Monday, January 25, 2016

UCHAMBUZI WA MAGAZETI NA CANDLE EDUCATION CENTRE TANGA

Uchambuzi wa magazeti unaletwa kwenu na Kituo cha Elimu Cha Candle Education Centre Tanga, Candle ni wataalamu wa ufundishaji wa masomo k=na kozi mbalimbali za kielimu ikiwemo Ufundi na QT
MTANZANIA
Waumini wa Kiislamu mkoani hapa wamemtaka Mufti wa Tanzania,  Sheikh Abubakari Zubeir, kutomrudisha madarakani aliyekuwa Sheikh wa Mkoa wa Dodoma, Mustapha Rajabu kwa madai kuwa anachangia kurudisha nyuma maendeleo ya uislamu.
Sheikh Mustafa alisimamishwa na Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA)   kupisha uchunguzi ambako alidaiwa kutumia vibaya fedha, mali na ofisi za Baraza hilo.
Walikuwa wakizungumza  mjini hapa jana kwenye kikao kilichofanyika kwenye Msikiti wa barabara ya tisa ambacho kiliongozwa na Mjumbe wa Baraza la Ulamaa Taifa, Sheikh Hamid Masoud Jongo,   na Katibu Mkuu wa BAKWATA, Selemani Lolila.
Walisema uongozi uliokuwa chini ya Sheikh Mustafa ulikuwa na matumizi mabaya ya fedha na mali  hivyo kurudisha nyuma maendeleo ya waumini wa dini ya kiislamu.
Mmoja wa waumini hao, Ramadhan Mzazi, alisema Mufti wa Tanzania anatakiwa kutomrudisha huku akieleza madai dhidi ya sheikh huyo kwamba akiwa madarakani alijimilikisha baadhi ya mali za BAKWATA jambo ambalo lilichangia kurudisha nyuma maendeleo.
“Sisi hapa Dodoma tuna shule mbili za Hijra na Jamhuri, shule hizi zimekuwa nyuma katika maendeleo sababu kubwa ni Sheikh huyo kuzitumia vibaya fedha zinazopatikana na walimu kila siku wanalalamika hawajapewa fedha sababu ikiwa ni yeye.
“Kwa manufaa ya Uislamu na maendeleo yetu Waislamu namuomba Mufti Sheikh Abubakari Zuberi, asimrejeshe madarakani kwani na sisi Waislamu tunataka maendeleo tumechoka kila siku sisi kuwa wa mwisho,” alidai Mzazi mbele ya viongozi hao wa BAKWATA.
Naye Awadh Mohammed alilitaka  Baraza la Ulamaa kumpelekea taarifa kuwa Mkoa wa Dodoma hawamtaki Sheikh huyo kwa madai amekuwa na kiburi cha madaraka.
Akijibu hoja hizo, Mjumbe huyo wa Baraza la Ulamaa, Sheikh  Jongo, alisema ameyapokea malalamiko ya waumini wa kiislamu hivyo atampelekea Mufti Zuberi kwa ajili ya kufanya uamuzi kwa mujibu wa utaratibu.
“Mshenga hauawi, haya mliyoyasema nitampelekea Mufti, jibu lolote atakalokuja nalo mlikubali na msije mkanilaumu mimi manake mimi napeleka kile mlinielezea,’’ alisema Sheikh Jongo.
Wajumbe wa Bakwata kwa sasa wako katika ziara ya kutatua migogoro na matatizo   katika mikoa mbalimbali.  Mbali na Dodoma pia watazunguka katika mikoa ya Mwanza, Iringa, Njombe, Ruvuma na Morogoro.
MTANZANIA
Msimamizi wa bomoabomoa  inayoendeshwa Dar es Salaam, Heche Suguta ambaye pia ni mwanasheria wa Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC), amesimamishwa kazi.
Habari zinasema hatua hiyo imechukuliwa  na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira,  January Makamba.
Suguta ambaye ni wakili daraja la pili amesimamishwa kazi na wenzake wawili  kwa   kukiuka miiko ya kazi  katika kusimamia kiwanda cha kusindika minofu ya punda kilichopo   Dodoma.
