Friday, December 16, 2016

HADITHI, ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 8

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU 8
 
ILIPOISHIA
 
“Nilionana na mwanamke mmoja aliyenieleza kuwa alikuwa mke wa Pascal. Mwanamke huyo alinipa maelezo ya kunishangaza. Aliniambia kuwa Pascal alikwisha kufa miezi miwili iliyopita katika ajali ya gari iliyotokea Kimara”
 
“Amedanganya! Pascal yuko hai na ndiye aliyemuua mchumba wangu” James alidakia.
 
“Amenithibitishia kuwa Pascal amekufa kweli. Alinionesha picha za magazeti. Ile habari iliandikwa kwenye magazeti na picha ya Pascal nimeiona ni kati ya watu waliokufa”
 
“Kwani wewe unamjua Pascal? Ulimuona wapi?”
 
“Niliona picha yake kwenye kivuli cha shahada alichosajilia simu yake”
 
James akatikisa kichwa.
 
“Haiwezekani!”
 
“Ninajua kuwa haiwezekani ndio sababu nimekufuata hapa”
 
James akanyamaza na kumtazama Inspekta huyo.
 
“Ninataka twende nyumbani kwa yule mwanamke ukaitazame ile picha halafu uniambie ndiye Pascal uliyemuona wewe”
 
“Sawa. Twende hata sasa hivi”
 
James alirudi kufunga mlango kabla ya kuondoka na gari alilokwenda nalo Inspekta Amour.
 
“Mimi naamini kuwa Pascal yuko hai. Kunaweza kuwepo na mbinu za kihalifu za kuonesha kuwa amekufa ili polisi wasiendelee kumtafuta” James alimwambia Amour kwenye gari.
 
“Wewe ndiye utakayetuthibitishia Pascal yuko hai au amekufa”
 
Walipofika Temeke kwenye nyumba ambayo Inspekta Amour alifika kwa mara ya kwanza na kuzungumza na mwanamke aliyemueleza kuwa Pascal alikuwa amekufa, walikaribishwa ndani.
 
“Umerudi tena?” Mwanamke huyo alimuuliza Inspekta Amour.
 
“Ndio. Nilikwambia kuwa ninaweza kurudi. Nimekuja na mtu ambaye alimuona Pascal katika siku za karibuni, nataka aone zile picha ili aweze kututhibitishia kama ndiye aliyemuona au la”
 
SASA ENDELEA
 
“Kwa hiyo nikatoe zile picha niwaletee”
 
“Tuletee yale magazeti ulionionesha”
 
Mwanamke akaingia chumbani. Baada ya muda kidogo alitoka akiwa ameshika yale magazeti.
 
“Haya hapa” alisema na kumpa Inspekta Amour.
 
Amour aliyachukua akayakunjua na kumuonesha picha ya Pascal iliyokuwa imechapwa kwenye gazeti mojawapo.
 
“Mtu uliyemuona ni huyu hapa?”
 
James alimtazama kisha hapo hapo alitikisa kichwa.
 
“Huyu siye Pascal ninayezungumza mimi, huyu ni mtu mwingine kabisa”
 
Amour alimuonesha James picha ya Pascal iliyokuwa imetundikwa kwenye ukuta.
 
“Picha yake nyingine ile pale, hebu itazame vizuri”
 
James akaitazama picha hiyo iliyokuwa juu.
 
“Ile na hii ni moja tu”
 
“Siye?”
 
“Siye kabisa”
 
Amour akakubali kwa kichwa.
 
“Sasa huyo ndiye Pascal aliyedaiwa kufa katika ajali ya gari lakini picha yake ndio iko kwenye usajili wa namba ya Pascal uliyemuona wewe”
 
“Imekuwaje?’
 
“Tunahitaji uchunguzi. Hebu twende kule kampuni ya simu”
 
Amour alimuaga yule mwanamke akatoka na James. Walifika katika ofisi ya kampuni ya simu. Amour aliomba apatiwe kivuli cha shahada ya Pascal iliyoko kwenye usajili wa namba yake ya simu.
 
Amour alipopatiwa kivuli hicho alirudi Temeke na James na kukutana tena na yule mwanamke.
“Unaona fotokopi hii iko kwenye usajili a namba ya Pascal…”
 
“Shahada iliyotolewa kopi ilipotea miaka mingi, Pscal alishatoa ripoti polisi” Mwanamke huyo alidakia wakati Amour akimueleza.
 
“Hata kama shahada yake ilipotea lakini nani aliyesajili namba hii ya simu?”
 
“Siwezi kujua. Kwanza namba ya simu iliyopo hapo haikuwa namba ya marehemu. Marehemu hakuwahi kusajili namba kwa shahada yake”
 
Inspekta Amour akatazamana na James kisha akamtazama yule mwanamke.
 
