wale ambao Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeziwekea alama ya X nyumba zao ambazo ni zaidi ya 10,000 hadi kufikia juzi, kwa mujibu wa Ofisa Mazingira Mwandamizi wake, Arnold Kisiraga.
Hadi jana mchana, Kisaraga alisema walikuwa wakiweka alama ya X katika nyumba za mabondeni zilizopo eneo la Stakishari, Segerea na kwamba wataendelea hadi Pugu, nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam.
Idadi hiyo imefikiwa kwa kuzingatia takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012 ambayo inabainisha kuwa kila kaya jijini hapa inakadiriwa kuwa na wastani wa watu wanne chini kidogo ya wastani wa Tanzania Bara wa watu watano (4.7) kwa kaya.
Mkurugenzi wa Sensa za Watu na Takwimu za Jamii, Ephraim Kwesigabo alisema kwa sasa wana takwimu za kaya pekee ambazo sehemu kubwa ya watu wake wamepanga.
Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Suna, Salim Hamis alisema katika mtaa wake kuna nyumba zaidi ya 900 ambazo kila moja inaweza kuwa na kaya kati ya tano hadi saba. “Wapangaji ni wengi katika nyumba hizi usione nyingi ni ndogo. Wengi wana hali ya chini ndiyo maana tumebanana hapahapa kwa kuwa hakuna namna tena,” alisema Hamis.
Kisiraga alisema makadirio ya awali ya nyumba 8,000 yalijikita kwa kuangalia zinazotambuliwa na Wizara ya Ardhi na manispaa lakini wamebaini “vijumba vidogo” vinavyoonekana kama vimeungana na nyumba kubwa za jirani kumbe vinajitegemea. Sehemu kubwa ya nyumba hizo zipo Kinondoni.
Alisema kadri wanavyozidi kupita mabondeni kuweka alama ya X ndivyo idadi ya nyumba zilizojengwa maeneo hatarishi zinavyoongezeka.
“Hii inatokana na mito kuendelea kupanuka kutokana kingo zake kuharibiwa na wachimba mchanga na kufanya nyumba za jirani kuingia kwenye mita 60 zinazokatazwa kisheria.
Kuna baadhi ya nyumba zilikuwa maeneo salama miaka 10 iliyopita lakini kwa sababu mto umesogea kwao basi watabomolewa kwa kuwa wapo maeneo hatarishi,” alisema Kisiraga.
Kuhusu hatua hiyo, mmoja wa wakazi walioathirika, George Mkondoa alisema: “Bado tupotupo tu hapa hatuna pa kwenda. Baadhi ya vitu nimejaribu kuvipeleka nyumbani Bagamoyo lakini vimebaki nusu.
Hivyo ilinibidi nijenge kibanda kidogo kwa muda tuishi na familia yangu.” Chiku Salim aliyekuwa na nyumba ya vyumba viwili aliyoibomoa mwenyewe, alisema hana pa kwenda kujenga licha ya kuokoa mabati na vifaa vingine katika nyumba yake.
Mmoja wa wapangaji, Steven Herman alisema: “Ubomoaji ulikuja ghafla na wengi unakuta walikuwa wamebakiza miezi mitatu au minne kodi zao ziishe hivyo kuhamishwa ghafla kumeleta mtihani wa kupata nyumba haraka ndiyo maana unakuta tunahaha hapa.” Alisema shida hizo zingeepukika iwapo wangekuwa na elimu ya kutosha kuhusu matumizi ya ardhi na mipango miji.
Mkurugenzi wa kampuni ya maendeleo ya ardhi na makazi ya Space & Development, Renny Chiwa alisema: “Ili kuwaokoa wananchi hao, ni lazima kuweka mazingira rafiki ya ukuaji wa sekta binafsi katika maendeleo na makazi. Kampuni zikipata mikopo ya nyumba kwa riba na masharti nafuu ushindani utakua na zitajenga maghorofa ambayo vyumba vyake vinaweza kupangishwa kati ya Sh30,000 hadi 100,000 kwa mwezi.
