Saturday, December 24, 2016

HADITHI, ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 11

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU 11
 
ILIPOISHIA
 
Licha ya kwamba mtu huyo alikuwa amepigwa risasi, polisi mmoja alimpiga teke kisha akamtia pingu.
 
“Hayaaminiki haya, yanafanya ujambazi kwa kutumia uchawi. Lazima tulitie pingu”
 
“Inuka” Polisi mmoja alimwambia.
 
“Acha tulipekue kwanza, linaweza kuwa na bastola” Mwenzake akamwambia.
 
“Bastola yake hii hapa, nimeshaichukua”
 
Polisi aliyemtia pingu alipoiona bastola ya mtu huyo alihamaki akampiga kibao.
 
“Hili liuaji kweli, lina bastola!”
 
“Mpakieni kwenye gari apelekwe kituoni kisha apelekwe hospitali” Amour aliwambia polisi hao.
 
“Inuka mwenyewe!” Polisi mmoja akamuamuru.
 
Mtu huyo alijaribu kuinuka lakini hakuweza.
 
“Pumbavu!” Polisi mmoja alimwambia na kumpiga kibao.
 
Walimshika mikono wakamburuza na kwenda kumrusha kwenye gari lao.
 
“Mpelekeni kituoni, mimi nakuja. Ninakwenda kuchukua gari langu” Amour aliwambia.
 
Wakati anakwenda kulichukua gari lake ABC Club, Amour alimpigia mkuu wa kituo cha polisi cha Kinondoni na kumueleza kuwa alikuwa amemkamata mtu waliyekuwa wanamtafuta aliyehusika na mauaji ya Maria.
 
“Umemkamata wapi?” Mkuu huyo aliuliza kwenye simu.
 
Amour alimueleza tukio zima lilivyotokea.
 
SASA ENDELEA
 
“Kwa sasa hivi yuko wapi?”
 
“Yuko kituo cha polisi cha Kimara. Tunaandikisha maelezo yake kabla ya kumpeleka hospitali”
 
“Sawa. Mimi nakuja huko huko kumuona”
 
“Sawa afande”
 
Amour akakata simu.
 
Dakika chache baadaye akawa amefika kituo cha polisi cha Kinondoni. Mtuhumiwa aliyekamatwa alikuwa ameshapekuliwa, alikutwa na simu moja, pesa taslim shilingi laki moja na vitambuliso viwili vilivyokuwa na majina tofauti, kimojawapo kikiwa na jina la Pascal Lazza.
 
“Tulikuwa tunakusubiri uandike maelezo” Mmoja wa polisi wa kituo hicho alimwambia Amour.
 
Baada ya Amour kukamilisha zoezi hilo, mkuu wa kituo cha polisi cha Kinondoni akawasili na kumuona mtuhumiwa aliyekuwa amekamatwa.
 
“Sasa moja kwa moja apelekwe hospitali ya Muhimbili. Atakuwa chini ya ulinzi wa polisi” akaagiza.
 
                                        ************
 
Kulipokucha asubuhi James alikuwa ameshajiandaa kwenda kazini. Wakati anatoka ndipo simu yake ilipoita.
 
Alipoona namba ya Inspekta Amour akaipokea haraka.
 
“Hello Inpekta!”
 
“Habari ya asubuhi?” Sauti ya Inpekta Amour ikasikika kwenye simu.
 
“Nzuri, za huko”
 
“Huku tuna habari mpya, yule mtu tumemkamata jana usiku!”
 
“Nani, Pascal?”
 
“Ndiyo Pascal”
 
James alishituka sana.
 
“Unaniambia kweli Inspekta?”
 
“Kweli kabisa. Nimemkamata mimi mwenyewe”
 
“Umemkamatia wapi?”
 
“Nilimkamata kwenye klabu moja ya usiku pale Kimara”
 
“Ninahitaji kumuona”
 
“Ndiyo sababu nimekupigia simu. Ninataka twende Muhimbili Hospital, ukamtambue”
 
“Yuko Muhimbili?”
 
“Nilimpiga risasi ya mguu. Amelazwa Muhimbili”
 
“Sasa nije hapo kituoni au…?”
 
“Itakuwa vyema kama utakuja hapa”
 
“Basi nakuja sasa hivi”
 
“Sawa”
 
James badala ya kutoka kwenda kazini, aliwasha gari lake akaenda kituo cha polisi. Alikutana na Inspekta Amour nje ya kituo. Alisalimiana naye na kupeana naye mkono.
 
“Umekuja na gari yako, sasa tangulia Muhimbili. Mimi nakuja” Amour akamwambia James.
 