Taarifa iliyotolewa  na Idara ya Mazingira, Ofisi ya Makamu wa Rais jana ilieleza kuwa uamuzi huo umefikiwa  baada ya kikao kilichoitishwa juzi na waziri huyo   kuzungumzia njia za kuimarisha utendaji  ndani ya wa NEMC.
Taarifa hiyo ilieleza kuwa  umekuwapo ukiukwaji wa makusudi  na wa wazi wa miiko ya kazi katika  kiwanda cha kusindika minofu ya punda uliofanywa na watumishi wa NEMC  walioshughulika na kiwanda hicho.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo,  Waziri ameagiza kusimamishwa kazi mara moja watendaji watatu wa baraza hilo.
Mbali na Suguta wengine waliosimamishwa ni Ofisa Mazingira Mwandamizi,  Dk. Eladius Makene   na Ofisa Mazingira,  Boniface   Kyaruzi.
NIPASHE
Tangazo la Mwenyekiti ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar (Zec), Jecha Salim Jecha, la tarehe ya marudio ya uchaguzi, limeliweka Jeshi la Polisi na Vikosi vya Serikali ya Mapinduzi (SMZ) `mguu sawa’ kwa kuimarisha ulinzi mkali visiwani humu.
Chanzo cha kuimarishwa kwa ulinzi huo kumetokana na watu wasiofahamika kusambaza vipeperushi vyenye ujumbe wa uvunjifu wa amani katika maeneo tofauti ya Manispaa ya Mji wa Zanzibar.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Mkadam Khamis Mkadam, alithibitisha kusambazwa kwa vipeperushi na polisi imeanza kuwasaka watu hao.
Alisema vipeperushi vya uchochezi vilianza kuonekana mitaani muda mfupi baada ya Zec kutangaza tarehe ya kurudiwa Uchaguzi Mkuu Machi 20, mwaka huu.
Hata hivyo, Kamanda Mkadam alisema kuwa uchunguzi wa awali umeonyesha moja kwa moja vipeperushi hivyo kuwa vina malengo ya kisiasa kutokana na ujumbe wake na kuwataka wananchi kutoa taarifa za kuwafichua watu hao.
“Tutahakikisha Zanzibar inakuwa shwari katika kipindi chote hasa wakati huu wananchi wanasubiri uchaguzi wa marudio kufanyika Machi 20, mwaka huu,” alisema Kamanda Mkadam.
Aidha, alisema kuwa kumekuwapo na viashiria vya uvunjifu wa amani Zanzibar na kuwataka wananchi na wafuasi wa vyama vya siasa na viongozi wao, kuhubiri amani na kuimarisha misingi ya umoja wa kitaifa.
“Jeshi la polisi halitamvumilia wala kumuonea huruma mtu yeyote atakayebainika kuvuruga amani ya nchi,” alisisitiza Kamanda Mkadam.
Aidha, alisema ni kweli polisi walitumia mabomu ya vishindo juzi kuwatawanya wananchi waliokuwa wamekusanyika katika mtaa wa Kundemba kinyume cha sheria.
Alisema kuwa katika mkusanyiko huo, mtu mmoja alikamatwa na baada ya kumpekua alikutwa akiwa na dawa za kulevya.
“Jeshi lililazimika kufyatua bomu ili kuwatawanya vijana waliokuwa katika eneo hilo na kurahisisha kumkamata kijana aliyekuwa na dawa za kulevya,” alisema.
Askari wa doria wakiwa katika magari ya Jeshi la Polisi waliochanganyikana na wa Vikosi vya SMZ, wamekuwa wakifanya doria katika mitaa mbalimbali ya kuingia na kutoka Manispaa ya Mji wa Zanzibar kabla ya kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa marudio.
NIPASHE
Wakati Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ikigomea uchaguzi wa wenyeviti wa Kamati za Bunge, baadhi ya wabunge wamekuwa wakiwatania wenzao waliopo kwenye Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa kuwalinganisha na watuhumiwa wa ugaidi walioshikiliwa na utawala wa Marekani katika gereza la Guantamo Bay (hivi sasa Gitmo) lililopo nchini Cuba.
