Monday, December 12, 2016

HADITHI, ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 5

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU 5
 
ILIPOISHIA
 
Ingawa hakuwa amerudishwa kazini, alishukuru kesi hiyo kuisha kwa vile ilikuwa imemuweka roho juu. Alijua kuwa alikuwa ametenda kosa lakini alitoswa na mtu ambaye alimshawishi kutenda kosa hilo bila kujua kuwa lingemletea balaa.
 
Licha ya kutorudishwa kazini, kule kusalimika na kifungo kulimuweka katika nafasi iliyomuwezesha kufunga uchumba na James, kijana ambaye alimpenda kidhati moyoni mwake.
 
Alijiambia kama atakosa kazi lakini atapata mume aliyempenda hakutakuwa na tatizo.
 
Alijitahidi sana kumficha James habari ya kesi yake, ingawa James alifahamu kuwa Maria alikuwa na kesi lakini hakuweza kuijua kwa undani kwa vile kesi hiyo iliisha siku chache tu kabla ya uchumba wao.
 
Siku iliyofuata baada ya siku ile ambayo walitokewa na Pascal, walianza kupanga harusi yao. Waliazimia kuoana siku chache zijazo wakati Jemes akiwa kwenye likizo. Na walianza maandalizi mapema.
 
Ilikuwa ni mwishoni mwa wiki ileile wakiwa kwenye maandalizi ya harusi yao, James akapokea meseji ya kushitusha kutoka kwa Maria. Ilikuwa saa mbili usiku. James alikuwa amemaliza kuvaa baada ya kutoka kuoga. Simu yake ilipotoa mlio wa kupokea meseji aliichukua na kuitazama. Akaona meseji iliyotoka kwa Maria.
 
Alipoifungua meseji hiyo iliandikwa.
 
“James njoo haraka yule mtu amekuja”
 
SASA ENDELEA
 
Kwa vile alikuwa ameshamaliza kuvaa alitoka haraka akajipakia kwenye gari lake na kuondoka. Wakati akiendesha kwa mwendo kasi James alikuwa ameazimia atakapofika ampige yule mtu kisha amfikishe polisi ili akajieleze yeye ni nani na kwanini anawafuatilia.
 
Alikuwa anakaribia kufika, simu yake ilipoita. Alipoitazama aliona alikuwa Maria. Akaipokea haraka.
 
“Hallo Maria!”
 
“Haaa….!” Sauti ya Maria ilisikika kisha ikakata.
 
James akaitazama simu na kuona ilikatwa ghafla. Akampigia Maria lakini simu ya Maria ikawa haipatikani. Akaiweka simu na kuendelea kulikimbiza gari hadi katika mtaa aliokuwa akiishi Maria.
 
Mbele ya nyumba ya Maria aliliona gari la Pascal lakini taa ya nje ya nyumba ya Maria ilikuwa imezimwa. Kulikuwa kiza. Alilisimamisha gari lake nyuma ya gari hilo. Wakati anafungua mlango ili ashuke alimuona Pascal akijipakia kwenye gari.
 
James alishuka na kumfuata. Pascal akawahi kuliondoa gari na kuondoka kwa kasi. James akakimbilia kwenye mlango wa nyumba ya Maria ambao aliukuta uko wazi. Akaingia ndani.
 
Kwenye sebule hakukuwa na mtu. James akasimama na kuita.
 
“Maria!
 
Hakukuwa na jibu, nyumba ilikuwa kimya. James alikwenda kwenye mlango wa chumba cha Maria akausukuma na kuingia ndani.
 
Alichokutana nacho kilimfanya atoe macho na kuacha mdomo wazi. Maria alikuwa amelala chini, damu nyembamba ilikuwa ikimtoka kifuani na kuchirizika hadi sakafuni. James alichutama na kumuinua upande wa kichwani.
 
Maria alikuwa akipumua kwa taabu.
 
“Maria umepatwa na nini?” James akamuuliza kwa sauti iliyotaharuki.
 
Maria alijitahidi kuinua mdomo akatamka kwa taabu.
 
“Pascal…Pascal…amenipiga risasi…ameniambia alikuwa akinitafuta sana na amethibitisha kuwa ni mimi…”
 
“Amekupiga risasi kwa kosa gani lakini…?”
 
Nguvu zilikuwa zimemuishia Maria. Hakuweza kutamka tena. Akaguna na kufumba macho.
 
“Maria…Maria…!” James akamuita huku machozi yakimtoka.
 
Maria alikuwa kimya.
 
“Maria!” James alimuita kwa sauti ya juu huku akimtikisa.
 
Maria alikuwa kama hakuwepo tena. Uliokuwepo pale ulikuwa ni mwili mtupu usio na uhai.
 
“Maria unanitoka hivi hivi wakati tulibakisha siku chache tu tuoane na ulinisisitizia kuwa tutaoana…Maria…” James alisema kwa hasira na uchungu huku matone ya machozi yake yakiangukia kwenye uso wa Maria.
 
