Saturday, December 24, 2016

HADITHI, ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 12

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU 12
 
ILIPOISHIA
 
Walipotoka nje ya hospitali kila mmoja alipanda gari lake wakaondoka na wakaja kukutana tena kwenye kituo cha polisi cha Kinondoni.
 
Wakiwa ndani ya ofisi ya idara ya upelelezi Amour alimuonesha James pama la mtuhumiwa ambalo lilikuwa limehifadhiwa.
 
“Pama lake ndio hilo hilo” James akasema.
 
“Hili linamsaidia kuficha uso wake ndio maana analitumia”
 
Amour pia alimtolea simu ya mtuhumiwa. Aliingia sehemu ya picha na kumtaka amuoneshe picha za marehemu Maria ambazo mtu huyo alikuwa amejitumia.
 
James baada ya kuangalia picha zilizokuwemo aligundua picha tatu zilizokuwa kwenye simu ya Maria. Picha mbili Maria alikuwa amejipiga akiwa na James na picha moja alijipiga akiwa peke yake.
 
“Picha alizojitumia hajazifuta, ni hizi hapa” James alimwambia Amour huku akimuonesha picha hizo.
 
Amour akazitazama.
 
“Alihitaji picha hizi kwa ajili gani?”
 
“Anajua mwenyewe”
 
“Inaonekana alilenga kukuua na wewe”
 
“Pengine lakini amewahiwa yeye”
 
SASA ENDELEA
 
“Pia tulimkuta na vitambulisho viwili vya kazi. Kimoja kina jina la Pascal na kingine kina jina la Samwel. Bila shaka jina lake halisi ni Samwel lakini bado tunaendelea na uchunguzi”
 
“Nakushukuru sana Inspekta kwa uchunguzi wako. Hivi sasa ninasubiri afikishwe mahakamani”
 
“Tutamfikisha mahakamani baada ya uchunguzi wetu kukamilika na haitakuwa muda mrefu.
 
“Kwa hiyo mimi naenda kazini”
 
“Wewe nenda kazini, tutakapokuhitaji nitakupigia simu”
 
“Asante sana”
 
James alimpa mkono wa kumuaga Inspekata Amour akanyanyuka na kuondoka.
 
Mchana kutwa siku ile Amour alikuwa katika pilika pilika ya kutafuta ushahidi zaidi wa kumuhusisha mtuhumiwa aliyemkamata na mauaji ya Maria.
 
Alikwenda katika maktaba ya polisi ambapo alama za vidole za Pascal zilikuwa zikifanyiwa uchunguzi. Alibaini kwamba Pascal hakuwahi kukamatwa siku za nyuma na hakukuwa na kumbukumbu yoyote kwamba aliwahi kuhusika na matukio ya uhalifu.
 
Isipokuwa ilibainika kwamba moja ya alama za vidole iliyokutwa kwenye simu ya Maria siku alipouawa ilikuwa ni ya mtuhumiwa aliyekamatwa.
 
Mchana wa siku ile Amour alikwenda tena hospitali ya Muhimbili akiwa na polisi kadhaa.
 
Dhamira yake ilikuwa kumhoji mtuhumiwa huyo hapo hapo hospitali.
 
“Jina lako nani?’ Amour alimuuliza.
 
“Naitwa Pascal Lazza” Mtuhumiwa huyo alimjibu.
 
“Hapana, unadanganya. Tuambie jina lako halisi”
 
“Jina langu halisi ndilo hilo”
 
“Jana tulikukuta na vitambulisho viwili, kimoja kina jina la Samwel lakini vyote vina picha yako”
 
“Pia unaweza kuniita Samwel”
 
“Wewe ni jambazi uliyekubuhu, unatumia majina mawili”
 
“Ndiyo mkuu”
 
“Jina la Pascal Lazza ulilipata wapi?”
 
“Alinipa baba yangu”
 
“Wewe muongo mkubwa…”
 
Amour alimueleza kuwa jina hilo lilikuwa la mtu mwingine aliyekwisha kufa. Lakini yeye aliokota au aliiba shahada yake ya kupigia kura na kwenda kujisajili kwenye namba yake ya simu na hivyo kuendelea kulitumia jina hilo katika shughuli zake za uhalifu.
 
Mtuhumiwa huyo akanyamaza kimya kuonesha kuwa alichoambiwa kilikuwa kweli.
 
“Kwa hiyo wewe unaitwa Samweli?”
 
“Ndiyo mkuu”
 
“Unaishi wapi?”
 
“Ninaishi Temeke”
 
“Una mke”
 
“Ndiyo mkuu”
 
“Ulipata wapi bastola?”
 
“Niliinunua na nilikuwa katika mipango ya kuomba kibali cha kuimiliki kihalali”
 
Akionesha kuyapuuza maelezo yake, Amour alimuuliza swali jingine.
 
“Ni kwanini ulimuua Maria?”
 
Pascal alikunja uso na kumtazama Inspekta Amour.
 
“Maria! Maria ni nani?” akamuuliza huku akionesha mshangao.
 
“Ni msichana ambaye wewe ulimuua kwa kumpiga risasi nyumbani kwake Kinondoni hivi karibuni”
 
Pascal akatikisa kichwa.
 
“Tangu nizaliwe sijaua mtu. Huyo msichana simfahamu”
 
“Eti nini…?”
 
“Nakwambia ukweli Inspekta”
 
“Kwanini ulinikimbia pale ABC Club, Kimara?”
 
“Sikukukimbia, niliondoka na hamsini zangu”
 
“Na kwanini nilipokusimamisha hukutaka kusimama?”
 
“Nisimame wakati sikufahamu!”
 
“Kwanini ulitaka kunigonga na gari?”
 
“Ni bahati mbaya. Ni kwa sababu ulikaa mbele ya gari na mimi nilikuwa na haraka”
 
“Unadhani majibu yako yatakusaidia?”
 
Pascal akakenua mdomo kama aliyekuwa anataka kutabasamu.
 
“Kwanini afande?”
 
“Tutakutoa hapa twende ukatuoneshe nyumbani kwako kisha tutakurudisha hapa hapa”
 
“Nitashukuru sana”
 
Amour akakunja uso.
 
“Kitu gani kinachokufanya ushukuru?” akamuuliza.
 
“Kunikutanisha na mke wangu. Ninaamini mpaka sasa hajui niko wapi”
 
Amour akanyamaza. Alimfuata daktari na kuomba aondoke na mtuhumiwa wao kwa muda wa saa moja kisha atamrudisha tena. Aliporuhusiwa Amour aliwaagiza polisi aliokuwa nao wamtoe mtuhumiwa huyo na kumpakia kwenye gari.
 
Zoezi hilo lilipofanyika, Pascal aliwapeleka polisi hao nyumbani kwake Temeke.
 
Mke wa Pascal alishangaa kuona mume wake akipelekwa na polisi huku mguu wake mmoja ukiwa umefungwa bendeji na hauwezi kukanyaga.
 
“Wewe ndiye mke wa Pascal au Samwel?” Amour alimuuliza mwanamke huyo.
 
“Mume wangu ni Simon Puto” Mwanamke huyo alisema.
 
“Yuko wapi Simon Puto?”
 
Mwanamke huyo alimuonesha Pascal.
 
“Anaitwa Simon Puto?” Amour akamuuliza.
 
“Ndiyo”
 
“Majina ya Pascal na Samwel huyatambui?”
 
Mwanamke huyo alibetua mabega yake.
 
“Mume wangu haitwi hivyo”
 
ITAENDELEA

No comments:

Post a Comment