Gereza hilo ambalo hivi sasa limepewa jina la Gitmo, limekuwa likitumiwa na Marekani kwa kuwahifadhi wapiganaji wanaokamatwa Iraq na Afghanistan bila ya kuwafungulia mashitaka yoyote.
Wabunge waliopo katika kamati hiyo ni Hussein Bashe, wa Jimbo la Nzega Mjini, Dk. Charles Tizeba (Buchosa), Margaret Sitta (Urambo Mashariki) na Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi.
Wengine katika kamati hiyo ni Dk. Faustine Ndugulile (Kigamboni), Kasuku Bilago (Buyungu), Dk. Raphael Chegeni (Busega), Peter Serukamba (Kigoma Kaskazini) na Dk. Elly Macha.
Wabunge wengine katika kamati hiyo ni Lucia Mlowe, Risala Kabongo, Dk. Jasmine Bunga, Jacqueline Ngonyani Msongozi na Susan Lyimo, ambao wote ni wa Viti Maalum.
Katika kamati hiyo iliyopachikwa jina la ‘Guantanamo Bay’, wapo pia Stephen Masele wa Jimbo la Shinyanga Mjini, Mussa Azzan Zungu (Ilala), Juma Nkamia (Chemba), Seleman Bungara (Kilwa Kusini), Zitto Kabwe (Kigoma Mjini), Lazaro Nyalandu (Singida Kaskazini), Saed Kubenea (Ubungo) na Josephine Genzabuke wa Viti Maalum.
Mmoja wa wabunge ameiambia Nipashe kuwa chanzo kimojawapo kwa wenzao hao (wa kamati ya Huduma za Jamii) kutaniwa kuwa wako katika gereza la Guantamo ni kuwa na wabunge wengi wenye majina makubwa kisiasa na ambao awali walitarajiwa kuongoza baadhi ya kamati nyeti, lakini mwishowe wakapangiwa katika kamati wasiyoitarajia.
Kwa muda mrefu, Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC);  Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC); Bajeti; Katiba na Sheria; Nishati na Madini; Miundombinu, Ardhi, Maliasili na Utalii na ile ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama; zilizoeleka kuwa na watu wenye majina makubwa kisiasa; jambo ambalo ni tofauti na sasa kwani baadhi ya walioteuliwa hawana umaarufu mkubwa.
Baada ya wajumbe wa Kamati ya Huduma za Jamii kufanya uchaguzi wao na Serukamba kushinda uenyekiti, baadhi ya wabunge walionekana kumtania (Serukamba) kwa kumuita ‘Kiongozi wa Gereza la Guantanamo’ huku wengine wakimuita ‘Kiongozi wa Jamii’. Katika Bunge la 10, Serukamba alikuwa ni mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu.
Pia, baadhi ya wabunge wa kamati hiyo, walionekana wakitaniana wenyewe kwamba sasa kazi yao itakuwa kukagua madarasa vijijini na pia ubora wa zahanati.
Mbali na kamati hiyo, wabunge pia walionekana kuwatania wajumbe wa Kamati ya Sheria Ndogo ambayo imesheheni wanasheria maarufu.
Wajumbe hao walikuwa wakitaniwa kwamba baadhi yao, licha ya kuwa na weledi mkubwa kwenye sheria, wamepangwa katika kamati ambayo kazi yake kubwa ni kuangalia sheria zinazohusiana na vijiji na serikali za mitaa.
Baadhi ya wanasheria maarufu waliomo kwenye kamati hiyo, ni pamoja na Mbunge wa Bariadi Andrew Chenge, Halima Mdee (Kawe), William  Ngeleja (Sengerema), Tundu Lissu (Singida Mashariki) na Ridhiwan Kikwete (Chalinze).
