Monday, November 21, 2016

HADITHI , YAMENIKUTA SALMA MIE SEHEMU YA 32

HADITHI
 
YAMENIKUTA SAMLA MIE
 
ILIPOISHIA
 
Baada ya yule mtu kunieleza hayo nilipigwa na butwaa nikawa sina la kumjibu.Alipoona nimeduwaa akaniuliza. 
 
“Kwani wewe ni nani wake?”
 
“Mimi ni mtumishi wake wa ndani” nikamjibu. Jina la utumishi nilikuwa silitaki lakini sasa nililing’ang’ania kwa kujua ndilo litakalo ninasua na matatizo ya Chinga.
 
“Sasa utalazimika uondoke. Kama una madai yoyote itabidi uyapeleke polisi.
 
“Unaniambia niondoke, niende wapi?” nikamuuliza.
“Utajua mwenyewe pa kwenda. Hapo umekuja kwa hicho kibarua na kibarua kimeshaota nyasi.Tajiri yako amekamatwa na si wa kutoka leo, sasa utakaa hapa ungoje nini?”
 
Sikuwa na la kumjibu, nikabaki kimya nikiwaza.
 
“Fungasha kila kitu chako ninataka kufunga nyumba yangu” yule mtu akaniambia sasa kwa kusisitizia.
 
“Naomba unisubirishe kidogo niende kwa jirani nikamueleza matatizo yangu”
 
“Ukichelewa utakuta nimeshafunga nyumba” akaniambia.
 
“Sitachelewa”
 
Nilitoka nikaenda nyumba ya tatu kutoka ile yetu ambapo kulikuwa na mashoga zangu wawili waliokuwa wakiishi humo. Mashoga hao Mariamu na Sikuzani tulizoeana hapo hapo mtaani. Mara kwa mara tulikuwa nikitembeleana na kupiga stori.
 
SASA ENDELEA
 
Nilipofika niliwakuta wamekaa barazani wakizungumza. Nikawaeleza matatizo yaliotokea pale nyumbani kwetu. Nikawambia kwamba licha ya Chinga kukamatwa, mwenye nyumba amenifuata kunitoa akitaka kufunga nyumba yake kwa sababu anamdai Chinga kodi ya miaka miwili na pia hataki mpangaji ambae ni jambazi.
 
“Sasa umechukua uamuzi gani?” Mariamu akaniuliza.
 
“Nichukue uamuzi gani shoga na mwenye nyumba anataka nyumba yake. Itabidi nitoke na pakwenda sipajui. Sasa nilikuwa naomba nijihifadhi hapa kwenu kwa siku mbili tatu ili nijue nitaenda wapi”
 
“Na vile vitu vilivyomo mle ndani utavipeleka wapi?” akaniuliza Sikuzani.
 
“Mimi nitachukua vitu vyangu vidogovidogo tu.Vile nilivyovikuta nitaviacha. Mwenye nyumba amesema atavizuia kwa sababu anadai kodi ya miaka miwili”
 
Baada ya kunisikiliza kwa makini Mariamu akaniambia. 
 
“Sasa shoga kama unavyotuona tuko wawili na chumba chetu ni kimoja, kama utaweza kujibana humo humo chumbani kwa siku hizo tatu, karibu”
 
“Nitawashukuru mashoga zangu kwa msaada huo kwani mwenzenu nimechanganyikiwa” nikawambia.
 
“Wala usichanganyikiwe shoga. Hali hiyo ni ya kawaida Jijini hapa. Kila siku watu wanatimuliwa kwenye nyumba za watu.Wengine hutolewa nyumbo na kuwekewa nje, hawajui pa kuvipeleka. Ni afadhali wewe umesitirika”
 
“Basi mashoga zangu ngojeni nikafungashe vyombo vyangu nivilete”
 
Nikarudi nyumbani na kuanza kukusanya nguo na vitu vyangu vingine, nikavitia kwenye mabegi mawili. Begi moja lilikuwa langu mwenyewe na jingine nililichukua mle ndani. Nikachukua ndoo tatu za plastiki. Mbili nilizijaza vyombo vya kutumia kama vile sufuria, sahani, mabakuli, vikombe na kadhalika. Ndoo moja nikaitia vitu vilivyokuwemo ndani ya friji.
 
