Tuesday, December 6, 2016

HADITHI, ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 1

RIWAYA MPYA
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU
 
KIDOKEZO
 
James Matei alimshuhudia waziwazi mchumba wake Maria Temba akipigwa risasi na kuuawa, kitendo ambacho kiliyakatisha matumaini yake ya kufunga ndoa na kuoana na msichana huyo aliyempenda kuliko kitu kingine chochote.
 
Muuaji alipokamatwa na polisi, James alithibitisha kwa uchungu mwingi mbele ya polisi kuwa mtu huyo ndiye aliyempiga risasi mchumba wake. Akawataka polisi wahakikishe kuwa sheria inafuata mkondo wake.
 
Muuaji alifikishwa mahakamani na Matei alitakiwa kwenda mahakamani kutoa ushahidi, ushahidi ambao polisi waliamini ungetosha kumtia hatiani muuaji huyo.
 
Lakini Matei aliposimama kizimbani aliushangaza upande wa mashitaka alipobadilika ghafla na kumtetea muuaji huyo aliyemshuhudia akimuua mchumba wake. Akaitaka mhakama imuachie huru.
 
Hata baada ya kukumbushwa kuwa yeye ndiye aliyemthibitisha kituo cha polisi kuwa alimpiga risasi Maria na kusababisha kifo chake, James alikana maelezo yake na kusisitiza kuwa hakuwa akimtambua.
 
Mahakama ilipomuachia huru, James alimkumbatia muuaji huyo na kuishukuru mahakama kuwa imetenda haki.
 
Je imekuwaje Matei akabadilika ghafla?
 
 SASA ANZA RIWAYA HII.
 
 
 
 
HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU
 
Kujuana kwao kulitokea kama bahati nasibu. Siku hiyo James Matei alikuwa katika matembezi yake ya kawaida akiwa kwenye gari lake aina ya Rav 4. Alikuwa akipita katika katika mitaa ya Kinondoni akitokea kwenye saluni moja alikokwenda kupunguzwa nywele.
 
Ilikuwa majira ya saa kumi na moja jioni. Hali ya hewa ilikuwa imebadilika tangu saa tisa. Wingu zito lilikuwa limetanda hewani na kusababisha mwanga wa jua kutoweka  na kuwa na kila dalili ya kunyesha mvua.
 
Akiwa kwenye barabara ya Mwanamboka James alimuona msichana aliyekuwa amesimama peke yake kwenye kituo cha daladala. Wakati anakikaribia kituo hicho mvua ikaanguka ghafla. Yule msichana alianza kutota.
 
Kwa sababu tu za kibinaadamu James alipunguza mwendo akalisimamamisha gari karibu na kituo hicho. Alishusha kioo akamtazama yule msichana.
 
“Twende” alimwambia.
 
Msichana aliyekuwa amejikunja alikimbilia kwenye gari hilo akafungua mlango wa nyuma na kujipakia.
 
“Pole sana” James alimwambia msichana huyo mwembamba na mrefu wa wastani.
 
“Asante kaka” Msichana alimjibu huku akijifuta maji kwenye uso wake.
 
“Najua ulikuwa unasubiri daladala, unakwenda wapi?”
 
“Siendi tena, naomba msaada wako unirudishe nyumbani”
 
“Nyumbani ni wapi?”
 
“Twende mbele kidogo”
 
James alitia gea ya kwanza na kuiondoa gari.
 
“Mimi naitwa James, mwenzangu unaitwa nani?” James akamuuliza msichana huyo.
 
“Naitwa Maria”
 
“Bila shaka ni mwenyeji wa Arusha”
 
“Umejuaje?”
 
“Lafidhi yako ndiyo iliyonitambulisha”
 
“Mimi ni muarusha, wewe je?’
 
“Mimi ni mngoni lakini nilizaliwa Tanga”
 
“Nimefurahi kukufahamu”
 
“Na mimi nimefurahi kukufahamu. Unaishi hapa kinondoni?”
 
“Mtaa wa tatu tu utakuwa umenifikisha nyumbani”
 
Baada ya James kumfikisha katika mtaa huo, Maria alimuonesha nyumba aliyokuwa anaishi. Ilikuwa nyumba ya kota ya shirika la nyumba la taifa.
 
“Asante kaka yangu” Maria akamshukuru James wakati James alipolisimamisha gari mbele ya nyumba hiyo.
 
“Asante na wewe. Itabidi utote tena kidogo. Mlango wako uko mbali”
 
“Si kitu,  umenisaidia sana”
 
Msichana alikuwa bado amesita kwenye siti kama vile kulikuwa na kitu akikisubiri kutoka kwa James. Pengine alidhani angeombwa namba ya simu au alihisi James angetaka wakutane siku nyingine ili ampe ahadi ya uongo.
 
Kama vile James alitambua mawazo yake, alimtazama na kutabasamu.
 
“Haya, jioni njema” akamwambia.
“Asante kaka”
 
Msichana akawa kama ameruhusiwa kutoka kwenye gari, akafungua mlango na kushuka. Aliufunga tena kisha akakimbia kuelekea kwenye mlango wa nyumba hiyo.
 
James akaliondoa gari na kuendelea na safari zake. Alivyoachana na msichana huyo alikuwa kama amemuondoa akilini mwake. Hakutarajia kama angekutana naye tena na hivyo mawazo yake yalikuwa kwenye mambo yake mengine.
 
Mvua ilikuwa ikiendelea kunyesha kwa nguvu na ndiyo iliyomfanya aamue kurudi nyumbani kwake mapema. Wakati anakaribia kufika nyumbani kwake Msasani akasikia simu ikiita katika siti ya nyuma.
 
Aligundua mapema kuwa haikuwa simu yake kutokana na kuwa na mlio tofauti. Kadhalika simu yake ilikuwa kwenye mfuko wake wa shati, haikuwa kwenye siti ya nyuma. Akashituka na kugeuza uso wake nyuma. Akaona simu iliyosahauliwa kwenye siti inaita. Akajiuliza ni simu ya nani?
 
Mara moja akapata jibu kuwa huenda msichana aliyempa lifti alikuwa amesahau simu yake. Aliegesha gari kando ya barabara kisha akaishika ile simu na kuitazama. Alijiuliza aipokee au aiache?
 
Kwa sababu ya kutaka kuwasiliana na mwenyewe aliona aipokee, akaipokea.
 
“Hallo!”
 
“Hallo…samahani kaka, nimesahau simu yangu” Sauti ya msichana iliyokuwa imejaa tashiwishi ilisikika kwenye simu.
 
“Wewe ni nani?” James akamuuliza.
 
“Mimi ni yule msichana uliyenipa lifti dakika chache zilizopita”
 
“Maria”
 
“Ndiyo Maria. Nashukuru kwa kunikumbuka”
 
ITAENDELEA

No comments:

Post a Comment