Friday, November 25, 2016

YAMENIKUTA SALMA MIE SEHEMU YA 33

HADITHI
 
YAMENIKUTA SALMA MIE
 
ILIPOISHIA
 
Wakati tunazungumza walitokea wanaume wawili,wakajiunga na sisi. Waliagiza bia na sisi walitununulia bia moja moja. Tukawa tunakunywa huku tunazungumza. Mmoja wa watu hao alionekana kunipenda mimi na mwengine akaelemea kwa Mariamu.
 
Sikuwa na shaka kwamba walikuwa wanajua kuwa kukaa kwetu pale baa ilikuwa ni kwa ajili ya kusubiri wanaume. Kwa kweli nilikuwa nikiona aibu kwa sababu licha ya kwamba kazi yenyewe ni ya aibu nilikuwa sina uzoefu nayo.
 
Baada ya mazungumzo marefu jamaa hao wakataka tukachukue vyumba pale gesti.Wakati huo tulikuwa tumeshakunywa bia mbili mbili.
 
Niliondoka na mwenzangu Mariam kwenda upande wa gesti.Wakati tunakwenda Mariam aliniambia. 
 
“Mkiingia chumbani patana naye kabisa. Wanaume wengine hawaaminiki. Kama atataka mlale wote utamwambia akupe shilingi elfu ishirini lakini usimpunguzie chini ya kumi na tano. Na kama ni ‘short time’ ni elfu kumi na tano na isiwe chini ya elfu kumi.Umenielewa?”
 
“Nimekuelewa”
 
Mtoa vyumba alikuwa mwanaume. Mariam ndiye aliyezungumza naye.
 
“Ni vyumba vya ‘short time’ au vya kulala?” jamaa huyo akatuuliza.
 
“Hatujajua” Mariam akamjibu
 
“Atalipa nani?”
 
“Watalipa wao.Tupe hivyo  vyumba, mwenzangu atamsubiri mtu wake chumbani. Mimi nitakwenda kuwaita wakija utawauliza. Kama ni ‘short time’ au vya kulala utawatoza kabisa”
 
“Sawa”
 
SASA ENDELEA
 
Jamaa akatufunguliwa vyumba viwili. Mariam akaniambia niingie kwenye chumba kimoja nimsubiri yule mwanaume aliyenitaka mimi. Nikaingia na kuketi kitandani. Baada ya kama dakika kumi hivi mlango ukafunguliwa.Yule mwanaume akaingia.
 
“Ni mpaka asubuhi au ni short time?” nikamuuliza hapo hapo.
 
“Ni short time” akanijibu.
 
“Umeshalipa chumba?”
 
“Nimeshalipa”
 
Nikamuona anavua shati
 
“Hebu njoo ukae hapa kwanza tuzungumze” nikamwambia.
 
Mwanaume huyo aliyeonekana kuwa na pupa akaja kitandani na kuketi na mimi.
 
“Utanipa shilingi ngapi?” nikamuuliza.
 
“Wewe unataka ngapi?”
 
“Elfu ishirini” nikamjibu.
 
“Mimi nina kumi” akaniambia.
 
“Nitakufanyia kumi na tano”
 
“Sikufichi short time huwa tunalipa hiyo kumi, kulala ndiyo ingekuwa kumi na tano” jamaa akaniambia.
 
“ Kwanza mimi kulala ni ishirini, short time ndiyo hiyo niliyokuambia”
 
Nikamuaona anaendelea kuvua shati.
 
“Tukubaliane kwanza”
 
“Si umeshakunywa bia zangu mbili, ukichanganya na elfu kumi nitakayokupa ni zaidi ya hizo unazotaka” akaniambia.
 
Kwa vile Mariam aliniambia hata elfu kumi naweza kupokea kwa short time, nikamwaambia. 
 
 “Sawa”
 
 Ilikuwa siku nzuri kwa upande wangu kwani nilipata wanaume watatu wa kuingia na kutoka na mwanaume mmoja wa kulala ambaye alinipa shilingi elfu kumi na tano. Niliondoka hapo gesti saa kumi na mbili  asubuhi kurudi nyumbani.
 
Mariam alipata mwanaume mmoja wa kuingia na kutoka na mmoja wa kulala. Sikuzani alipata mwanaume mmoja tu wa kulala. Sikujua wenzangu walikuwa wamepata shilingi ngapi lakini waliniuliza mimi nimepata kiasi gani. Nikawaambia kiasi nilichopata.
 