Wabunge wengine maarufu kwenye kamati hiyo ni Prof. Anna Tibaijuka (Muleba Kusini), ambaye kwenye Bunge lililopita alikuwa Waziri wa Nyumba na Maendeleo ya Makazi kabla ya uteuzi wake kutenguliwa kufuatia kuhusishwa kwake na kashfa ya Escrow pamoja na Sadifa Juma Khamis (Donge) ambaye pia ni Menyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM).
Akizungumza na Nipashe mwishoni mwa juma, Naibu Katibu Mkuu wa Bunge, Uendeshaji, John Joel, alisema wameamua kupanga watu werevu kwenye sheria katika kamati hiyo kwa sababu serikali inaanzia kwenye mitaa na halmashauri.
Alisema katika eneo hilo kuna sheria nyingi zinazotungwa ambazo haziendani na zile zinazotungwa na Bunge, hivyo wameamua kuchagua watu makini ili wazisimamie.
Inaelezwa zaidi kuwa mbali na kutarajiwa kuwamo kwenye kamati nyeti kama ya PAC, wengi waliomo kwenye kamati ya Huduma za Jamii walikuwa wakitarajiwa kushika nafasi za juu zikiwamo hata za uwaziri na pia uspika, akiwamo Zungu aliyekuwa mwenyekiti wa Bunge katika Bunge la 10.
Kadhalika, inaelezwa kuwa ndani ya kamati hiyo, wamo watu ambao wamekuwa wasemaji wa masuala mengi ndani ya CCM, akiwamo Bashe.
Jitihada za kumpata mwenyekiti wa kamati hiyo, Serukamba, kuzungumzia suala hilo jana zilishindikana baada ya simu yake ya mkononi kuita muda mwingi bila kupokelewa.
Zitto alipoulizwa kama anajua kuwa kamati aliyopo sasa inataniwa kwa jina la Guantanamo Bay, alisema ni kweli, lakini hajui ni kwanini.
“Kwakweli sijui kwa nini wanatuita hivyo, nadhani ni sababu ya kuwa kamati imesheheni wabunge wenye majina makubwa.
Maana toka juzi tukikutana na wabunge wengine wanasema ‘ah wazee wa Guantanamo’… tunacheka tu, sijui sababu. Ila wacha tufanye kazi kwa umakini kwenye sekta ya elimu, afya na michezo,” alisema Zitto ambaye katika Bunge la 10 alikuwa ndiye mwenyekiti wa PAC huku Serukamba akiongoza Kamati ya Miundombinu.
Mwaka 1903, Tomas Estrada Palma, aliyekuwa Rais wa Cuba, alilikodisha eneo hilo kwa Wamarekani.
Baada ya vitendo vya ugaidi kushamiri, mwanzoni mwa mwaka 2002, washukiwa wa kwanza wa ugaidi walipelekwa kwenye gereza hilo kwa amri ya aliyekuwa Rais wa Marekani, George. W. Bush na Rais wa sasa, Barack Obama, alipoingia madarakani mwaka 2009, aliahidi kufunga gereza hilo ingawa hadi sasa hajatimiza ahadi yake hiyo.
Baadhi ya wadadisi wanaamini kuwa Marekani ilifungua gereza hilo nje ya ardhi ya Marekani ili wanajeshi wake wapate fursa ya kutumia mbinu zilizopigwa marufuku katika ardhi yao za kuwahoji wafungwa.
Kwa muda mrefu, gereza hilo pia limekumbwa na tuhuma za ukiukwaji wa haki za binadamu,  wafungwa wakidaiwa kuteswa, kupigwa na hata kulazimishwa kukiri baadhi ya makosa wasiyowahi kuyatenda.
NIPASHE
Mwanasheria Mkuu (AG) wa zamani Zanzibar, Othman Masoud Othman, amesema Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, anapaswa kujiuzulu kwa sasa na Jaji Mkuu kuiongoza visiwa hivyo kwa kuunda kamati maalum itakayochunguza uhalali wa kufutwa kwa matokeo ya uchaguzi mkuu visiwani humo.
Aidha, amesema Rais Dk. John Magufuli anapaswa kuingilia kati mgogoro uliopo visiwani humo, ili kuinusuru nchi kuingia katika mgongano wa kisiasa.