“Nikusubiri nje?’
 
“Ndiyo nisubiri. Hutaweza kuingia peke yako”
 
“Sawa”
 
James akarudi kwenye gari lake akaliwasha na kuelekea Muhimbili.
 
Wakati anafika Muhimbili aliliona gari la Inspekta Amour likiwa nyuma yake. Alishuka kwenye gari na Amour akashuka. Wakafuatana hadi ndani ya jengo hilo la hospitali. Kwanza walikwenda katika ofisi ya madaktari wakakutana na daktari aliyekuwa akimshughulikia mtuhumiwa wao.
 
“Umekuja Inspekta?” Daktari huyo akamuuliza Inspekta Amour.
 
“Ndiyo nimekuja na mtu ambaye ninataka amtambue ili tujue kama ndiye mtu tuliyekuwa tunamtafuta”
 
“Sawa. Nitawapeleka akamuone”
 
Walitoka pamoja.
 
“Vipi, hali yake inaendelea vizuri?” Amour akamuuuliza daktari huyo.
 
“Anaendelea vizuri. Kwa bahati njema ile risasi haikuvunja mfupa. Iliingia kwenye nyama. Baada ya kuitoa tumemuweka dawa na kumfunga bendeji”
 
“Ni vizuri ili apone haraka tumfikishe mahakamani”
 
Katika chumba alichokuwa amelazwa mtu huyo kulikuwa na askari mwenye bunduki aliyekuwa akimlinda.
 
Walipoingia kwenye chumba hicho, Amour na James walimkuta mtu huyo akiwa amefungwa bendeji mguuni. Alikuwa ametulia kimya akiwaza.
 
James alipomuona tu hakungoja kuulizwa.
 
“Ndiye yeye” alisema akionesha uhakika wa asilimia mia moja.
 
Amour akamtazama James.
 
“Una uhakika kwamba ndiye yeye?” akamuuliza.
 
“Inspekta umemaliza kazi, sijui nikupe zawadi gani”
 
“Wewe utakuwa shahidi wetu muhimu kwa sababu kwa mujibu wa maelezo yako umemuona mtuhumiwa mara mbili”
 
“Nina hakika naye na nilisema sitamsahau…”
 
Aliposema hivyo James alikuwa amekunja ngumi mkono mmoja akakipiga ngumi kadhaa kiganja chake cha mkono mwingine kusisitiza maneno yake.
 
“Basi imetosha, sasa turudi kituoni”
 
Walimuaga daktari na kuondoka.
 
“Inspekta umefanya kazi nzuri, ninakusifu” James alimwambi Amour.
 
“Hizi ni kazi zetu” Amour akamjibu huku akitabasamu kupewa sifa.
 
“Mimi nilidhani asingepatikana tena”
 
“Ulikosea kudhani hivyo. Sisi polisi tunajua kwamba mbio za sakafuni huishia ukingoni. Wewe fanya uhalifu wako na kuwa mjanja wa kuwakwepa polisi lakini ujue mbio zako zitaishia ukingoni. Iko siku utakamatwa tu”
 
“Ni kweli mbio za sakafuni huishia ukingoni” James aliikariri methali ya Inspekta Amour.
 
Walipotoka nje ya hospitali kila mmoja alipanda gari lake wakaondoka na wakaja kukutana tena kwenye kituo cha polisi cha Kinondoni.
 
Wakiwa ndani ya ofisi ya idara ya upelelezi Amour alimuonesha James pama la mtuhumiwa ambalo lilikuwa limehifadhiwa.
 
“Pama lake ndio hilo hilo” James akasema.
 
“Hili linamsaidia kuficha uso wake ndio maana analitumia”
 
Amour pia alimtolea simu ya mtuhumiwa. Aliingia sehemu ya picha na kumtaka amuoneshe picha za marehemu Maria ambazo mtu huyo alikuwa amejitumia.
 
James baada ya kuangalia picha zilizokuwemo aligundua picha tatu zilizokuwa kwenye simu ya Maria. Picha mbili Maria alikuwa amejipiga akiwa na James na picha moja alijipiga akiwa peke yake.
 
“Picha alizojitumia hajazifuta, ni hizi hapa” James alimwambia Amour huku akimuonesha picha hizo.
 
Amour akazitazama.
 
“Alihitaji picha hizi kwa ajili gani?”
 
“Anajua mwenyewe”
 
“Inaonekana alilenga kukuua na wewe”
 
“Pengine lakini amewahiwa yeye”
 
ITAENDELEA

No comments:

Post a Comment