” Mtafiti wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, Patience Mlowe alisema wananchi walifanya makosa kuvamia maeneo hayo kinyume na sheria na Serikali ilikosea kwa kuwaacha waendeleze makazi kwa kuwasogezea huduma za Serikali za Mitaa, maji na umeme hivyo kuwapa uhakika wa maisha ya kudumu na kushauri utengenezwe mpango maalumu wa kuwasaidia.
“Hakuna Mtanzania anayeunga mkono wananchi hawa waendelee kukaa maeneo hatarishi ya mabondeni. Ila kinachoendelea sasa kinawaathiri kisaikolojia, kinawaumiza.
Wale ni Watanzania, Serikali lazima iwasaidie tu. Watafutiwe makazi mbadala kwa muda wanapojipanga kusimama tena,” alisema Mlowe. Alisema ubomoaji huo, unaowaacha wananchi hao kama wakimbizi katika nchi yao, unavunja haki za binadamu na unalitia doa Taifa kimataifa. “Hatujui mpaka sasa mpango wa Serikali juu ya watoto wadogo waliobaki bila makazi na ambao wanasubiri kwenda shule baada kuanza kufunguliwa,” alisema.
MWANANCHI
Wizara ya Mambo ya Ndani imeanza operesheni ya kuwasaka raia wa kigeni wanaoishi na kufanya kazi nchini kinyume cha sheria ili warudishwe makwao.
Operesheni hiyo imeanza ikiwa zimepita siku chache tangu Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu, Anthony Mavunde kumuagiza kamishna wa kazi nchini kufuta vibali vya kazi vya muda kwa wageni.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Hamad Masauni alisema wameanza operesheni hiyo baada ya kubaini kuwapo kwa raia wengi wa kigeni wanaoishi na kufanya kazi nchini kinyume cha sheria. “Serikali haiwezi kukaa kimya wakati vijana wanakosa ajira huku kazi zile walizotakiwa kufanya zikifanywa na raia wa kigeni.
Kibaya zaidi kuna baadhi ya kampuni, viwanda na taasisi zilizoajiri wageni zinawadhalilisha na kuwanyanyasa wafanyakazi wa Kitanzania, tumeanza kuwabaini na wataondolewa,” alisema.
Masauni aliwataka maofisa Uhamiaji kuwachukulia hatua za kinidhamu wote watakaobainika kuhusika kutoa vibali kinyume cha sheria. Aliiagiza Uhamiaji kutoa ripoti ya kila kinachoendelea kwenye operesheni hiyo.
Aidha, alitaka operesheni hiyo isitafsiriwe kuwa Tanzania haitaki raia wa kigeni, isipokuwa lazima sheria na kanuni zilizopo zifuatwe.
Ofisa Uhamiaji wa Mkoa wa Dar es Salaam, John Msumile aliwataka wananchi kutoa ushirikiano wakati wa operesheni hiyo na kwamba, wanatarajia kuwakamata wageni zaidi ya 350.
“Tumeanzia Kariakoo na tutasambaa kwenye manispaa zote za Mkoa wa Dar es Salaam, naomba kila mmoja ashiriki kwenye operesheni hii ya kuwaondoa raia hawa wa kigeni wanaoingia nchini kinyume cha sheria,” alisema.
Kuhusu vibali vya muda, Masauni alisema Serikali inaandaa utaratibu mwingine wa kushughulikia wageni waliotakiwa kupewa vibali vya muda baada ya kupata malalamiko juu ya suala hilo.
“Tumepata malalamiko kupitia balozi zetu juu ya kufutwa vibali hivi kwa sababu vilianza kutolewa kwa kukiuka sheria, kwa kuwa vina umuhimu wake, Serikali inaangalia namna ya kushughulikia jambo hili,” alisema.
Alisema ushughulikiaji wa suala hilo utakwenda sambamba na kuwabaini waliokuwa wakikiuka sheria kwa kutoa vibali hivyo kiholela na kuisababishia Serikali hasara.