Aliyasema hayo jana wakati wa kongamano la wazi juu ya changamoto za kisheria zilizojitokeza baada ya kufutwa kwa uchaguzi mkuu wa Zanzibar uliofanyika Oktoba 25, mwaka jana, lililoandaliwa na Chama Cha Wanasheria Tanganyika (TLS), jijini Dar es Salaam jana.
Alisema Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu, anapaswa kuingoza Zanzibar kwa sasa na kuunda tume huru itakayochunguza uhalali wa kisheria uliosababisha kufutwa kwa matokeo ya uchaguzi huo na kusababisha mvutano wa kisiasa visiwani humo.
Alisema endapo kamati hiyo itabaini kuwa hakukuwa na uhalali wa kufutwa kwa uchaguzi huo, waliohusika kufutwa watatakiwa kufikishwa katika mikono ya sheria.
Naye mwanasheria kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Harold Sungusia, alisema changamoto zilizojitokeza wakati wa uchaguzi mkuu bara ni nyingi mojawapo ni kutokuwa na maandalizi ya kutosha kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC)
“Zaidi ya mikutano 172 ilifanyika nje ya muda uliopangwa, kwa mujibu wa utafiti tuliofanya katika mikoa mitano ya Dar es Salaam, Tabora, Arusha, Mbeya na Tanga, wanasisasa wengi hawakufuata sheria ya muda,” alisema Sungusia.
Sababu nyingine ni lugha zilizotumika katika baadhi ya mikutano ya kampeni haikuwa nzuri na kwamba wagombea wengi walitumia lugha za matusi huku zaidi ya mikutano 188 iliyofanywa na wagombea ilikuwa na lugha za matusi.
Alisema viashiria vya rushwa pia vilitawala katika uchaguzi huo, ambapo zaidi ya mikutano 139 kulikuwa na viashiria vya rushwa na changamoto nyingine waliyobaini ni ucheleweshwaji wa kutangaza matokeo katika baadhi ya vituo vya kupigia kura.
Naye Wakili wa Kujitegemea, Fatma Karume, alisema ili kutojirudia kwa kile kilichotokea Zanzibar, inapaswa kuwapo kwa mahakam huru na tume ya uchaguzi huru.
Alisema bila ya kuwapo kwa vitu hivyo hali mbaya ya kisiasa visiwani humo inaweza kujirudia kila uchaguzi utakapofanyika.
Kaimu Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa Chama Cha Wananchi CUF, Ismail Jussa, alisema hicho kinashikilia msimamo wake wa kutotaka kurudia uchaguzi visiwani humo.
 HABARILEO
Waziri wa Elimu, Sayansi na Mafunzo ya Ufundi, Prof. Joyce Ndalichako, amesema mfumo wa wastani wa alama za mtihani (GPA) haukuwa sabababu ya yeye kuondoka katika nafasi ya Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Taifa (Necta).
Prof, Ndalichako alisema hayo wiki iliyopita wakati akijibu maswali ya waandishi wa habari mjini hapa kutokana na uvumi uliozagaa mitaani ikiwemo kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii kuwa alijiuzulu nafasi hiyo kutokana na kushinikizwa kuukubali mfumo huo.
Alisema aliondoka Necta baada ya kufanya kazi katika baraza hilo kwa miaka tisa, hivyo muda huo aliona unatosha kwa yeye kuliongoza baraza hilo la mitihani nchini.
“GPA haikuniondoa Necta kama ambavyo nimekuwa nikisikia maneno mitaani kuwa niliondoka ili kupisha mfumo huu wa GPA kuanza kutumiwa na baraza hili la mitihani nchini,”alisema.
Prof. Ndalichako alisema kuondoka kwake kulisukumwa na kazi kubwa alizokuwa amezifanya katika baraza hilo, pamoja na kuweka mifumo mbalimbali ya kisasa katika usajili na mambo mengine ya kitaalamu ambayo hayakuwapo kabla yake.
