Tuesday, November 29, 2016

YAMENIKUTA SALMA MIE SEHEMU YA 34

HADITHI
 
YAMENIKUTA SALMA MIE
 
ILIPOISHIA
 
Nilikaa pale hospitali kwa wiki mbili. Sikumuona Sikuzani wala Mariam aliyekuja kunitazama hata siku moja, wakati nilikuwa na hakika kuwa walipata habari kuwa niligongwa na gari na niko Muhimbili.
 
Baada ya wiki hizo mbili, kidonda kilichokuwa mguuni kwangu kilikuwa kimepona ingawa hakikuwa kimekauka kabisa. Kadhalika sehemu za mwili wangu nilizoumia nazo zilikuwa zimepona. Hapo hospitali nilipewa magongo mawili ya msaada ili niweze kuendea msalani.
 
Daktari aliyekuwa katika wodi yangu alinipa ruhusa lakini aliniambia niende nikatafute msaada wa pesa sehemu yeyote ile ili niweze kupelekwa India kufanyiwa operesheni ya jicho kabla ya wiki nne kumalizika.
 
Nilitoka hapo hospitali nikiwa sijui pa kwenda.Vile nilivyofikishwa pale hospitali ndivyo nilivyotoka, sikuwa na kitu chochote zaidi ya mfuko wa plastiki na shilingi elfu tano nilizosaidiwa na daktari kwa ajili ya usafiri.
 
SASA ENDELEA
 
Sikuwa na pakwenda zaidi ya kupanda daladala na kurudi kule Sinza kwa kina Mariam.
 
Nilipofika Sinza, wakazi wa nyumba niliyokuwa ninaishi waliponiona walipatwa na mshangao. Kwanza hawakunitambua mpaka nilipojitambulisha.
 
Nikaambiwa kuwa Mariam na Sikuzan hawakuwepo.
 
"Wamekwenda wapi?" nikawauliza
 
"Wamefungwa" dada mmoja aliyekuwa shoga mkubwa wa kina Mariam akaniambia. Nikashituka.
 
"Wamefungwa kwa kosa gani"?nikamuuliza.
 
"Walikamatwa usiku.Wakashitakiwa kwa kosa la kuendesha biashara ya umalaya"
 
"Ilikuwa lini?"
 
"Siku ya pili baada ya siku ile uliyopata ajali"
 
"Wamefungwa kwa miaka mingapi?"
 
"Si miaka, ni miezi sita tu kila mmoja"
 
Hapo nikajua sababu ya kutomuona Mariam wala Sikuzan kuja kunitembelea hospitali nilikokuwa nimelazwa.
 
"Siku waliyohukumiwa nilikwenda mahakamani.Mariam alinipa funguo ya chumba chao akaniambia kama utatokea nikupe"
 
"Shida yangu ilikuwa ni kutoa vitu vyangu ili niviuze nipate nauli ya kunirudisha Tanga. Siwezi tena kuishi Dar" nikamwaambia
 
"Sasa ngoja nikupe huo ufunguo"
 
Dada huyo aliyekuwa akiitwa Agnes aliingia chumbani mwake akanitolea ufunguo na kunipa.Nikafungua ule mlango na kuingia mle chumbani. Nikafungua dirisha ili niweze kuona vizuri. Agnes naye akaingia.
 
Nikaanza kukusanya vitu vyangu. Kulikuwa na mabegi yangu mawili ya nguo.Nikayafungua na kutoa nguo zote zilizokuwemo.Nilichagua nguo chache tu, nikazirudisha kwenye begi moja. Nguo zingine nikamwaambia Agnes ninaziuza.
 
"Nitafutie wateja, nataka nipate nauli"
 
"Nauli ya shilingi ngapi?"
 
"Nataka nipate kama shilingi laki moja hivi kwani huko niendako sijui kukoje. Hivi vyombo vingine pia ninaviuza,sitavichukua"
 
Agnes akachukua baadhi ya vyombo na kuchagua nguo alizozipenda, akaniuliza anipe kiasi gani.
 
"Nipe utakazo nipa dadaangu"
 
"Elfu themanini, sijui kama utaridhika nazo kwa hivyo vitu nilivyochukua"
 
"Nipe tu dadaangu"
 
Agnes aliponipa pesa hizo, nilimuambia akanitafutie wateja wengine wa kununua vile vitu vilivyobaki.
 
"Labda nichukue hizi nguo niende nazo hukohuko.Sasa niambie bei yako"
 
"Bei yoyote dadaangu,elfu kumi, kumi na tano, wewe uza tu"
 
Agnes akachukua zile nguo na kutoka nazo. Nikabaki mle chumbani kwa karibu masaa mawili. Aliporudi alikuwa hana nguo hata moja. Akanipa shilingi laki moja.
 
