Wednesday, December 14, 2016

ALIYEMUUA MCHUMBWA WANGU SEHEMU YA 6

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU 6
 
ILIPOISHIA
 
James akaeleza kwa kirefu sababu za kumshuku mtu huyo. Alieleza alivyokutana naye kwa mara ya kwanza kwenye hoteli. Na pia alivyofika nyumbani kwa Maria na kujirushia picha za Maria kwenye simu yake na kisha kuondoka.
 
Akaendelea kueleza jinsi Maria alivyomtumia meseji usiku ule akimueleza kuwa mtu huyo alikuwa amefika nyumbani kwake ambapo James aliwasha gari na kuwafuata. Lakini njiani Maria akampigia simu. Kabla ya kuongea lolote, simu ikakatwa. Na yeye alipojaribu kumpigia simu ikawa haipatikani.
 
“Nilipofika nyumbani kwa Maria nilikuta gari la yule mtu, wakati nashuka kwenye gari nikamuona yule mtu anajipakia kwenye gari lake, nikamfuata lakini kabla ya kumfikia aliondoa gari kwa kasi.
 
“Taa ya nje ya nyumbani kwa Maria ilikuwa imezimwa. Nilipoingia ndani ndipo nilipomkuta Maria amelala chini chumbani kwake. Akaniambia kwa kauli yake kuwa amepigwa risasi na Pascal”
 
“Uliwahi kumuuliza ni kwanini Pascal alimpiga risasi?” Inspekta Amour alimuuliza James.
 
“Nilimuuliza lakini hakuwahi kunijibu, wakati wake ulikuwa umeshafika”
 
SASA ENDELEA
 
“Gari la Pascal ni aina gani?’
 
“Ni hizi Toyota Corolla ya rangi ya kijani”
 
“Nipatie namba yake ya usajili”
 
“Sikuwahi kuzikariri”
 
“Ulisema uliwahi kuchukua namba yake ya simu kutoka kwenye simu ya Maria, nipatie ile namba”
 
“Nimeshaipiga mara nyingi lakini haipatikani” James alimwambia Inspekta baada ya kumsomea namba hiyo kutoka kwenye simu yake.
 
“Hii ni kazi yetu sisi, sisi tunaamini kuwa tutampata”
 
“Nitashukuru sana kama atapatikana, na mimi mwenyewe pia ninamtafuta”
 
“Sawa. Wewe ndio umemuona, unaweza kututajia yukoje”
 
“Ni mrefu, mweusi na anavaa pama jeusi”
 
“Wakati ulipomuona akijipakia kwenye gari leo alikuwa amevaa nini?”
 
“Alivaa suti nyeusi na hata siku ya kwanza nilipomuona alikuwa amevaa suti nyeusi”
 
“Sawa. Sisi tutamtafuta lakini tunaomba ushirikiano wako. Ukisikia tetesi yoyote kuhusu yeye usisite kuja kutufahamisha. Au ukimuona mahali haraka tupigie simu”
 
“Sawa” James alimkubalia lakini ndani ya moyo wake alijiambia vingine.
 
Alijiambia kama atamuona mtu huyo mahali popote atamalizana naye hapo hapo na hatahitaji kuwaarifu polisi. Alikuwa na uhakika kuwa uwezo wa kummaliza alikuwa nao.
 
“Sasa unaweza kwenda lakini kesho asubuhi ufike tena hapa kituoni”
“Nitafika”
 
James akaondoka na kurudi Kinondoni nyumbani kwa marehemu. Nyumba ilikuwa imefurika ndugu na jamaaa. Wazazi pamoja na kaka wa marehemu ambao walipata taarifa hizo mapema walikuwa miongoni mwa waombolezaji waliokuwa wakibubujikwa na machozi.
 
Mara tu baada ya James kuondoka kituo cha polisi, Inaspekta Amour alipokea taarifa ya uchunguzi wa alama za vidole zilizopatikana kwenye vitasa vya milango nyumbani kwa Maria na pia kwenye simu yake.
 
Uchunguzi huo wa alama za vile ulionesha kuwa kulikuwa na aina tatu za alama hizo zilizopatikana kwenye vitasa vya milango na kwenye simu ya Maria.
 
Kazi ya kwanza ya Inspekta Amour ilikuwa ni kutafuta alama hizo zilikuwa ni za akina nani. Usiku huo huo alikwenda hospitali ya Muhimbili ambako mwili wa marehemu Maria ulihifadhiwa. Alifuatana na kachero Stambuli ambaye alikuwa mtaalamu wa uchunguzi wa alama za vidole.
 
Walipofika Muhimbili walichukua alama za vidole vya Maria. Alama hizo zilikujalinganishwa na alama zilizopatikana nyumbani kwa Maria ambapo ilifahamika kwamba aina moja ya alama hizo ilikuwa ni ya marehemu mwenyewe.
 
Asubuhi yake James alipofika kituo cha polisi, alama zake za vidole zikachukuliwa na kupelekwa kufanyiwa uchunguzi. Ikagundulika kuwa aina ya pili ya alama zilizokutwa nyumbani kwa marehwmu, ilikuwa alama ya vidole vya James.
 
Polisi walishuku kwamba aina ya tatu ya alama hizo ilikuwa ni ya Pascal aliyekuwa akituhumiwa kwa mauaji.
Kazi ya pili ya polisi ilikuwa ni kulinganisha alama hizo zilizoshukiwa kuwa za Pascal na alama za wahalifu mbali mbali waliowahi kukamatwa na polisi. Dhamiri ya polisi ilikuwa ni kuona kama alama hizo zitalingana na alama za mhalifu mmojawapo.
 