“Nimefika pale Necta nikakuta kuna baadhi ya watendaji wanadai hawaejenda likizo kwa zaidi ya miaka mitatu, hii yote ilikuwa ni kutoka na mifumo iliyokuwa ikitumika ambayo kwa kiasi kikubwa ilikuwa kwenye vichwa vya watu hivyo wao kama hawatakuwapo basi kazi nyingine hazifanyiki…nikamua kuanzisha mifumo ya kisasa na kuacha kutegemea vichwa vya watu,” alisema.
Prof. Ndalichako alisema sababu nyingine iliyomuondoa Necta ni kutaka kujiendeleza kielimu kutoka alipokuwa wakati huo na kupanda katika ngazi nyingine, kwani kama angeendelea kubaki asingeweza kujiendeleza.
“Nilitoka Necta nikarudi Chuo Kikuu cha Dar es Salaamu ili kujiendeleza na hivi sasa mimi ni profesa lakini nilipokuwa Necta nilikuwa dokta, hivyo hayo maeneno yanayozagaa kuwa mimi nilikimbia GPA si ya kweli hata kidogo na mfumo huo ulianzishwa mimi nikiwa sipo pale,” aliongeza kusema.
HABARILEO
Wamiliki wote waliokabidhiwa viwanda vya serikali baada ya kubinafsishwa, lakini wakashindwa kuviendeleza, wametakiwa kuanzia Julai wawe wameanza uzalishaji.
Vinginevyo, wameelezwa kuwa hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.
Waziri wa Viwanda, Biashara ya Uwekezaji, Charles Mwijage alitoa tamko hilo juzi mjini hapa baada ya kutembelea na kukagua viwanda vya serikali, vilivyobinafsishwa kwa wawekezaji .
Mwijage alimwagiza Mkurugenzi wa Viwanda wa wizara yake kufuatilia Wizara ya Fedha na Mipango na taratibu mbalimbali za kisheria kwa wamiliki wa viwanda, vilivyofungwa ama kushindwa kuendelea kuzalisha, kabla ya hatua nyingine za kisheria kuchukuliwa kwa watakaoshindwa kutekeleza agizo .
“Viwanda vya mashirika yote ambayo yalibinafsishwa na kupewa wawekezaji, nahitaji kuona vinafanya kazi mwaka ujao wa bajeti Julai 2016,” alisema Mwijage akiwa na Menejimeti ya Kiwanda cha Abood Seed Oil (Moproco).
Alisema lengo la serikali ni kuona viwanda vyote vilivyobinafsishwa na kushindwa kutimiza malengo yaliyokusudiwa, vinafanya kazi za uzalishaji kulingana na maelekezo yaliyomo ndani ya mikataba ili kuwezesha kutoa ajira nyingi za Watanzania.
Alisema mkoa wa Morogoro ni wa uwekezaji wa viwanda na baadhi vilijengwa kutokana na upatikanaji rahisi wa malighafi, zinatokana na sekta ya kilimo .
Vile vile alisema mpango wa ubinafsishaji, ulikuwa ni kutoa fursa pana kwa wawekezaji kutoa ajira nyingi na kuongeza kasi ya uzalishaji wa bidhaa kukuza uchumi, tofauti na ilivyo sasa.
“ Serikali ya awamu ya tano ni ya viwanda na Morogoro ni sehemu iliyopewa kipaumbele cha kwanza cha uwekezaji wa viwanda vipya na kufufuliwa vya zamani, hivyo ni jukumu la wizara yangu kuona viwanda vyote vinafanya kazi kuanzia mwaka ujao wa fedha,” alisema akiwa na viongozi wa serikali mkoani hapa.
Akiwa katika kiwanda cha G&T Shoe ( Moro Shoe Ltd), Waziri alimwagiza Mkurugenzi wa Viwanda wa Wizara, Obadia Nyagilo kuwasiliana na Mamlaka ya Maeneo Huru ya Uuzaji Bidhaa Nje ya Nchi (EPZA), eneo hilo apewe mwekezaji mwingine mwenye uwezo wa kujenga kiwanda .