Pia, alisema Serikali ipo kwenye mchakato wa kuanzisha mahakama ya kijeshi ya Uhamiaji ili kukomesha vitendo vya rushwa na ukiukwaji mwingine wa sheria unaofanywa na baadhi ya watumishi wa idara hiyo.
MWANANCHI
Serikali ya Awamu ya Tano imekusanya ziada ya Sh900 bilioni kupitia kodi katika kipindi cha miezi miwili tangu aingie madarakani.
Wakati Novemba makusanyo hayo yalikuwa Sh1.3 trilioni, ikiwa ni ongezeko la Sh400 bilioni, Desemba makusanyo hayo yanayosimamiwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), yalifikia Sh1.4 trilioni sawa na ongezeko la Sh500 bilioni kutoka wastani wa makusanyo ya Sh900 bilioni zilizokuwa zinakusanywa kila mwezi na Serikali ya Awamu ya Nne.
Iwapo makusanyo hayo ya ziada ya Sh900 bilioni yangeelekezwa kwenye ununuzi wa magari ya wagonjwa, yangenunuliwa magari 3,000 kwa gharama ya Sh300 milioni kila moja na kuwezesha kila mkoa kupata magari 120.
Takwimu za ongezeko la Desemba zilitolewa Dar es Salaam jana na Kaimu Kamishna wa TRA, Alphayo Kidata ambaye alisema kuanzia Julai hadi Desemba mwaka jana, mamlaka yake ilikuwa imekusanya wastani wa Sh6.4 trilioni ambayo ilikuwa ni sawa na asilimia 95.5 ya lengo la kukusanya Sh6.5 trilioni.
Kidata alisema sababu za ongezeko la makusanyo hayo ni kuziba mianya ya upotevu wa mapato na kuweka mifumo mizuri ya ufuatiliaji.
Katika hatua nyingine, Kidata alisema jumla ya Sh11.8 bilioni zimekusanywa kutoka kwa wafanyabiashara walioondosha makontena katika Bandari Kavu kinyume na taratibu za forodha. Alisema kuwa makusanyo hayo yanajumuisha Sh5.3 bilioni kutoka kwa kampuni na wafanyabiashara 19 ambao wamemaliza kulipa kodi za makonteza yao na wengine 19 ambao wamelipa sehemu ya kodi wanayodaiwa.
Yafafanua madai ya Bakwata Wakati huohuo; TRA imefafanua madai ya kuwapo upendeleo katika kutoa masharti ya ufuatiliaji wa misamaha ya kodi kwa taasisi zisizo za kiserikali na mashirika ya dini, ikisema unafanywa kwa kufuata taratibu na sheria.
Tamko la Kidata kwa vyombo vya habari limekuja kufuatia kauli iliyotolewa hivi karibuni na Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), kuwa kumekuwapo na sintofahamu katika agizo la TRA lililowataka kupeleka taarifa kuhusu magari yaliyosamehewa kodi na matumizi yake ndani ya siku saba, likihoji iwapo agizo hilo lilitolewa pia kwa taasisi nyingine.
Kidata alisema Sheria ya Mamlaka ya Mapato Tanzania inaipa mamlaka hiyo kusimamia, kukagua na kuhakiki mapato ya Serikali na kuzuia aina yoyote ya ukwepaji wa kodi kwa maendeleo ya Taifa.
“Mamlaka inayo dhamana ya kusimamia kusiwepo na matumizi mabaya ya misamaha ya kodi ambayo hutolewa kwa mujibu wa sheria kifungu cha 5 (3) cha TRA,” alisema Kidata.
Alisema TRA haina upendeleo na haibagui wala kulenga taasisi moja ya kidini. Katika taarifa hiyo Kidata alisema kwa kipindi cha Oktoba hadi Desemba 2015, TRA iliwaandikia barua walipakodi 65 na katika wahusika hao kuna taasisi na mashirika ya dini ni 39.
Kidata alisema ukaguzi huo husaidia TRA kupata taarifa muhimu ili kuishauri Serikali namna bora ya kutoa misamaha kwa manufaa ya Taifa
HABARILEO
Serikali imekataa viwango vya nauli mpya vilivyopendekezwa na Kampuni ya Uda Rapid Transit (UDA-RT), itakayotoa huduma ya usafiri wa mabasi yaendayo haraka Dar es Salaam. Pamoja na kukataa imeweka bayana kuwa viwango hivyo viko juu ambavyo wananchi wengi watashindwa kuvimudu.