Zoezi hilo lilifanyika makao ya polisi ambako ndiko kulikokuwa na maktaba ya alama zote za wahalifu waliowahi kukamatwa hapa nchini.
 
 Inspekta Amour aliamini kuwa endapo alama hizo zitagundulika kuwa ni za mmoja wa wahalifu waliowahi kukamatwa, wataweza kumgundua Pascal mara moja kwani kwa kawaida alama hizo uhifadhiwa pamoja na picha ya muhusika, jina lake na rekodi yake
 
Kwa hiyo polisi wataweza kuiona picha ya Pascal pamoja na rikodi yake. Kama picha hiyo itathibitishwa na James kuwa ndiye Pascal mwenyewe, itakuwa ni kazi rahisi kumkamata kwani polisi watajua atapatikana wapi kwa mijubu wa kumbukumbu zake walizonazo.
 
Kutokana na uwingi wa alama za vidole za wahalifu zilizokuwa maktaba ya polisi, zoezi ya kutafuta alama hizo ni za nani lilitarajiwa kuchukua zaidi ya siku moja.
 
Baada ya maziko ya Maria kufanyika Kinondoni, James alijiambia alikuwa na kazi moja tu ya kumtafuta mtu aliyemuua mchumba wake na kumkatisha ndoto yake njema ya kuoana na msichana huyo.
 
Mara kwa mara James alikuwa akiijaribu ile namba ya Pascal lakini mara zote alizoipiga ilikuwa haipatikani. Sambamba na kumsaka Pascal kwenye simu alikuwa akilitafuta lile gari mitaani akiamni kuwa kama litakuwa bado liko Dar kuna siku atanasa.
 
Wakati wakisubiri uchunguzi wa alama za vidole uliokuwa ukifanywa na polisi wa makao makuu ya polisi, Inspekta Amour alikuwa akiifuatilia ile namba ya Pascal. Alifika katika kampuni ya simu iliyomiliki namba ile na kutaka kupata rikodi yake.
 
Inspekta Amour alifahamishwa kuwa ilisajiliwa kwa jina la Pascal Lazza wilaya ya Temeke mwaka mmoja uliopita. Kwa mujibu wa kivuli cha shahada ya Pascal ambacho kilionesha alikuwa mfanyakazi wa Kampuni ya mabati ya jijini, Pascal alikuwa mkazi wa Temeke.
 
Baada ya kupata maelezo yote aliyohitaji, Inspekta Amour aliona kazi ya kumtafuta Pascal itakuwa fupi. Ni kiasi tu cha kwenda katika kampuni ya mabati kumuulizia na kumtia mikononi.
 
Inspekta Amour alitoka katika ofisi ya kampuni ya simu akiwa na furaha. Alikuwa na uhakika kwamba angeweza kumkamata Pascal siku ileile.
 
Alipotoka kwenye ofisi ya kampuni ya simu, alikwenda Temeke ambako ndiko kilipokuwa kiwanda hicho cha mabati. Kwanza alifika kituo cha polsi cha Temeke akaomba polisi watatu wa kituo hicho ili kwenda kumkamata Pascal.
 
Alipowapata polisi hao alikwenda nao kwenye kiwanda hicho na kuonana na meneja wa kiwanda aliyekuwa mtu mwenye asili ya kiasia.
 
“Kuna mfanyakazi wako mmoja anaitwa Pascal Lazza” Inspekta Amour alimwambia meneja huyo aliyeonekana kushituka.
 
“Pascal Lazza alikuwa mfanyakazi wetu lakini kwa sasa hafanyi kazi hapa” Meneja huyo alijibu huku akitikisa kichwa.
 
“Anafanya wapi?”
 
“Sijui, lakini hapa kwetu alishaacha kazi”
 
Amour akiwa amepatwa na mshangao kutokana na jibu hilo aliwatazama polisi wenzake kabla ya kuuliza.
 
“Aliacha kazi lini?”
 
“Kama miezi sita iliyopita”
 
“Aliacha kazi au alifukuzwa kazi?’
 
“Aliacha kazi mwenyewe”
 
“Tulikuwa tunamtafuta, unadhani tutampata wapi?”
 
“Sijui”
 
Jibu hilo la mkato liliwavunja nguvu polisi hao ambao walilazimika kuondoka ofisini hapo. Dodosa dodosa ya Inspekta Amour kwenye mitaa ya Temeke ilimfikisha katika nyumba ambayo ilielezwa alikuwa akiishi Pascal.
 
Inspekta Amour alipolitaja jina la Pascal, mwanamke aliyekuwa amemkaribisha kwenye nyumba hiyo alitoa tabasamu la huzuni.
 
“Mbona Pascal sasa hivi ni marehemu, Pascal alishakufa” Mwanamke huyo alimwambia Amour aliyeonekana kushangaa.
 
“Alikufa lini?”
 
“Sasa ni karibu miezi mitatu”
 
“Unamzungumzia Pascal Lazza aliyekuwa akifanya kazi kiwanda cha mabati?”
 
“Ndiye yeye ninayekwambia, alishakufa. Mimi hapa ninayekueleza ni mjane wake”
 
“Ninapata taabu kuamini kwa sababu Pascal amekuwa akionekana na anawasiliana na watu”
 
Mwanamke huyo akashituka.
 
“Pascal ameonekana wapi?”
 
ITAENDELEA

No comments:

Post a Comment