Moro Shoe Ltd ambacho kinamilikiwa na Guled Shoe Co. Ltd, kiliungua moto kikiwa chini ya mwekezaji huyo na eneo hilo limebaki gofu. Waziri pia aliagiza uangaliwe utaratibu wa namna ya kutwaa kiwanda cha Morogoro Ceramic Wares Ltd na kupatiwa mwekezaji mwingine.
HABARILEO
Watumishi sita wa Halmashauri ya Mji wa Kahama mkoa wa Shinyanga, wamekamatwa na Polisi.
Wafanyakazi hao ni miongoni mwa waliosimamishwa kazi hivi karibuni na wengine kuwekwa katika uangalizi maalumu kwa tuhuma za kula njama za kujipatia zaidi ya Sh milioni 800, zilitolewa na Mgodi wa dhahabu wa Buzwagi.
Fedha hizo zilitolewa na mgodi huo kwa lengo la kutekeleza miradi ya maendeleo ya wananchi wa halmashauri hiyo.
Waliokamatwa ni Katibu wa Bodi ya Zabuni, Joseph Maziku ambaye ni Ofisa Ugavi na Wajumbe, Kulwa Ntaudyimara (Ofisa Utumishi) na Annastazia Manumbu (Ofisa Elimu Sekondari).
Wengine ni Joachim Henjewele ambaye ni Mkuu wa Idara ya Ardhi, Elius Mollel, Ofisa Biashara na Gervas Lugodisha kutoka Ofisi ya Ugavi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga Mika Nyange, alikiri kukamatwa kwa watumishi hao.
Alieleza kuwa leo atatoa ufafanuzi juu ya hatua iliyofikiwa kuhusu tuhuma za watumishi hao, baada ya kuwasiliana na Mkuu wa Polisi wa wilaya ya Kahama.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Anderson Msumba, alisema watumishi hao walikamatwa juzi na Polisi baada ya kampuni moja, kati ya kampuni nyingi zilizohusika katika fedha hizo, kujitokeza katika ofisi za halmashauri kudai malipo, wakati nyaraka zake zinapishana na za kampuni iliyopewa kazi na Bodi ya Zabuni.
Nyaraka za Halmashauri zinaonesha kuwa Bodi ya Zabuni iliipa kazi Kampuni ya Noble Cliff Construction na kuonesha malipo yatafanyika kupitia akaunti ya benki ya NMB, huku madai ya kampuni hiyo yalionesha kulipwa fedha kupitia Benki ya Afrika (BOA).
Baada ya kuwepo mabishano ya kutofautiana kwa mikataba, Msumba alidai alimtuma Mweka Hazina wake kwenda kukagua akaunti hizo na kukuta ile ya BOA, ambayo kampuni hiyo ilidai ilipwe, ilishafungwa siku nyingi na ya NMB ambayo ilipitishwa na Bodi ya Zabuni, ilikuwa ikimilikiwa na mtu binafsi.
Msumba alidai hali hiyo ilionesha kulikuwa na kasoro katika mchakato wa utoaji wa zabuni. Wajumbe wote wa Bodi ya Zabuni ya Halmashauri ya Mji wa Kahama, wamekamatwa kutokana na sakata hilo na hadi jana walikuwa mahabusu katika Kituo Kikuu cha Polisi cha wilaya.
Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Vita Kawawa alitoa tuhuma kuhusu fedha hizo za Buzwagi katika kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo hivi karibuni.
Baada ya hapo, Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Abel Shija, aliwasimamisha kazi watumishi watano kwa tuhuma hizo za kutumia vibaya fedha za Mgodi wa Buzwagi. Aliagiza waliohamishwa na wanatuhumiwa, warejeshwe kujibu tuhuma zao.
MWANANCHI
Operesheni ya kukamata raia wa kigeni wanaoishi na kufanya kazi nchini bila ya kuwa na vibali imebaini China na Burundi zinaongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya wahamiaji haramu ikilinganishwa na nchi nyingine.