Kauli hiyo ya serikali imetolewa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ambaye pia ameagiza wizara zote zinazohusika kukutana haraka iwezekanavyo na kujadili viwango vipya vya nauli vinavyoendana na hali halisi ya maisha ya wananchi. “… sasa nataka mamlaka zote zilizohusika wakutane na kuja na viwango vipya vya nauli kama huyu mwekezaji ameshindwa aseme, Serikali inaweza kuendesha mradi yenyewe,” alisisitiza Majaliwa.
Wizara na taasisi zilizoagizwa kukutana ni Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi); Wizara ya Ujenzi na ya Uchukuzi; Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra) pamoja na kampuni ya UDA-RT.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam muda mfupi baada ya kurejea akitokea Ruvuma, alikokamilisha ziara yake ya kikazi jana, alisema viwango hivyo vilivyopendekezwa na vinavyotarajiwa kujadiliwa na Mamlaka ya Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra) havifai na havikubaliki.
Alisema Novemba 25, mwaka jana alitembelea mradi huo wa DART na kumuagiza Katibu Mkuu wa Tamisemi, Mtendaji Mkuu wa DART pamoja na Wakala wa Barabara (Tanroads) kupitia mfumo mzima wa uendeshaji wa mradi huo, lakini hadi leo hakuna mpango wowote wa biashara uliowasilishwa serikalini na UDA-RT.
Alisema pamoja na hayo, pia kampuni hiyo imeshindwa kuweka bayana gharama za uendeshaji wa mradi huo, uliotakiwa kuanza rasmi Januari 10, mwaka huu. Majaliwa alisema wakati kampuni hiyo ikishindwa kuweka wazi mpango wake wa kibiashara, alishangaa juzi kusikia imewasilisha vi wango vya nauli vilivyopendekeza ambavyo vilikuwa vya gharama ya juu.
“Kwa kukosekana tu gharama halisi za uendeshaji mradi, ni dhahiri kuwa nauli zilizopendekezwa hazina uhalisia,” alisema. Kampuni hiyo ilipendekeza safari kwenye njia kuu kuwa Sh 1,200 na safari katika njia kuu na pembeni kuwa Sh 1,400 na wanafunzi nusu ya nauli hizo. “Gharama hizi ni kubwa mno.
Mradi huu unalenga kumlinda na kumsaidia mwananchi wa kawaida, wakiwemo watumishi wa umma ambao wengi wao wamejenga pembezoni mwa mji kuweza kusafiri kutoka maeneo ya pembeni hadi katikati ya jiji kwa gharama nafuu na kwa urahisi na si kumkandamiza,” alisema Majaliwa.
Alisema kipato cha wananchi kwa ujumla wakiwemo watumishi wa umma, bado si kikubwa. Alitoa mfano kwamba, mtumishi anayelipwa mshahara wa Sh 250,000 kwa mwezi, kwa nauli iliyopendekezwa pamoja na watoto wake, fedha yote inaishia kwenye nauli.
Alisema kwa hali ilivyo, Serikali haiwezi kuridhia viwango hivyo ambavyo ni wazi vitamkandamiza mwananchi badala ya kumsaidia. “Bado tunayo nafasi ya kuendesha mradi huu, si lazima tuanze Januari 10 kama ilivyopangwa, ni bora tuchelewe na kuanza tukiwa na viwango vya nauli vinavyoridhisha badala ya kuanza na nauli hizi ambazo ni gharama kubwa mno.”
Juzi Sumatra ilikutana na wadau kwa ajili ya kujadili mapendekezo hayo ya nauli, ambayo hata hivyo yalipingwa na wadau wengi wa sekta ya usafiri. Walishauri nauli iwe kati ya Sh 400 na Sh 500 kutimiza malengo ya kusaidia wananchi wa kipato cha kawaida.