“Nimekuelewa. Asante sana” alimwambia na kumtazama tena James.
 
“Twenzetu James”
 
Walipokuwa kwenye gari wakirudi Kinondoni Amour alimuuliza James.
 
“Umejua ni nini kimefanyika?”
 
“Bado sijajua”
 
“Muuaji wa mchumba wako haitwi Pascal. Alitumia hila kusajili namba ya simu kwa kutumia shahada ya mtu mwingine. Ile shahada aliiokota akaenda kujisajili nayo”
 
“Yule mwanamke amesema mume wake aliipoteza shahada yake”
 
“Sasa huyo muuaji aliiokota au aliiba, akaenda kujisajili nayo. Kwa hiyo jina hilo si la kwake na picha pia si yake”
 
“Sasa lengo lake lilikuwa nini?”
 
“Kama atafanya uhalifu kwa kutumia ile namba asiweze kupatikana. Kama ambavyo imetokea tumekwenda kumtafuta mtu mwingine ambaye tayari ameshakufa”
 
“Wahalifu ni wajanja sana na wana mbinu nyingi za kutekeleza uhalifu wao bila kuguswa na mkono wa sheria”
 
“Si wajanja, mimi nasema wajinga. Huyo jamaa nitamkamata tu”
 
“Natamani akamatwe hata leo. Ameniharibia ndoto yangu ya maisha”
 
“Ulikuwa na ndoto gani?”
 
“Nilikuwa nimepanga kumuoa Maria mwezi ujao”
 
“Sikiliza James, unaweza kupata mchumba mwingine”
 
“Hatakuwa kama yule. Pengo aliloniachia halitazibika kirahisi”
 
“Hapo ndipo ‘kusahau’ kunapopata umuhimu. Utakapoweza kumsahau Maria na kupata mchumba mwingine, huwezi kugundua tofauti”
 
Jams akatikisa kichwa.
 
“Haitakuwa rahisi sana” akasema.
 
“Haitakuwa rahisi sana lakini itakuwa. Amini hivyo”
 
Siku iliyofuata Amour alifika tena katika kampuni ya simu na kuulizia kama namba ya Pascal ilikuwa imefanya mawasiliano na namba nyingine yoyote. Akajibiwa kwamba namba hiyo ilikuwa bado haiko hewani.
 
“Naweza kupata namba zozote alizowahi kufanya nazo mawasiliano nyakati za nyuma”
 
“Zipo”
 
“Nipatieni chache tu”
 
Amour aliandikiwa namba nne tofauti tofauti ambazo zilikuwa za kampuni ile ile.
 
Alipewa karatasi iliyoandikwa namba hizo. Aliichukua akaaga na kuondoka.
 
Alipofika ofisini kwake alizijaribu namba zote nne. Tatu zilikuwa hazipatikani lakini moja ilikuwa hewani. Akaipiga.
 
Simu iliita kwa sekunde chache kisha ikapokelewa.
 
“Hallo!” Sauti iliyosikika ilikuwa ya kike.
 
“Habari?”
 
“Nzuri. Nani mwenzangu?”
 
“Nilipewa namba hii na Pascal” Amour alijaribu kumlaghai.
 
“Alikupa kwa ajili gani?”
 
“Aliniambia kama ninamuhitaji nikuulize wewe”
 
“Kwani mimi ni karani wake, mpigie mwenyewe kwa namba yake”
 
Msichana akakata simu.
 
Amour akampigia tena. Alishamuona alikuwa jeuri.
 
Msichana akapokea simu.
 
“Sasa mbona unanikatia simu, kwani wewe ni nani wake?”
 
“Kwani alipokupa namba hii alikwambia mimi ni nani wake?”
 
“Mbona tunaulizana maswali dada’ngu, kwani ukinijibu itakuwaje?’
 
“Ulichokuwa unataka wewe ni kujua Pascal yuko wapi au kujua uhusiano wetu?’
 
Amour akajidai kutoa kicheko.
 
“Umekuwa mkali sana lakini ndio tabia ya warembo wengi wa jiji hili, si kitu niambie nitampata wapi Pascal”
 
“Kwa sasa sijui yuko wapi”
 
“Ni muda gani mtakutana?” Amour aliendelea kumuuliza.
 
Msichana akang’aka.
 
“Tukutane wapi? Kwani alikwambia ana mpango wa kukutana na mimi. Wewe kama unamtaka njoo hapa saa mbili usiku. Kama atakuja kunywa utamkuta”
 
ITAENDELEA kesho Usikose

No comments:

Post a Comment