Tangu kuanza kwa operesheni hiyo nchini Desemba 8, mwaka jana hadi Januari 14, mwaka huu, idadi ya raia wa kigeni wasiokuwa na vibali waliokamatwa kutoka China walikuwa ni 285, Burundi 284, wakifuatia 157 wa Ethiopia.
Raia wengine waliokamatwa ni kutoka India 41, Zambia 40, DRC 34, Malawi 27, Kenya 26, Uganda 13, Ivory Coast 10, Korea tisa, Nigeria wanane, Somalia saba, Madagascar watano, Rwanda watatu, Lebanon, Zimbabwe, Ghana na Afrika Kusini mmoja kila moja na wengine 11 uraia wao ni wa utata.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga akizungumza katika mwaka mpya wa China Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.
“Kati ya hawa, baadhi wamepelekwa katika kambi za wakimbizi, hasa raia waliotoka Burundi, wengine wamepewa amri ya kuondoka nchini na wengine kesi zao ziko katika hatua mbalimbali mahakamani.” Kitwanga alibainisha kuwa operesheni hiyo ya kukamata raia wa kigeni wanaoishi na kufanya kazi nchini bila vibali haitawagusa wenye vibali halali.
Kitwanga alisema wizara yake imetoa vibali vya ukazi kwa wageni 40,765 kutoka mataifa mbalimbali kati ya mwaka 2014 na Januari mwaka huu na kwamba idadi hiyo inaendelea kuongezeka siku hadi siku. “Wageni waliofukuzwa kwa sababu mbalimbali mwaka 2015 ni 1,642,” alisema.
MWANANCHI
Wakazi wa Bonde la Mkwajuni katika Mtaa wa Hananasifu na Suna, Manispaa ya Kinondoni ambao nyumba zao zilibomolewa, wanaishi kwenye eneo hilo licha ya kuendelea kuathiriwa na mvua.
Wakazi hao ambao hivi karibuni vibanda vyao vilibomolewa kwa amri ya Serikali, wameendelea kubakia na kujenga vibanda juu ya vifusi vya nyumba zilizobomolewa.
Mmoja wa wakazi wa eneo hilo, Nicolata Myanga alisema hawataondoka eneo hilo kwa kuwa Serikali haijawapa viwanja.
“Serikali kama inataka tuondoke ije itege bomu tu hapa tufe, tutakwenda wapi? Tunaambiwa tumepewa viwanja viko wapi? Hivi kweli mimi na uzee wangu huu nimepewa kiwanja naambiwa ondoka nitang’ang’ania hapa ili iweje?” alihoji Myanga mwenye umri wa miaka 68.
Mkazi mwingine wa eneo hilo, Magreth Dimoso alisema hali ya maisha yao inazidi kuwa ngumu kila siku, lakini mbaya zaidi ni kuwa kadri mvua zinavyonyesha hawana pa kukimbilia kwa kuwa hata baadhi ya vibanda walivyojenga vimesombwa na maji.
Mwathirika mwingine wa bomoabomoa hiyo, Anastatus Mponda alisema maisha yao ni magumu kuliko hata ya wakimbizi.
Maisha ya ombaomba Kutokana na hali ngumu waliyonayo, baadhi yao wamegeuka kuwa ombaomba, kwani hata mwandishi wa habari hizi alipofika alilakiwa kwa salamu ya kuombwa Sh1,000 na Jumanne Iddy.
Maimuna Juma aliyekuwa amekaa nje ya kibanda chake akiwa anambembeleza mwanaye aliyekuwa akilia kwa sababu ya njaa, alipomuona mwandishi aliomba msaada wa fedha akamnunulie chakula.
Uongozi wa mtaa wanena Mwenyekiti wa Mtaa wa Suna, Salumu Hamis alisema kuwa kuna kaya zaidi ya 700 zinaishi sehemu hiyo na kwamba, kati ya jumla ya kaya 900 zilizokuwa zinaishi hapo, 150 pekee ndizo zilipewa viwanja Mabwepande,” alisema.
Kwa habari, matukio na michezo ni hapahapa Tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment