Saturday, December 10, 2016

HADITHI, ALIEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 4

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU 4
 
ILIPOISHIA
 
Lakini kusudio lake halikutimia. Aliweza kuwa nyuma yake katika mitaa miwili tu, kufika mtaa wa tatu gari hilo lilimchenga. Hakuliona tena. Ikambidi James arudi kazini kwake.
 
Wakati wote akiwa ofisini alijiuliza mtu yule ni nani na kwanini alitaka kujua kuhusu uchumba wake na Maria. Alipoona hapati jibu akaamua kuachana na mawazo hayo. Aliendelea na kazi zake hadi jioni alipotoka ofisini.
 
Alikwenda moja kwa moja nyumbani kwa Maria Kinondoni. Wakati anaikaribi nyumba ya Maria alishituka alipoliona gari la yule mtu aliyemuandama likiondoka nyumbani kwa Maria.
 
“Huyu mtu anafahamiana na Maria?” James akajiuliza bila kupata jibu. Alilisimamisha gari akashuka na kuelekea kwenye mlango wa nyumba ya Maria.
 
Aliusukuma mlango na kuingia ndani. Alimkuta Maria akitoka kuoga.
 
“Ndio unafika?” Maria akamuuliza.
 
Badala ya kumjibu James naye alimuuliza.
 
“Ulikuwa na mgeni yeyote humu ndani?” 
 
“Mgeni gani?’
 
“Yule mtu nilimuona akiondoka na gari hapo nje”
 
“Mtu yupi?”
 
“Yule niliyekueleza kwenye simu”
 
SASA ENDELEA
 
“Sijamuona, mimi nilikuwa naoga’
 
“Wakati nafika nilimuona anaondoka na gari”
 
“Mh! Mtu mwenyewe simjui na kwakweli hakuna mtu aliyeingia humu. Labda alibisha mlango, alipoona kimya akaondoka”
 
“Kama aliingia utajuaje wakati ulikuwa unaoga?”
 
Macho ya Maria yalikwenda kwenye simu yake aliyokuwa ameiweka kwenye kochi. Simu ilikuwepo.
 
“Sidhani kama aliingia…”
 
Maria aliichukua simu yake.
 
“Hii simu sikuiweka hivi…”
 
Maria alianza kuikagua simu yake kwa wasiwasi.
 
“Oh simu imetumika! Kuna picha zangu zimetumwa kwenye namba hii…!”
 
“Picha gani?”
 
“Picha nilizojipiga mwenyewe na picha tulizopiga tukiwa sote…hebu tazama”
 
James aliishika ile simu na kuangalia mfumo wa utumaji picha.
 
“Hii namba huifahamu?”
 
“Siijui” Maria alimjibu kwa wasiwasi na kuongeza.
 
“Huyo mtu aliingia kweli na kujitumia picha zangu sasa hivi”
 
“Lazima tumjue yule mtu ni nani na kwanini anatufuatafuta”
 
“Tutamjuaje na ameshakwenda zake”
 
“Muda ule nilimfuata na gari lakini alinichenga”
 
“Muda upi?”
 
“Pale hoteli. Nilipotoka nilimuona ameegemea gari akizungumza na simu. Aliponiona akaingia kwenye gari na kuondoka na mimi nikamfuata”
 
“Ukamuona anakwenda wapi?”
 
“Alinichenga tukapoteana. Sasa wakati naja kwako nikaona gari lake linaondoka”
 
Maria akatikisa kichwa.
 
“Sijui huyo mtu ni nani jamani!”
 
“Nitamchunguza na nitamjua”
 
James alibonyeza namba ya kutuma pesa. Akaingiza ile namba ya Pascal na kiasi cha pesa. Likaja jina la mmiliki wa namba ile. Lilikuwa Pascal Lazza.
 
“Anaitwa Pascal Lazza. Ndiye yeye. Aliniambia anaitwa Pascal”
 
“Hebu mpigie umuulize”
 
James akaipiga ile namba.
 
Sauti ya mtandaoni ikamwambia kuwa namba haipatikani.
 
“Ameshazima simu. Namba yake haipatikani”
 
“Mimi sipendi kuandamwa andamwa namna hii!”
 
“Nitaijaribu wakati mwingine. Ngoja niichukue”
 
James aliiweka ile namba kwenye simu yake akairudisha simu ya Maria.
 
Maria aliingia chumbani kwake na kuvaa kisha akarudi sebuleni.
 
“Mimi nafikiri kuna kitu, si bure” James alimwambia Maria.
 
“Kama kitu gani?” Maria alimuuliza kwa wasiwasi.
 
“Nafikiri tatizo liko kwenye uchumba wetu”
 
“Una maana kuna watu hawataki tuoane?”
 
“Kitu kama hicho”
 
“Wanajidanganya James, sisi tutaoana tu. Hakuna wa kutuzuia. Watakuuliza maswali, wataiba picha lakini haitasaidia”.
 
                                ***********
 
Siku chache zilizopita, Mahakama ilikuwa imemuachia huru Maria baada ya kutomkuta na hatia katika kesi iliyokuwa ikimkabili ya kupoteza kwa makusudi faili la kesi ya mshitakiwa kwa lengo la kupoteza ushidi.
 
Ingawa hakuwa amerudishwa kazini, alishukuru kesi hiyo kuisha kwa vile ilikuwa imemuweka roho juu. Alijua kuwa alikuwa ametenda kosa lakini alitoswa na mtu ambaye alimshawishi kutenda kosa hilo bila kujua kuwa lingemletea balaa.
 
Licha ya kutorudishwa kazini, kule kusalimika na kifungo kulimuweka katika nafasi iliyomuwezesha kufunga uchumba na James, kijana ambaye alimpenda kidhati moyoni mwake.
 
Alijiambia kama atakosa kazi lakini atapata mume aliyempenda hakutakuwa na tatizo.
 
Alijitahidi sana kumficha James habari ya kesi yake, ingawa James alifahamu kuwa Maria alikuwa na kesi lakini hakuweza kuijua kwa undani kwa vile kesi hiyo iliisha siku chache tu kabla ya uchumba wao.
 
Siku iliyofuata baada ya siku ile ambayo walitokewa na Pascal, walianza kupanga harusi yao. Waliazimia kuoana siku chache zijazo wakati Jemes akiwa kwenye likizo. Na walianza maandalizi mapema.
 
Ilikuwa ni mwishoni mwa wiki ileile wakiwa kwenye maandalizi ya harusi yao, James akapokea meseji ya kushitusha kutoka kwa Maria. Ilikuwa saa mbili usiku. James alikuwa amemaliza kuvaa baada ya kutoka kuoga. Simu yake ilipotoa mlio wa kupokea meseji aliichukua na kuitazama. Akaona meseji iliyotoka kwa Maria.
 
Alipoifungua meseji hiyo iliandikwa.
 
“James njoo haraka yule mtu amekuja”
 
ITA ENDELEA kesho hapa hapa usikose

No comments:

Post a Comment