Kwanza nikapeleka begi moja kisha nikarudia jingine. Nilipomaliza mabegi, nilibeba zile ndoo. Nilitangulia kubeba ndoo mbili kisha nikairudia ile moja.
 
Nilipomaliza nilimwaambia yule mtu aliyekuwa akinisubiria kuwa nimeshaondosha vitu vyangu ingawa vingine nilivyochukua havikuwa vyangu bali nilivichukua nikaanzie maisha huko mbele ya safari.
 
Yule mtu akafunga milango ya vyumba vyote.Nikatoka naye, akamalizia kufunga mlango wa mbele kisha akaniaga na kuingia kwenye gari yake. Na mimi nikaondoka kwenda kwa mashoga zangu.
 
Mambo ya Dar ni makubwa!.Wale mashoga zangu ni wasichana warembo kweli kweli lakini nilipoingia chumbani mwao kuweka vyombo vyangu niliona hawakuwa na kitanda. Walikuwa wanalala kwenye godoro lililowekwa chini na kufungiwa chandarua. Humo chumbani mwao hamkuwa na chochote zaidi ya kimeza kilichokuwa na vipodozi pamoja na kipande cha kioo kilichovunjika.
 
Zaidi ya hapo walikuwa na ndoo karibu nne zilizokuwa na maji na madishi matatu, mawili yakiwa yamejaa vyombo. Nguo zao walikuwa wakiweka kwenye mabegi, kila mmoja alikuwa na begi lake. Kwa kweli kile chumba kilikuwa kama geto.lakini nilishukuru kupata sitara kwani sikuwa na pa kwenda.
 
Ingawa niliwaambia mashoga hao kuwa ningekaa hapo kwa siku mbili tatu, ukweli ni kuwa sikujua nitaenda wapi baada ya siku hizo. Hapo ndipo nilipoanza maisha kwa mashoga zangu hao. Habari ya Chinga nikaisahau kabisa. Kama nikudanganywa nimeshadanganywa na kama ni balaa limeshanikuta.Sikuwa na haja ya kufikiria tena yaliyopita.
 
Zile siku tatu nilizowaahidi wale mashoga zangu zikapita lakini hakukuwa na aliyeniuliza.
 
Maisha yalikuwa tofauti sana. Pale tulikuwa tunaishi kihuni. Wale wasichana tunakuwa pamoja mchana, tunapika kwa kuchangia hela na tunakula pamoja. Ikifika usiku wenzangu wananiachia chumba na tunakutana tena asubuhi.
 
Baada ya wiki mbili nikaanza kuishiwa hela ya kuchangia chakula.Wenzangu walinisaidia kwa siku tatu. Siku ya nne wakaniambia watakapo toka usiku nitoke nao.
 
Ilipofika usiku wakati wenzangu wakijipara na mimi nikajipara.Tukatoka pamoja. Hawakuwa wakienda mbali.Tulizunguuka mtaa wa pili ambako kulikuwa na baa na gesti humo humo.Tukaingia katika ile baa tukakaa kwenye viti.
 
Jinsi wenzangu walivyokuwa wakisalimiana na wahudumu wa baa ile walionekana kuwa ni wenyeji. Mara kwa mara wahudumu hao walikuwa wakiwauliza Mariamu na Sikuzani. 
 
“Mmetuletea mgeni?” na wao walijibu  “Nishoga yetu tunamtembeza tembeza”
 
Wakati tumeketi mashoga zangu wakaanza kunisomesha.Wakaniambia hapo baa ndiyo mahali wanapopatia riziki zao kutoka kwa wanaume wanaotaka huduma zao.
 
Nilivyowaelewa ni kwamba walikuwa wanajiuza. Hakukuwa na aliyeniambia wamenileta hapa kwa ajili ya gani, ilikuwa ni akili kichwani mwangu kwamba na mimi nijiunge nao.
 
Sikutaka kujivunga wala kushangaa kwa sababu kwa upande wangu maji yalikuwa shingoni. Sikuwa na namna ya kuishi katika jiji hilo.Ilibidi niwaige wenzangu ili nipate namna ya kuishi kwani sikutaka kurudi Tanga.
 
“Sasa wenzangu mnieleweshe inakuwaje?” nikawauliza huku nikilazimisha kicheko cha uongo ili wasizielewe hisia zangu kwamba jambo hilo sikulipendelea hata kidogo lakini sikuwa na budi.
 
Mariamu ndiye aliyechukua jukumu la ualimu akaniambia.
 
“Akitokea mteja akitaka kutoka na wewe, mwaambie kwanza akununulie bia unywe kiasi kidogo tu cha kukuondoa aibu na kukufanya uchangamke. Usinywe sana kiasi cha kutojitambua kwani atakwenda kukufanya vitendo visivyo na maana. Umenielewa shoga?
 
“Nimekuelewa”
 
“Ukifika huko mtakako kwenda patana naye bei kwanza. Sisi tunamuangalia mtu uwezo wake na pupa yake. Kama tumemgundua ana pesa na anakupapatikia unamtoza shilingi elfu hamsini kwenda mbele kwa kulala naye. Kama unamuona ni wa kawaida tu akikupa hata ishirini unakubali”
 
“Sasa ninamuambia anipe kabisa au….?”
 
“Anaweza kukupa kabisa au asubuhi mkitoka. Kuna wakati wa ambao, wateja hana hata elfu kumi unachukua. Na kuna wateja wengine wanatumia gesti hii hii. Unalala naye hapa hapa”
 
 
Nikawa natingisha tingisha kichwa kuonesha kumkubalia.
 
“Kuna wanaume wengine ni wa ‘short time’.Hao kwa usiku mmoja unaweza kuwapata wengi siku za mwisho wa mwezi”
 
“Na hao mnawatoza kiasi gani?”
 
“Unapatana naye. Akiingia sawasawa unamla hata elfu kumi na tano lakini isiwe chini ya elfu kumi”
 
Wakati tunazungumza walitokea wanaume wawili,wakajiunga na sisi. Waliagiza bia na sisi walitununulia bia moja moja. Tukawa tunakunywa huku tunazungumza. Mmoja wa watu hao alionekana kunipenda mimi na mwengine akaelemea kwa Mariamu.
 
Sikuwa na shaka kwamba walikuwa wanajua kuwa kukaa kwetu pale baa ilikuwa ni kwa ajili ya kusubiri wanaume. Kwa kweli nilikuwa nikiona aibu kwa sababu licha ya kwamba kazi yenyewe ni ya aibu nilikuwa sina uzoefu nayo.
 
Baada ya mazungumzo marefu jamaa hao wakataka tukachukue vyumba pale gesti.Wakati huo tulikuwa tumeshakunywa bia mbili mbili.
 
Niliondoka na mwenzangu Mariam kwenda upande wa gesti.Wakati tunakwenda Mariam aliniambia. 
 
“Mkiingia chumbani patana naye kabisa. Wanaume wengine hawaaminiki. Kama atataka mlale wote utamwambia akupe shilingi elfu ishirini lakini usimpunguzie chini ya kumi na tano. Na kama ni ‘short time’ ni elfu kumi na tano na isiwe chini ya elfu kumi.Umenielewa?”
 
“Nimekuelewa”
 
Mtoa vyumba alikuwa mwanaume. Mariam ndiye aliyezungumza naye.
 
“Ni vyumba vya ‘short time’ au vya kulala?” jamaa huyo akatuuliza.
 
“Hatujajua” Mariam akamjibu
 
“Atalipa nani?”
 
“Watalipa wao.Tupe hivyo  vyumba, mwenzangu atamsubiri mtu wake chumbani. Mimi nitakwenda kuwaita wakija utawauliza. Kama ni ‘short time’ au vya kulala utawatoza kabisa”
 
“Sawa”
 
ITAENDELEA kesho hapahapa usikose uhondo huu nini kitamtokea Salma baada ya kurubiniwa na mashoga zake.

No comments:

Post a Comment