“Ni nani huyu Pascal? Umemkosea nini Maria?” James aliendelea kujisemea peke yake.
 
“Siamini kama umekufa Maria” James aliendelea kusema peke yake.
 
Aliulaza chini mwili wa Maria kisha akalipapasa shavu lake.
 
“Buriani Maria” akamwambia na kuongeza. “Nakuhakikishia kuwa nitamsaka Pascal na nitamkomoa”
 
Akanyanyuka na kugeuka kwenye mlango ili atoke lakini akautazama tena mwili wa aliyekuwa mchumba wake.
 
“Tangulia Maria. Mbele yako nyuma yangu. Nitamsaka Pascal!”
 
Aliposema hivyo aliinua hatua na kutoka mbio mle chumbani. Aliufungua mlango wa nje akalikimbilia gari lake. Alitumia sekunde tatu tu kufungua mlango, kujipakia na kuliwasha gari hilo na kuondoka kwa kasi.
 
Alilikimbiza gari hilo katika mitaa kadhaa ya Kinondoni akilitafuta gari la Pascal. Alikuwa ameapa kama atamuona zitakuwa za Pascal au zake. Lakini aligundua kuwa gari hilo lilikuwa limeshafika mbali na asingeweza kuliona tena.
 
Akageuza njia na kuelekea kituo cha polisi cha Kinondoni. Dakika chache tu baadaye akawa anazungumza na Inspekta Amour aliyekuwa msaidizi wa mkuu wa kituo hicho.
 
Baada ya kumueleza jinsi mauaji ya mchumba wake yalivyotokea, timu ya polisi ikiongozwa na inspekta huyo ilitinga nyumbani kwa Maria.
 
James aliwaongoza hadi kwenye chumba cha Maria na kuwaonesha maiti ya Maria iliyokuwa imelala kimya. Kama si ile damu iliyokuwa imevuja kwenye kifua chake, mtu yeyote angemdhania kuwa alikuwa mzima bali alikuwa amelala.
 
Polisi wakaanza kushughulika na kuchukua vipimo ikiwa ni pamoja na kumpiga picha marehemu, kuchukua alama za vidole kwenye milango na kumpekua marehemu.
 
Baada ya zoezi hilo lililochukua takriban dakika sitini, Mwili wa Maria ulipakiwa kwenye gari la polisi kupelekwa hospitali. James akatakiwa kufika kituo cha polsi kwa ajili ya kutoa maelezo zaidi.
 
Aliyemhoji James alikuwa inspekta Amour.
 
“Unaitwa nani?”
 
“Naitwa James Matei”
 
“Umri wako?”
 
“Miaka thelathini na miwili”
 
“Marehemu alikuwa anaitwa nani?”
 
“Anaitwa Maria Faustus Wimbi”
 
“Ulijuana lini na Maria?”
 
“Miezi michache tu iliyopita”
 
“Hebu nieleze mlivyokutana kwa mara ya kwanza”
 
James akaeleza alivyokutana na Maria kwa mara ya kwanza hadi walipofikia kufunga uchumba.
 
“Nani unamshuku kumuua mchumba wako?” Inaspekta Amour akaendelea kumuuliza.
 
“Ninamshuku mtu mmoja anayejiita Pascal”
 
“Kwa nini unamshuku mtu huyo?’
 
James akaeleza kwa kirefu sababu za kumshuku mtu huyo. Alieleza alivyokutana naye kwa mara ya kwanza kwenye hoteli. Na pia alivyofika nyumbani kwa Maria na kujirushia picha za Maria kwenye simu yake na kisha kuondoka.
 
Akaendelea kueleza jinsi Maria alivyomtumia meseji usiku ule akimueleza kuwa mtu huyo alikuwa amefika nyumbani kwake ambapo James aliwasha gari na kuwafuata. Lakini njiani Maria akampigia simu. Kabla ya kuongea lolote, simu ikakatwa. Na yeye alipojaribu kumpigia simu ikawa haipatikani.
 
“Nilipofika nyumbani kwa Maria nilikuta gari la yule mtu, wakati nashuka kwenye gari nikamuona yule mtu anajipakia kwenye gari lake, nikamfuata lakini kabla ya kumfikia aliondoa gari kwa kasi.
 
“Taa ya nje ya nyumbani kwa Maria ilikuwa imezimwa. Nilipoingia ndani ndipo nilipomkuta Maria amelala chini chumbani kwake. Akaniambia kwa kauli yake kuwa amepigwa risasi na Pascal”
 
“Uliwahi kumuuliza ni kwanini Pascal alimpiga risasi?” Inspekta Amour alimuuliza James.
 
“Nilimuuliza lakini hakuwahi kunijibu, wakati wake ulikuwa umeshafika”
 
ITAENDELEA kesho hapahapa usikose

No comments:

Post a Comment