Wednesday, November 16, 2016

HADITHI, YAMENIKUTA SALMA MIE SEHEMU YA 30

 
YAMENIKUTA SALAMA  MIE
 
ILIPOISHIA
 
Nikajilaumu kwa kuchukua maamuzi ya kumkimbia mume wangu na kumuamini Chinga bila kutumia busara. Kwa kweli nilifanya kosa kubwa.
 
Lakini si hilo tu. Kulikuwa na tatizo jingine baya zaidi la kuambukizwa virusi vya ukimwi. Kama Chinga ameweza kumuambukiza mke wake,na mimi atakuwa ameshaniambukiza. Kilichobaki kwangu ni kusubiri siku virusi vitakavyoanza kufanya kazi yake.
 
Sikuweza kujua wakati huo nitakuwa wapi na sikuweza kujua nitahudumiwa na nani?.Lakini yote niliyataka mwenyewe.
Nilikuwa nikiishi vizuri na mume wangu,nikapata ushawishi wa kwenda kumfanyia dawa za mapenzi kwa tamaa ya kupata pesa. Dawa zikampofua macho mume wangu, hali ya maisha ikazorota mpaka ikabidi nimkimbie. Na huku nilikokimbilia ninakutana na makubwa zaidi kuliko yale niliyoyakimbia.
 
Wakati nikiwa katika lindi hilo la mawazo, nilisikia mlango wa chumba ukigongwa kwa kishindo. Nikajua ni yule msichana. Nikanyanyuka na kwenda kuufungua.
 
“Ulikuwa umelala?” akaniuliza.
 
“Nimejivyoosha tu, sijalala usingizi” nikamjibu.
 
“Mbona hukuniuliza nitakula nini wakati mimi ni mgeni nimekuja, unaingia ndani unalala? Kama ninataka kitu nimtume nani?.Au huyo John hakukueleza kuwa mimi ni mke wake?”
 
Maneno ya yule msichana yakanitibua. Lakini nilivuta subira.
 
SASA ENDELEA
 
“Sasa maneno mengi ya nini dada? Kwani wewe ulikuwa wataka nini?” nikamuuliza.
 
“Nataka chakula”
 
“Zungumza na huyo John, mimi sina chakula”
 
“Nina pesa yangu, nataka utoke ukaninunulie chipsi”
 
Nikaguna. Sikujua kuwa niliguna kwa nguvu mpaka akanisikia.
 
“Mbona unaguna? Wewe ni mtumishi wa John kweli au ulikuwa ni mwanamke wake?”akaniuliza.
 
“Umenionaje?” na mimi nikamuuliza kijeuri.
 
“Sikuelewielewi, mtumishi gani unatumwa unaguna, au mpaka akutume John?”
 
“Wewe nipe hiyo pesa yako nikakununulie hizo chipsi, hayo mengine tumsubiri huyo John atakapo kuja”
 
Bila shaka majibu yangu yalimtia hofu akanyamaza. Alitoa noti ya shilingi elfu tano akanipa.
 
“Kaninunulie chipsi kavu na nusu kuku” akaniambia.
 
Nilichukua ile elfu tano yake nikatoka huku nikiwa na mawazo.Niliona kama nitamkatalia anaweza kumshauri Chinga anifukuze na mimi sikuwa na pa kwenda. Nilitaka nibaki pale nyumbani nijue Chinga atachukua uamuzi gani.
 
Nilikwenda katika bar moja iliyokuwa jirani ambako palikuwa na jamaa akiuza chipsi.
 
Nikanunua sahani moja ya chipsi kavu na nusu kuku.Niliandaliwa na kutiliwa kwenye mfuko mdogo wa plastiki
 
Wakati ninarudi nilipitia dukani nikanunua vocha kwa ajili ya simu yangu na kuijaza hapo hapo. Njia mzima nilikuwa nikimlaani Chinga kwa ulaghai wake na huku nikijilaumu mimi mwenyewe kwa kuchukua uamuzi bila kufikiri.
 
Nilimkuta Vicky ameketi sebuleni akinisubiri.Alikuwa amevua nguo zake na kuvaa khanga. Alionesha kuwa alikuwa anatoka kuoga.
 
“Niwekee kwenye meza” akaniambia kisha akaniuliza. 
 
 “Kuna soda kwenye friji?”
 
“Zipo” nikamjibu huku nikielekea kwenye meza. Ndani ya moyo wangu nilimwaambia “Usijifarague dada, mimi ni mke mwenzako.Tunajaribu kukuzuga tu”
 
Pengine nilijisemea hivyo ili kujifariji na kujipa moyo kutokana na kule kudhalilishwa na kufanywa kama mtumwa.
 
Nilimuwekea ule mfuko wa chipsi kwenye meza kisha nikaenda kumtolea soda na kumuwekea.
 
Wakati ninaondoka aliniuliza.
 
“Wewe unakula nini?”
 
“Kula tu” nikamwaambia.
 
Akainuka na kwenda kwenye meza.
 
“Njoo tule” akaniambia wakati anaketi.
 
Sikumjibu. Nikaondoka na kuingia chumbani. Kabla sijakaa nikasikia akiniita kwa sauti kali. Jina langu alikuwa halijui, aliniita  “Wee msichana hebu njoo”
 
Nikatoka na kumfuata, uso nikiwa nimeukunja.
 
“Wasemaje?” nikamuuliza.
 
“Hivi ni vitu gani ulivyoniletea?” akaniuliza huku akinionyesha ule mfuko wa chipsi.
 
“Si chipsi na kuku, ama ulitaka nini?”
 
“Kuku gani! Sijui ni nyama ya nini?.Nyama hata haikukaushwa, ina damu damu! Wewe unaweza kula nyama kama hii?”
 
Aliishika na kunionyesha.
 
Nilitafuta neno la kumjibu nikalikosa.Nikabaki kumtazama.
 
“Nakuuliza wewe unaweza kula nyama hii?” akaniuliza tena.
 
Nilivuta subira. Sikutaka kulumbana naye, nikamwaambia .
 
“Bahati mbaya, sikuiona”
 
“Hukuiona kwani huna macho au umefanya kusudi,maana tangu nimekuja naona umechukia?”
 
Sikumjibu nikaondoka. Nilipoingia chumbani sikutoka tena.
Usiku kucha sikupata usingizi kwa mawazo. Mawazo yaliponizidi nilijaribu kumpigia Chinga lakini simu yake ikawa haipatikani. Nikaiacha simu na kuendelea kutafuta usingizi.
 
Usingizi niliupata kwa tabu. Nilipolala tu nikaota ndoto niko na Rita. Hafla ikanyesha mvua na hapakuwa na mahali pa kujisitiri. Tukawa tunatota. Mvua ikawa kali, maji yakajaa, nito ikawa inafurika. Rita akaniambia.
 
 “Tukimbie, maji yanakuja!”
 
Wakati nainua mguu nikateleza na kuanguka chini, Rita akakimbia peke yake na kuniacha. Maji yakawa yananifuata mimi. Karibu yangu kulikuwa na jiwe kubwa, nikapanda juu ya jiwe hilo. Maji yakazidi kujaa mpaka yakanifikia kule juu. Nikaisikia sauti ya Rita aliyekuwa amesimama juu ya mlima akinicheka.
 
Ndoto yangu ilikatishwa na kishindo cha kugongwa kwa mlango. Nikazinduka na kufumbua macho. Kulikuwa kumeshakucha. Nikaondoka kitandani na kuvaa khanga kisha nikafungua mlango.
 
Nilimkuta Vicky amesimama mbele ya mlango.
 
“Mtumishim gani unalala hadi saa mbili, hii nyumba haijafanyiwa usafi?” akaniuliza kwa kufoka.
 
“Dada mbaona unanijia juu, kwani wewe ndiye uliyenileta hapa?. Kwanza mimi sikujui, huwezi kunipa amri zako!” na mimi nikamjibu kwa kufoka vilevile.
 
Akanyea  “Yaani wewe huwezi kufanyakazi za nyumbani mpaka uamrishwe na John!” akaniuliza lakini sasa sauti yake haikuwa na nguvu.
 
“Siyo hivyo, amri zako zimezidi.Mimi mwenyewe ninajua majukumu yangu, nitafanya usafi kwa wakati wangu”
 
“Basi dada nenda kalale. Hii nyumba itakuwa chafu mpaka John atakapo kuja”
 
“Na ikae, kama usingenikuta mimi ungemuamrisha nani?”
 
“Mimi nimeshajua wewe si mtumishi wa John, usingeniletea jeuri namna hii. Na John akija unaondoka hapa nyumbani!”
 
“Utajiju…!” na mimi nikamwambia na kuufunga mlango kwa kubwata.
 
“Utajiju wewe!” Nikamsikia akinijibu huku akielekea uani.
 
 Nilikaa kitandani nikawaza kisha nikatoka kwenda msalani. Nilipotoka msalani nikashika fagio kwa hiari yangu na kuanza kufagia.Vicky alikuwa chumbani. Alitoka baadaye na kunikuta nikifagia sebuleni. Alinitupia jicho tu na kuniminyia midomo bila kunisema chochote.
 
Alikuwa amevaa nguo za kutokea na mkoba wake ulikuwa kwapani. Alipofika pale sebuleni alitoa simu yake na kuipiga. Simu ilipopokelewa nilimsikia akisema. 
 
“Kama nilivyokwambia, ndiyo natoka. Hapo jioni utakaporudi utanipitia kwa dada, sawa?”
 
Akaisikiliza kisha akaitikia na kukata simu.Aliitia simu yake kwenye mkoba akatoka.
 
Alipotoka nilikwenda kumchungulia kwa dirishani nikamuona anaelekea kwenye kituo cha daladala. Nikaendelea kumtazama mpaka alipokata kona.
 
Bila shaka walishapigiana simu na Chinga tangu akiwa chumbani. Na alimwaambia kuwa nimemjibu jeuri ndipo akapanga safari ya kwenda kwa dada yake. Nikawaza.
 
Niliacha kufagia nikaenda chumbani na kuchukua simu yangu. Na mimi nikampigia Chinga. Nilipiga kwa muda mrefu lakini Chinga hakupokea simu yangu. Jambo hilo lilinihuzunisha sana. Ikabidi nijiulize tena iwapo kweli Chinga bado alikuwa na dhamiri ya kuendelea na mimi.
 
Kutokana na dukuduku lililonipata sikutoka tena kuendelea kufanya usafi wa nyumba. Nikajilaza kitandani na kuendelea kuwaza.
 
Sikutoka mle chumbani hadi ilipotimu saa sita mchana. Nilikwenda kuchukua soda kwenye friji nikanywa na keki nilizokuwa nimeziweka jikoni kisha nikaenda kuoga.
 
Niliporudi nilimpigia simu tena Chinga lakini sasa simu yake ikawa haipatikani.Nilizidi kuumia moyo wangu na kujuta kumkubali Chinga.
 
ITAENDELEA kesho hapa hapa usikose nini kitatokea

No comments:

Post a Comment