Pamoja na hayo wadau hao wakiwemo wananchi na Baraza la Walaji la Sumatra (Sumatra CCC), walihoji sababu za mabasi hayo yanayobeba watu wengi kwa safari moja na yanayotumia barabara zisizo na foleni, yatoze nauli kubwa wakati daladala zinazochukua abiria wachache na kukabiliwa na msongamano mkubwa katika barabara za kawaida, wanatoza nauli za chini.
HABARILEO
Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein, amesema yeye bado ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar huku akiwataka wasioamini katiba hiyo, wapeleke shauri hilo Mahakama Kuu ya Zanzibar yenye uwezo pekee wa kutafsiri katiba.
Amebainisha kuwa yeye anaongoza nchi kwa mujibu wa Katiba na Sheria na kwamba kama si uwezo huo aliopewa kikatiba hana sababu ya kuendelea kukaa madarakani pamoja na serikali anayoingoza.
“Tuko madarakani na uongozi wote wa serikali… yupo Makamu wa Kwanza wa Rais, Makamu wa Pili wa Rais na mawaziri,” alisisitiza Dk Shein na kuongeza kuwa hao wanaodai kujiondoa serikalini huo ni uamuzi wao wenyewe.
Alibainisha kuwa yeye na serikali anayoiongoza kuendelea kuwepo madarakani si kwa uamuzi wake na wala hana ubavu wa kujiweka madarakani bali ni Katiba ambayo inajieleza wazi.
Dk Shein alitoa kauli hiyo jana kwa nyakati tofauti alipokuwa akizungumza na wananchi wa Mkoa wa Kusini Pemba katika siku yake ya kwanza ya ziara yake ya siku tatu kisiwani humu kukagua na kuzindua miradi ya maendeleo, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 52 ya Mapinduzi.
Aliwaambia wananchi kuwa yako mengi yanayosemwa lakini hawapaswi kuyasikiliza kwa kuwa kama ni serikali yeye ndiye Rais hivyo wanapaswa kumuamini anachowaeleza.
“Ya mjini yapo yasikilizeni lakini kwa Serikali mimi ndiye Rais na nisiposema mimi nitawatuma wasaidizi wangu kuwaeleza,” Dk Shein alisema na kuongeza kuwa ya vyama kila mtu ana chama chake.
Alisema kama ni suala la Chama Cha Mapinduzi (CCM) yeye ndiye Makamu Mwenyekiti Zanzibar na kama kuna la kuwaeleza wana CCM na wananchi atawaeleza yeye na viongozi wenzake wa chama hicho pamoja na taarifa za vikao vya chama vyake.
Dk Shein aliwaeleza wananchi hao kuwa ushindani wa kisiasa si ugomvi bali ni utaratibu wa kupeana changamoto katika uongozi
HABARILEO
Wazir Mkuu Kassim Majaliwa ameagiza kufukuzwa kazi kwa madaktari na wahudumu ya sekta ya afya katika hospitali ya mkoa wa Ruvuma, wanaojihusisha na vitendo vya utoaji mimba kwa wanafunzi na hata watu wazima.
Waziri mkuu ametoa agizo hilo jana, wakati akizungumza na madaktari, wauguzi na watumishi wengine wa hospitali ya mkoa wa Ruvuma, baada ya kumaliza kutembea idara na vitendo mbalimbali vilivyopo chini ya hospitali hiyo.
Alisema amepata taarifa kuwa baadhi ya madaktari na wauguzi katika hospitali hiyo, wamekuwa na tabia ya utoaji mimba na kutumia vifaa vya serikali kutekeleza vitendo hivyo jambo ambalo ni kinyume na maadili ya utumishi.
Amemuagiza Mganga mkuu kufanya ukaguzi wa kushtukiza katika hospitali hiyo ili kubaini watumishi wanaojihusisha na tabia ya kutoa mimba wanafunzi na kuwachukulia hatua kali.
