Thursday, December 15, 2016

ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 7

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU 7
 
ILIPOISHIA
 
Jibu hilo la mkato liliwavunja nguvu polisi hao ambao walilazimika kuondoka ofisini hapo. Dodosa dodosa ya Inspekta Amour kwenye mitaa ya Temeke ilimfikisha katika nyumba ambayo ilielezwa alikuwa akiishi Pascal.
 
Inspekta Amour alipolitaja jina la Pascal, mwanamke aliyekuwa amemkaribisha kwenye nyumba hiyo alitoa tabasamu la huzuni.
 
“Mbona Pascal sasa hivi ni marehemu, Pascal alishakufa” Mwanamke huyo alimwambia Amour aliyeonekana kushangaa.
 
“Alikufa lini?”
 
“Sasa ni karibu miezi mitatu”
 
“Unamzungumzia Pascal Lazza aliyekuwa akifanya kazi kiwanda cha mabati?”
 
“Ndiye yeye ninayekwambia, alishakufa. Mimi hapa ninayekueleza ni mjane wake”
 
“Ninapata taabu kuamini kwa sababu Pascal amekuwa akionekana na anawasiliana na watu”
 
Mwanamke huyo akashituka.
 
“Pascal ameonekana wapi?”
 
SASA ENDELEA
 
“Ameonekana jana na karibu wiki hii yote”
 
“Wapi?”
 
“Hapa hapa Dar es Salaam”
 
Mwanamke huyo licha ya kushituka alitikisa kichwa.
 
“Si kweli. Mtu aliyekufa ataonekanaje?’
 
“Kuna mtu alimuona jana Kinondoni akiwa na gari aina ya Toyota Corolla ya rangi ya kijani”
 
“Itakuwa si yeye. Kwanza marehemu hakuwa na gari”
 
Inspekta Amour akatikisa kichwa.
 
“Ninahisi kwamba unanificha. Pascal yuko hai, ninaomba uniambie yuko wapi?”
 
Mwanamke huyo akanywea.
 
“Hebu njoo ndani” alimwambia Amour huku akirudi ndani.
 
Amour aliingia ndani na kukaribishwa sebuleni. Aliiona picha kubwa ya Pascal Lazza ikiwa imetundikwa kwenye ukuta. Sura ya Pascal aliitambua baada ya kuilinganisha na ile aliyoiona kwenye kivuli cha shahada ya Pascal iliyokuwa imesajiliwa kwenye mtandao wa simu.
 
Lakini picha hiyo iliyokuwa imetundikwa ilimpa alama ya kuuliza baada ya kuona ilikuwa imezungushiwa shada la maua kuonesha kuwa hakuwa hai.
 
“Nisubiri” Mwanamke huyo alimwambia Amour. Akaingia chumbani. Baadaye kidogo alitoka akiwa ameshika gazeti na kitabu cha picha.
 
Alimpa Inspekta Amour lile gazeti.
 
“Kama unakumbuka kulitokea ajali ya gari eneo la Kimara miezi miwili iliyopita ambapo watu wawili walipoteza maisha” Mwanamke huyo alimwambia Amour.
 
“Kama kulitokea ajali…?’
 
“Miongoni mwa hao waliokufa alikuwa mume wangu, angalia kwenye gazeti habari zao ziliandikwa”
 
Amour akaliangalia lile gazeti. Katika ukurasa wake wa kwanza kulikuwa na picha kubwa ilioonesha gari lililokuwa limegongwa na kuharibika vibaya sehemu ya mbele. Chini yake kulikuwa na picha ndogo mbili. Picha moja ilimuonesha Pascal na picha ya pili ilimuonesha mtu mwingine ambaye Amour hakuweza kumfahamu.
 
Habari iliyoandikwa ilihusu kugongwa kwa gari hilo na lori la mafuta ambapo watu wawili waliokuwemo kwenye gari hilo walifariki dunia hapo hapo. Mmoja wa watu hao alikuwa Pascal Lazza!
 
Amour aliikumbuka ile ajali na yeye alifika katika eneo la tukio na aliwashuhudia watu hao. Hakuwa na cha kupinga.
 
Alinyamaza kimya kwa sekunde kadhaa akiwaza.
 
“Umeamini?” Mwanamke akamuuliza.
 
“Mimi mwenyewe pia nilikuwepo katika eneo la tukio”
 
“Kuna picha zake nyingine za maziko ziko hapa kwenye albamu”
 
“Sitahitaji kuziona. Acha niende, nitarudi tena kwako baadaye”
 
Amour alimrudishia gazeti yule mwanamke, akatoka.
 
Alimfuata James nyumbani kwa marehemu Kinondoni lakini aliambiwa James aliondoka dakika chache zilizopita kuelekea nyumbani kwake.
 
Akajipakia tena kwenye gari na kumpigia simu. James alipopokea simu alimuuliza.
 
“Uko wapi James?”
 
“Wewe nani?”
 
“Unazungumza na Inspekta Amour”
 
“Oh Inspekta Amour! Niko nyumbani hapa”
 
“Nanahitaji kukuona, nitakupataje?”
 
“Unaweza kuja nyumbani au kama ni lazima mimi nije huko”
 
“Acha nije nyumbani kwako”
 
“Njoo”
 
Amour akakata simu na kuliwasha gari. Kwa vile alikuwa akiifahamu nyumba ya James alimfuata. Alifika hadi mbele ya nyumba ya James akampigia tena simu.
 
“Nimeshafika, niko nje” alimwambia.
 
“Sawa, nakuja”
 
Sekunde chache baadaye James alifungua geti. Akaliona gari alilofika nalo Amour. Inspekta Amour hakushuka kwenye gari. James alilifuata gari hilo.
 
“Zunguka upande wa pili uingie kwenye gari” Amour alimwambia James.
 
James alizunguka upande wa pili wa gari hilo akafungua mlango na kujipakia.
 
“Kuna kitu ambacho kimenishangaza sana” Amour akamwambia James kwa sauti tulivu.
 
“Kitu gani?” James akauliza.
 
“Nilikwenda kwenye ofisi za kampuni inayomiliki ile namba ya Pascal. Pale nilipata maelezo yote kuhusu yeye. Usajili wake ulionesha kuwa alikuwa mkazi wa Temeke na mfanyakazi wa kiwanda cha mabati” Amour akaanza kumuleza James.
 
“Enhee..?” James akauliza kwa shauku.
 
“Lakini nilipokwenda kwenye hicho kiwanda, niliambiwa kuwa Pascal alishaacha kazi karibu miezi sita iliyopita. Nikajitahidi kupajua mahali anapoishi, nikafanikiwa kuipata nyumba yake”
 
Uso wa James ulikuwa kama unaotaka kutabasamu kwa kuhisi kuwa Pascal alikuwa ameshakamatwa.
 
“Nilionana na mwanamke mmoja aliyenieleza kuwa alikuwa mke wa Pascal. Mwanamke huyo alinipa maelezo ya kunishangaza. Aliniambia kuwa Pascal alikwisha kufa miezi miwili iliyopita katika ajali ya gari iliyotokea Kimara”
 
“Amedanganya! Pascal yuko hai na ndiye aliyemuua mchumba wangu” James alidakia.
 
“Amenithibitishia kuwa Pascal amekufa kweli. Alinionesha picha za magazeti. Ile habari iliandikwa kwenye magazeti na picha ya Pascal nimeiona ni kati ya watu waliokufa”
 
“Kwani wewe unamjua Pascal? Ulimuona wapi?”
 
“Niliona picha yake kwenye kivuli cha shahada alichosajilia simu yake”
 
James akatikisa kichwa.
 
“Haiwezekani!”
 
“Ninajua kuwa haiwezekani ndio sababu nimekufuata hapa”
 
James akanyamaza na kumtazama Inspekta huyo.
 
“Ninataka twende nyumbani kwa yule mwanamke ukaitazame ile picha halafu uniambie ndiye Pascal uliyemuona wewe”
 
“Sawa. Twende hata sasa hivi”
 
James alirudi kufunga mlango kabla ya kuondoka na gari alilokwenda nalo Inspekta Amour.
 
“Mimi naamini kuwa Pascal yuko hai. Kunaweza kuwepo na mbinu za kihalifu za kuonesha kuwa amekufa ili polisi wasiendelee kumtafuta” James alimwambia Amour kwenye gari.
 
“Wewe ndiye utakayetuthibitishia Pascal yuko hai au amekufa”
 
Walipofika Temeke kwenye nyumba ambayo Inspekta Amour alifika kwa mara ya kwanza na kuzungumza na mwanamke aliyemueleza kuwa Pascal alikuwa amekufa, walikaribishwa ndani.
 
“Umerudi tena?” Mwanamke huyo alimuuliza Inspekta Amour.
 
“Ndio. Nilikwambia kuwa ninaweza kurudi. Nimekuja na mtu ambaye alimuona Pascal katika siku za karibuni, nataka aone zile picha ili aweze kututhibitishia kama ndiye aliyemuona au la”
ITAENDELEA kesho usikose uhondo huu

No comments:

Post a Comment