"Nimekwenda kuziuza kwa majirani" akaniambia.
 
"Nakushukuru dadaangu. Hivi vyombo vyangu vilivyobaki nitawaachia mashoga zangu kina Mariam.Wakitoka jela watakuja kuvikuta. Utawaambia nimetoka hospitali na nimerudi Tanga”
 
"Sawa mdogo wangu. Nitakuja kuwaambia"
 
"Tatizo langu kubwa ni huu mguu wangu uliokatwa na haya macho yangu. Hili jicho langu moja limeharibika kabisa. Hili jingine nimeambiwa limeingia kipande cha kioo huku pembeni, nalo linaweza kuharibika kama sitapelekwa India.Na siku nilizoambiwa zimebaki wiki mbili tu.Sijui nitafanya nini?"
 
"Ukifika Tanga utawaeleza ndugu zako. Natumaini watakuchangia"
Sikumjibu kitu. Niliguna tu kisha nikanyanyuka.
 
"Dadaangu ndiyo natoka naenda Ubungo. Gari lolote nitakalo lipata ndilo nitakaloondoka nalo"
 
Agnes alinishindikiza hadi kwenye kituo cha daladala.Tukaagana hapo, nikapanda daladala na yeye akarudi.
 
Nilipofika Ubungo moyo wangu ulikuwa mzito sana kurudi Tanga. Kwa muda nikawa nimesimama nikitafakari.Nilihisi kurudi Tanga ilikuwa sawa na kujimaliza kabisa.Tatizo langu sasa lilikuwa kupata msaada wa kuokoa jicho langu. Nilikuwa na uhakika kwamba huko Tanga nisingepata ndugu yeyote wa kunisaidia pesa hizo hasa kutokana na visa nilivyovifanya.
 
Kama kuna mahali pa kupata msaada, nilijiambia, ni hapa hapa Dar es salaam.
 
Nikajiuliza sasa niende wapi kutafuta msaada huo? Niende Ikulu…niende wizara ya afya…au niende kwa mbunge?
 
Wakati naendelea kutafakari nikamuona Mzee mmoja mwenye asili ya Kiasia amesimama karibu yangu akizungumza na simu. Alipomaliza kuzungumza nikamfuata.
 
“Shikamoo Baba” nilimwamkia.
 
“Marahaba” akanijibu.
 
Nilimuhisi alikuwa akinidhania kuwa nilikuwa ombaomba  niliyetaka kumuomba msaada.
 
Nikamuona akijipekua mifukoni.
 
“Sihitaji pesa baba, kuna maneno nataka kukwambia. Naomba unisikilize.” nikamwambia.
 
Mzee huyo akanishangaa kidogo.
 
 “Unasemaje?” akaniuliza.
 
“Baba kama unavyoniona nina matatizo lakini tatizo kubwa ninalotaka kukueleza ni kuhusu jicho langu hili” nikamwambia na kumuonyesha lile jicho langu linaloona.
 
“Mimi nilipata ajali ya gari hivi karibuni iliyosababisha mguu wangu mmoja ukatwe na jicho langu moja kuharibika.
 
“Sasa hili jicho langu ambalo linaona lilingia kipande cha kioo kwa pembeni. Madaktari wa Muhimbili wameniambia ni chembe ndogo sana ya kioo. Sasa tatizo liliopo ni kwamba natakiwa kupelekwa India kufanyiwa upasuaji kabla ya wiki mbili. Madakdari wameniambia baada ya wiki mbili kumalizika jicho hili nalo litaharibika kabisa na nitakuwa kipofu”
 
Yule mzeebaada ya kunisikiliza kwa makini aliniuliza.
 
“Sasa ulikuwa unahitaji nini?”
 
“Nilikuwa nahitaji msaada wa kupelekwa India kutibiwa” nikamjibu haraka .
 
“Kwani wewe huna ndugu?”
 
“Ninao lakini ndugu zangu ni maskini, hawawezi kupata pesa zinazohitajika.”
 
“Zinahitajika kiasi gani.”
 
“Nimeambiwa zinahitajika shilingi milioni nane”
 
“Bado si tatizo kwa sababu zipo taasisi zinazosaidia watu kama nyinyi. Kuna taasisi moja ya misheni ilianzishwa mwaka jana. Ishapeleka watu wengi nchini India kutibiwa maradhi yaliyoshindikana hapa kwetu.”
 
ITAENDELEA

No comments:

Post a Comment