“Wodi ya wazazi namba tano kuna watu wanaojihusisha na vitendo vya utoaji mimba wanawake, nina taarifa za kutosha juu ya tabia hiyo, ni marufuku kwa daktari yeyote kutumia vifaa vya hospitali kufanya vitendo vichafu vya kuwatoa mimba wasichana wadogo hususan wanafunzi.
“Hatutakuwa na msamaha kwa daktari yeyote anayeshiriki vitendo vya kutoa mimba, mganga mkuu na mganga mfawidhi tafadhalini sana chukueni hatua kwa mtumishi mwenye tabia hii, sitaki kusikia tena kwamba wodi ya wazazi inatumika kwa ajili ya utoaji mimba,” alionya.
Mbali na hilo, amewataka watumishi hao kufanya kazi kwa bidii na kuzingatia maadili na miiko ya utumishi wao kwa sababu kazi yao ni muhimu kwa kuwa inashilikia maisha ya watu.
Pia ameupongeza uongozi wa hospitali hiyo kwa kutumia mashine za kielektroniki (EFDs) katika kukusanya mapato ya hospitali, hatua iliyosaidia kuongeza mapato yake kutoka Sh 600,000 kwa mwezi hadi kufikia Sh milioni 2.4.
MTANZANIA
JENGO la Polisi Makao Makuu, jijini Dar es Salaam limenusurika kuteketea kwa moto baada ya kutokea hitilafu ya umeme katika jengo hilo.
Moto huo uliwashtua wafanyakazi wa polisi makao makuu ambao walikuwa wakikimbizana kutoka nje ili kunusuru maisha yao.
Akizungumzia tukio hilo, Msemaji wa Jeshi la Polisi, Advera Bulimba,  alisema moto huo ulianzia katika dari kwenye jengo la ghorofa ya nne ambao baada ya kuanza kuungua moto na moshi kuenea katika baadhi ya maeneo ya jengo hilo.
Alisema wafanyakazi walipoona cheche katika ghorofa hiyo ndipo walipoanza kutoa taarifa kwa wafanyakazi wenzao na kutoka nje ili kujiokoa.
“Moto ulianzia katika dari ambapo kulikua kunatoa cheche nyingi na baadae tumetoa taarifa katika kikosi cha ulinzi na uokoaji zimamoto wamekuja kuuzima,” alisema.
Alisema moto huo haujaleta madhara yoyote kwa wafanyakazi wala katika vitu vyovyote vya ofisi.
“ Tunashukuru kikosi cha zimamoto kufika mapema na kwa wakati hata hivyo watu walikuwa wakisema tulikuwa katika mazoezi lakini si hivyo bali ni moto tu na tayari umedhibitiwa,” alisema.
MTANZANIA
Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii, imejitwisha mzigo wa deni la Sh bilioni 4 ambalo Bodi ya Utalii inadaiwa.
Deni hilo ni  ambalo linahusu matangazo yanayoanzia mwaka 2013/ 2014 ambalo lilikuwa likihusu matangazo yote ya utalii yaliyokuwa yakifanyika ndani na nje ya nchi katika viwanja mbalimbali vya soka vya Ulaya.
Akizungumza na viongozi wa bodi hiyo, jana jijini Dar es Salaam, Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghebe alisema wizara inachukua jukumu la kulipa deni hilo ili bodi hiyo iweze kufanya kazi kwa amani.
“Deni hilo lisukumiwe wizara ili tulifanyie kazi, kwa kuwa  kama mkiendelea kubaki nalo nyinyi mtashindwa kufanya kazi kwa amani,”alisema Maghembe.
Alisema kutangaza utalii ni zoezi endelevu kwa kuwa ndio chanzo cha mapato kikubwa kuliko sekta yeyote nchini, hivyo aliwataka viongozi wa bodi hiyo kubadili namna ya kufikiri na kutumia rasilimali ilizonazo katika kuwashawishi wawekezeji.
“Lazima tubadili namna ya kufikiri kwa kutenga maeneo mazuri ya uwekezaji na kujitangaza kwa wadau wanaohusika juu ya kujenga hotel kwa vile viwanja tunavyo vya kutosha,”alisema Maghembe.
Pia Maghembe alisema kwamba ni wakati sahihi wa kuwa na mfuko wa kuwawezesha wawekezaji wadogo wa  ndani ili kufika viwango vya kimataifa.
Waziri huyo alisisitiza kwamba mbali na kutoa elimu juu ya wawekezaji hao, bodi hiyo inatakiwa kujitahidi katika miaka miwili ijayo kufikisha watalii milioni 2 badala ya milioni 1 iliyopo sasa.
Aidha Maghembe aliitaka bodi hiyo kuacha kulalamika juu udogo wa bajeti na kuwataka kupanga mipango yao kuendana na kiwango cha fedha walizonazo.
“Serikali ya awamu yatano imedhamiria kupambana na changamoto zinazotokana na watu binafsi, hivyo hakuna haja ya kulalamika juu ya suala la bajeti badala yake ni muhimu kuangalia vipaumbe muhimu ili kuendana na fedha mlizonazo,”alisema Maghembe.
Profesa Maghembe aliitaka bodi hiyo kuruhusu matangazo yote ya utalii yaliyokuwa tayari kuendelea kuoneshwa katika maeneo mbalimbali ndani na nje, huku akiahidi kuzifanyia kazi changamoto zilizojitokeza katika bodi hiyo
MTANZANIA
Mahakama Kuu Kitengo cha Ardhi imezuia nyumba anayoishi Mchungaji wa Kanisa  la  Assemblies of God Mikocheni, Dk. Getrude Lwakatare kubomolewa.
Uamuzi huo wa mahakama ulitolewa juzi na Jaji John Mgeta, baada ya Wakili wa Lwakatare, Emmanuel Muga kuwasilisha maombi ya kupinga ubomoaji huo chini ya hati ya dharura.
Jaji Mgeta alizuia ubomoaji wa jengo hilo ama kuchukua hatua yoyote kuhusu jengo hilo lililopo Kawe Beach.
Muga aliwasilisha maombi akimwakilisha mdai ambaye ni mtoto wa Mchungaji Lwakatare, Robert Brighton dhidi ya wadaiwa NEMC, Manispaa ya Kinondoni na wadau wengine wote.
“Mheshimiwa jaji, nawasilisha maombi ya zuio la kubomoa nyumba ya mteja wangu chini ya kifungu namba 95 cha Sheria ya Mwenendo wa Madai na kifungu namba 2(3) cha JALA vinavyotoa mamlaka kwa mahakama kutoa nafuu stahili pale kunapokuwa na ukiukwaji wa kuvunja haki ya wazi,” alidai.
Akitoa uamuzi huo alisema tayari pande husika zilikuwa na kesi namba 70 ya mwaka 2012 na ikamalizika kwa kutoa hukumu na kukazia hukumu iliyompa haki ya ushindi mdai.
“Mahakama ilimpa haki mdai, lakini chakushangaza mdaiwa anakiuka matakwa ya hukumu na kutaka kubomoa nyumba, kwa hali isiyokuwa ya kawaida mdai anahitaji ulinzi wa mahakama hii ya haki,”alisema Jaji Mgeta.
Alisema nyumba hiyo ipo katika kiwanja namba 2019 na 2020 ambapo hati yake ilitolewa mwaka 1979.
Inadaiwa mwaka 2011 NEMC ilitoa notisi ya kuvunja nyumba hiyo baada ya kushinikizwa na wakazi wa eneo hilo wakidai ujenzi wake unaziba Mto Ndumbwi na uko jirani na mikoko.
Wakili Muga aliwasilisha maombi ya kuzuia nyumba  ya mteja wake kubomolewa  baada ya Wizara  ya  Maliasili  na  Utalii kupitia  wakala  wa  misitu  Tanzania (TFS ), kuweka alama  ya X wakidai imo katika hifadhi  ya  bahari.
MTANZANIA
Kamati za Bunge zinatarajiwa kutangazwa wakati wowote kuanzia sasa, kabla ya mkutano wa pili wa Bunge la 11 kuanza Januari 26.