Tuliporudi nyumbani tulipiga mswaki na kuoga. Baada ya kuvaa nilitoka. Nilikwenda kwenye bucha ya nyama, nikanunua kilo moja ya nyama. Nikaenda gengeni nikanunua kilo moja ya mchele na vitakataka vingine vya kupikia. Nikapitia dukani ambako nilinunua mikate miwili na siagi, nikarudi nyumbani na kupika chai.
 
Chai ilipokuwa tayari nikawakaribisha wenzangu tukanywa kisha tukarudia kulala mpaka saa tano tulipoamka na kuanza kushughulikia kupika.
 
Maisha yakawa hivyo. Taratibu na mimi nikaanza kuizoea ile kazi. Kuna siku nilienda kupima HIV nikaambiwa nimepata maambukizo. Kwa vile hilo nilishalijua, sikuwa na wasiwasi. Niliambiwa kinga yangu bado ilikuwa na nguvu hivyo nikatakiwa kila mwezi niende kwenye kile kituo kupima tena ili niweze kushauriwa muda wa kuanza kupata dozi ya kurefusha maisha.
 
Hata hivyo nilishauriwa nisiache kutumia kinga  (Condom) ili nisiambukize wengine na mimi nisiendelee kuambukizwa.
 
Kutokana na kazi yangu ya uchangudoa ilikuwa ni vigumu kufuata ushauri huo kwani nilikutana na wanaume ambao walikuwa hawataki kutumia kinga. Kwa vile mimi mwenyewe tayari nilikuwa muathirika niliwakubalia.
 
Zilikuwa zimepita kama wiki tatu tangu nianze kazi ile ya kujiuza ambayo kwa kweli inalipa ingawa ni ya fedheha. Usiku mmoja wakati tumeketi na wenzangu pale bar tukisubiri wateja alikuja mwanaume mmoja akatunywesha sana kisha akaondoka na Sikuzani. Sikujua walikwenda wapi.
 
Baadaye alikuja mwanaume mwingine akaendelea kutunywesha mimi na Mariam mpaka mimi nikawa sijielewi.
Nakumbuka Mariam aliondoka na yule mwanaume akaniacha peke yangu. Lakini baadaye kidogo alikuja mwanaume mwingine akawa ananisemeshasemesha.
 
Vile ambavyo nilikuwa nimelewa sana sikumbuki hata mazungumzo tuliyokuwa tumezungumza. Baadaye akaja Mariam na kunichukua. Alinishika mkono na kuniambia.
 
“Twende huku”
 
Nikamuacha yule jamaa kwenye kiti. Tulikwenda upande ule wa gesti. Mariam akaniambia.  
 
 “Kuna jamaa anataka msichana wa kulala naye na ameshaingia chumbani. Sasa wewe nenda ukalale naye”
 
“Yuko chumba gani?” nikamuuliza
 
Mariam akanipeleka mpaka kwenye mlango wa chumba hicho.
 
“Yumo humu.Yeye amelewa na wewe umelewa. Sasa mtajuana wenyewe lakini usisahau kupatana naye kabisa. Asije akakugeuka asubuhi”
 
“Sawa”
 
Nikaufungua mlango na kuingia humo chumbani. Nilimkuta huyo jamaa amejilaza kitandani. Alipoona naingia akainuka na kuketi. Na mimi nikaenda kuketi naye pale kitandani.Alikuwa amelewa sana.
 
Nilipoketi alinizunguushia mkono kiononi,akaniuliza.  “Mrembo hujambo?”
 
Nikamjibu  “Sijambo, nakuhofia wewe”
 
“Nilikuwa nataka msichana mrembo kama wewe” akaniambia.
 
“Ndiyo mimi nimeshakuja.Unataka short time au kulala kabisa?” nikamuuliza kwa sauti ya kilevi.
 
“Kulala kabisa”
 
“Utanipa shilingi ngapi?”
 
“Sijui wewe unataka shilingi ngapi?”
 
“Elfu thelathini”
 
“Elfu thelathini zote za nini? wewe msichana mbona una tamaa sana ?”
 
“Sasa utanipa ngapi?”
 
“Kwa vile ni mzuri sana nitakupa elfu ishirini”
 
“sawa”
 
Nikalala naye.
                                  
 Asubuhi kulipokucha, mimi ndiye niliyeamka kwanza. Nikaenda maliwatoni kisha nikarudi na kuvaa. Wakati ninavaa yule jamaa naye akaamka na kuketi kitandani.
 
ITAENDELEA






No comments:

Post a Comment