Taarifa za uhakika kutoka ndani ya Ofisi za Bunge zimelieleza gazeti hili kwamba, suala hilo lipo jikoni na wiki hii Spika anatarajiwa kutangaza kamati za Bunge.
Akizungumzia hilo jana jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Habari, Owen Mwandumbya alikiri suala la kamati za Bunge kushughulikiwa na Spika, Job Ndugai, huku akisisitiza kuwa suala hilo lipo katika hatua nzuri.
“Spika anashughulikia suala la kamati naamini hivi karibuni zitakuwa zimekamilika na kutangazwa hadharani hata kabla ya kuanza kwa Bunge lijalo,” alisema Owen.
Kamati hizo zinatarajiwa kutangazwa mapema kwa sababu kabla ya kuanza kwa Bunge Januari 26 taratibu zinataka kamati za Bunge zianze kwanza mikutano yake.
Kamati za Bunge huundwa kwa mujibu wa Katiba Ibara ya 96, likiwa limepewa madaraka ya kuunda kamati za Bunge za aina mbalimbali na muundo wake umefafanuliwa na Kanuni za Kudumu za Bunge.
Katika muundo huo zipo kamati za kisekta na zile zisizokuwa za kisekta, ambazo kwa pamoja hufanyakazi na kutekeleza majukumu yao kwa niaba ya Bunge.
Kwa mujibu wa Kanuni ya 89 Bunge limeunda Kamati 15 ambazo ni Kamati ya Uongozi, Kamati ya Fedha na Uchumi, Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala, Kamati ya Uwekezaji na Biashara na Kamati ya Mambo ya Nchi za Nje.
Nyingine ni Kamati ya Kanuni za Bunge, Kamati ya Ulinzi na Usalama, Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, Kamati ya Huduma za Jamii na Kamati ya Maliasili na Mazingira.
Nyingine ni Kamati ya Maendeleo ya Jamii, Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC), Kamati ya Kilimo na Ardhi pamoja, Kamati ya Miundombinu na Kamati ya Huduma za Jamii.
Hata hivyo kanuni ya 88 (12) imetoa fursa kwa kila kamati kuunda kamati nyingine ndogo kwa ajili ya uendeshaji bora wa shughuli zake.
NIPASHE
Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mwigulu  Nchemba, ameivunja Bodi ya Shirikisho la Vyama vya Ushirika vya Wakulima wa Tumbaku mkoani Iringa (ITICOJE).
Sambamba na hatua hiyo, amewafukuza kazi viongozi wa vyama vya msingi vya ushirika vya wakulima wa tumbaku, waliojaribu kujimilikisha matrekta yaliyokopwa na vyama vyao.
Nchemba alitoa kauli hiyo jana alipozungumza kwenye kikao alichokiitisha kwa kushirikiana na viongozi wa mkoa wa Iringa kwa lengo la kusikiliza malalamiko ya wakulima wa tumbaku waliokuwa  wakiwalalamikia viongozi wao.
Malalamiko hayo ya wakulima nusura yamponze Mkurugenzi wa Benki ya CRDB tawi la Iringa, Kisa Samuel, ambao waliotoa mkopo huo wenye kila dalili ya ufisadi. Mkurugenzi huyo alitakiwa kujibu kwa nini benki  imetoa mikopo hiyo yenye harufu ya ufisadi.
Nchemba alisema CRDB mbali na kutaka fedha za watu ambao ni wanachama, imewaacha wanaohodhi matrekta wakati tangu mwanzo walijua wanatumia mwavuli wa vyama kuwatapeli wakulima.
Hata hivyo, Kisa alisema wameingia mkataba na vyama vya msingi na si mtu mmoja mmoja, ndiyo maana hata kadi zina majina ya vyama.
Katika mkutano huo ulidumu takriban saa nne, Nchemba alihitimisha kwa kusema: “Kuanzia leo nitamke kwamba yale matrekta kuanzia kadi zile, umiliki wa kadi, ratiba na mwonekano wake yaende kwenye vyama vya msingi ambavyo ndivyo vimelipia matrekta.
Kwa habari, matukio na michezo ni hapahapa Tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment