Friday, May 22, 2015

SOMA MAKUBWA YALIYOJIRI MAGAZETINI LEO, MAY 22 TZ

Uchambuzi huu wa magazeti unaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya kituo cha Elimu Cha Candle Education Centre Tanga. Kituo kinaongoza kufaulisha wanafunzi kidato cha pili hadi cha sita na wanaojiendeleza kielimu. Kituo pia kiko na hostel na walimu waliobobea katika masomo. Wapo Tanga mkabala na Bank ya CRDB simu 0715 772746
EEEH
MWANANCHI
Kamati Kuu ya CCM, ambayo ndiyo inaanzisha mambo yote muhimu ya chama hicho, leo inakutana kuandaa ajenda za mkutano wa Halmashauri Kuu, huku suala linalosubiriwa kwa hamu likiwa ni hatima ya makada sita wanaotajwa kuwania urais ambao wanatumikia adhabu ya kuzuiwa kujihusisha na uchaguzi.
Kwa mara ya kwanza, CCM inakabiliwa na kazi ngumu ya kuamua hatima ya makada iliowafungiwa katika kipindi muhimu cha kuteua mgombea mpya wa urais kutokana na mwenyekiti wa sasa wa chama hicho, Jakaya Kikwete kutoweza kugombea nafasi hiyo kwa kipindi cha tatu kutokana na matakwa ya kikatiba.
Mmoja wa watu walio karibu na uongozi wa chama hicho aliiambia Mwananchi jana kuwa CCM imejikita zaidi katika kutafuta mwanachama atakayekipa ushindi kwenye Uchaguzi Mkuu, lakini suala la makada waliofungiwa ambao baadhi yao wanapewa nafasi kubwa ya kupitishwa, halitachukua muda mrefu kulijadili.
Kikao hicho kitafanyika kwenye ukumbi wa Halmashauri Kuu uliopo jengo la makao makuu ya CCM mjini hapa, maarufu kama White House mjini Dodoma.
Ukumbi huo una historia ya muda mrefu ndani ya CCM ya kutolewa kwa uamuzi mgumu katika matukio kadhaa ya kisiasa, ukiwamo ule ulioweka historia ya Aboud Jumbe kuingia akiwa Rais wa Zanzibar na mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, lakini akatoka bila cheo chochote mwaka 1984.
Pia kwenye ukumbi huo kulifanyika uamuzi wa mambo mengine makubwa, hasa nyakati za kuchuja wagombea urais au uongozi wa chama, mambo ambayo pia yanaweza kutokea katika vikao vinavyoanza leo au vya baadaye.
Alipoulizwa kuhusu kikao hicho jana, katibu wa itikadi na uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema Rais Kikwete ataongoza kikao cha leo kilichopangwa kuanzia saa 4:00 asubuhi na kwamba maandalizi yamekamilika, huku baadhi ya wajumbe wakiwa wameshawasili.
Alipoulizwa kuhusu nini wategemee wanachama na wananchi, Nape alijibu kwa kifupi kuwa watarajie kuwa “CCM watatoka wakiwa kitu kimoja” kuliko inavyotarajiwa na wengi.
Hata hivyo, mbali na hofu kuhusu hatua za kinidhamu kwa wajumbe walioadhibiwa kwa kuanza kampeni mapema na kukiuka maadili, taarifa nyingine kutoka kwa baadhi ya wajumbe wa vikao hivyo zilidai kuwa mkutano huo utajikita zaidi kuangalia utaratibu mzima wa kuchukua fomu za wagombea wote wa urais, ubunge na udiwani.
“Vikao hivi vinaangalia utaratibu tu wa jinsi ya kuchukua fomu na wala havitagusia suala la mchujo wa wagombea urais wala ubunge,” alisema mtoa taarifa huyo.
Kamati Kuu imetanguliwa na vikao vya mfululizo vya Sekretarieti na Kamati ndogo ya Kanuni.
Kamati ya Kanuni na Maadili ilitarajiwa kukutana jana usiku au leo asubuhi kabla ya Kamati Kuu.
MWANANCHI
Kitendo cha Chama cha Wananchi (CUF) kufanya uchaguzi wa Kura za Maoni katika majimbo ya Kawe na Ubungo yanayoshikiliwa na wabunge wa Chadema, kimeibua hisia tofauti miongoni mwa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Mvutano huo unatokana na kinachoelezwa ni makubaliano ya vyama hivyo kuwa kila kimoja kiandae wagombea wake katika majimbo yote ambao watashindanishwa katika Ukawa, bila kuhusisha majimbo ambayo tayari yana shikiliwa na vyama vinavyounda umoja huo.
Mbali na kigezo hicho, mgawanyo wa majimbo unazingatia matokeo ya uchaguzi wa mwaka 2010, idadi ya madiwani kwa kila chama, matokeo ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2014, mtandao wa chama nchini na nguvu ya mgombea iwapo Chadema kitamsimamisha katibu mkuu wake, Dk Willibrod Slaa kwa mara ya pili.
Juzi, CUF ilifanya uchaguzi wake wa kura za maoni katika Mkoa wa ya Dar es Salaam ambapo pamoja na majimbo mengine, iliwapitisha Leila Hussen kukiwakilisha chama hicho katika Jimbo la Kawe na Mashaka Ngole katika Jimbo la Ubungo.
Kutokana na hatua hiyo, vyama vya NCCR-Mageuzi na NLD vimesema CUF imeanza kwenda kinyume na makubaliano ya Ukawa, ingawa CUF na Chadema wameeleza kuwa haikuwa kosa kufanya kura ya maoni kwenye majimbo hayo.
Ingawa viongozi hao wametofautiana kimtazamo kuhusu hatua hiyo ya CUF, wamesisitiza kuwa kuweka mgombea mmoja wa upinzani kupitia Ukawa bado ni njia sahihi na pekee itakayowezesha kuiondoa CCM.
Mwenyekiti wa NLD, Dk Emmanuel Makaidi alisema Ukawa haijafikia uamuzi wa kuiachia Chadema majimbo ya Ubungo na Kawe, lakini CUF imekosea kuwasimamisha wagombea katika majimbo hayo kwa kuwa vikao vya kuwapata wagombea wa upinzani  bado vinaendelea.
“Ukweli ni kwamba hakuna kikao cha Ukawa kilichopitisha kuyaacha majimbo hayo kwa Chadema, ila CUF wamefanya kosa moja tu, kutangaza wagombea wake hadharani. Kama ni mchakato wa maandalizi, walipaswa kuwaanda wagombea hao ndani ya chama chao ili kusubiri uamuzi wa vikao vya Ukawa,Dk Makaidi
“Hata sisi NLD tuna wagombea wetu  Dar es Salaam, lakini hatuwezi kuwatangaza kwa sababu tunasubiri vikao vya Ukawa.”
Alipoulizwa kuna tatizo gani kumtangaza mgombea sasa huku wakiendelea kusubiri vikao vya Ukawa alijibu, “Huku ni kuwachanganya wananchi. Kama kila chama kitatangaza mgombea wake sasa halafu Ukawa ikaja na mgombea mmoja, huku ni kuchanganya watu.”
NIPASHE
Spika wa Bunge, Anne Makinda, amemzuia Waziri Mkuu Mizengo Pinda, kujibu swali la Mbunge Kigoma Kaskazini, David Kafulila (NCCR-Mageuzi), aliyehoji kwa nini mmiliki wa kampuni ya kufua umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL), Habinder Seth Singh, anaendelea kulipwa na Tanesco Sh. bilioni tano kila mwezi licha ya azimio la bunge.
Kafulila alisema: “Bado Seth anaendelea kulipwa Sh. bilioni tano (capacity charge) kila mwezi.”
Alisema moja ya maamizio ya bunge ilitaka mmiliki huyo asilipwe fedha hizo.
Kabla ya Waziri Mkuu Pinda kuanza kujibu, Spika Anne alisema: “Hili swali ni jipya kabisa, naomba Waziri Mkuu usilijibu.” Baadaye alimwita mbunge mwingine kuuliza swali.
Pia alieleza kwamba katika hukumu ya Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Uwezeshaji (ICSID), ilitaka Tanesco kutolipa kiasi hicho cha fedha, lakini mpaka sasa bado Seth anaendelea kulipwa Sh. bilioni tano kila mwezi.
Kafulila aliuliza swali hilo ikiwa ni swali la nyongeza kufuatia lile alilouliza awali kuhusu taasisi ya Serikali ya Marekani inayotoa misaada kwa nchi zinazoendelea (MCC) kusitisha kutoa msaada wa fedha baada ya mwaka jana kufanya hivyo kwa kutangaza kutotoa Dola za Marekani milioni 700 kwa Tanzania kutokana na sakata la akaunti ya Tegeta Escrow.
Alisema Waziri wa Fedha alilidanganya Bunge kwa kusema taasisi hiyo haijasitisha kutoa fedha kwa Tanzania kutokana na sakata hilo.
Lakini alisema Katibu Mkuu wa wizara hiyo hiyo, alitoa taarifa baadaye akisema taasisi hiyo imesitisha kutoa fedha ilizokusudia sababu kubwa ikiwa ni sakata la escrow.
Kafulila alitaka kujua msimamo wa serikali kuhusu uwongo uliotolewa na Waziri wa Fedha.
Akijibu Waziri Mkuu Pinda alisema; “Mbunge anataka nitoe msimamo kuhusu uwongo aliotoa waziri wangu…hili si la kwangu ni la Bunge.”
Kuhusu tatizo la bajeti ya maendeleo toka kwa wahisani, alisema limekuwa likitokea kwa kipindi cha miaka minne sasa na sio kwa sababu ya sakata la akaunti ya escrow.
NIPASHE
Kambi  Rasmi ya  Upinzani Bungeni imeshangilia kukwama  kwa Katiba mpya ikisema unabii  wao umetimia kwa kasi ambayo haikutegemewa.
Kambi hiyo imesema licha ya kuiandaa katiba hiyo kwa kutumia mafisadi, kuipitisha kwa kuipigia kura za wafu, kuipokea japo ilisusiwa na wadau wengi kilichojiri ni kwamba Rais Jakaya Kikwete, ataondoka madarakani bila kuacha Katiba mpya.
“Uhakika pekee tulio nao ni kuwa Rais Profesa Dokta Jakaya Kikwete, ataondoka madarakani bila Katiba mpya aliyowaahidi Watanzania,”  Tundu Lissu.
Akiwasilisha taarifa ya kambi hiyo jana bungeni kuhusu hotuba ya makadirio ya Bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka 2015/16 iliyosomwa bungeni jana na Waziri wake, Dk. Asha-Rose Migiro, Lissu alimnukuu Rais akiwahakikishia wananchi siku ya maadhimisho  ya miaka 50 ya Muungano mwaka jana, kuwa Katiba ingepatikana mwaka huu.
Aliiponda kuwa iliandaliwa na wajumbe wa Bunge Maalum lililojaa mafisadi watuhumiwa  wa kashfa za Escrow, Richmond/Dowans, Operesheni za Tokomeza na  Kimbunga dhidi ya Watanzania waishio mipakani.
“Ilipitishwa na kura zilizopigwa na wafu, mahujaji waliokuwa wanafanya Hijja wakimpiga shetani mawe katika Mlima Arafa, Saudi Arabia, wagonjwa waliolazwa hospitalini,”  Lissu.
Alisisitiza kuwa hii ni serikali iliyoshindwa japo CCM inadai kuwa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) uliweka mpira kwapani na kuondoka uwanjani, lakini CCM licha ya kubaki na washirika wao wameshindwa.
Lissu alihoji ni lini kura ya maoni itafanyika na kwa kutumia sheria ipi?
“Kwa maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani, kama Tume ya Uchaguzi  itasajili wapiga kura nchi nzima, hakuna  na hakutakuwa na  uhakika wa kufanyika kwa kura ya maoni kuhalalisha katiba inayopendekezwa,” .
Anasema kitakachokwamisha ni matakwa ya Sheria ya Kura ya Maoni ambayo imeweka utaratibu mgumu wa uendeshaji wa kura ya maoni, ambapo kila hatua inayotakiwa kuchukuliwa haiwezekani kuahirishwa wala kuongezewa muda.
 “NEC ilishaeleza kuwa Sheria ya Kura ya Maoni ina maeneo ambayo hayawezi kutekelezeka na baadhi yake kuwa na tafsiri zaidi ya moja yakiwamo uhesabuji wa kura ya maoni na utangazaji wa matokeo,” alisema na kuongeza:
“Suluhisho la changamoto hii ni  sheria ya Kura ya Maoni ifanyiwe marekebisho kwenye maeneo ambayo hayatekelezeki au kuwa na tafsiri zaidi ya moja.” Alisema na kuongeza kuwa hadi sasa serikali haijaleta muswada  wa marekebisho ya sheria hiyo ili kuwezesha kufanyika kwa kura ya maoni siku za usoni.
“Kama ilivyokuwa ahadi hewa ya kura ya maoni mwezi uliopita serikali inadanganya Watanzania kuwa kutakuwa na kura ya maoni katika mazingira ya sasa ya kisheria. Kwa sababu hiyo, huyu ni Waziri aliyeshindwa.
Akizungumzia bajeti finyu ya mahakama, alisema tishio kubwa kwa uhuru wa mahakama za Tanzania, sio kuingiliwa na wanasiasa na watendaji wakuu wa serikali bali ni serikali kuinyima fedha.
 “Tishio ni serikali kutumia udhibiti wake wa hazina ya taifa kuinyima mahakama rasilimali za kuiwezesha kutimiza wajibu wake kikatiba,”.
NIPASHE
Migomo ya wanafunzi wa vyuo vikuu iliyoanza juzi kuishinikiza Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) kuwalipa fedha za kujikimu, sasa imesambaa nchi nzima.
Jeshi la Polisi Wilaya ya Temeke jana lilitumia mabomu ya machozi kuwatawanya wanafunzi wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu (Duce) cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam waliokuwa wamekusanyika katika eneo la chuo hicho kwa nia ya kufanya mgomo na maandamano.
Tukio hilo lilitokea jana saa 2.00 asubuhi, baada ya polisi kufika katika eneo hilo wakiwa na silaha za moto na mabomu ya machozi.
Waziri Mkuu wa Serikali ya Wanafunzi wa chuo hicho, Bugemwe Melkizedeki, alithibitisha wanafunzi hao kutaka kufanya mgomo.
Hata hivyo, alisema yeye pamoja na viongozi wengine wa serikali ya wanafunzi wakati mgomo huo ukiandaliwa kufanyika.
Alisema wakati huo yeye na viongozi wenzake walikuwa benki wakifuatilia malipo hayo.
Melkizedeki alisema hadi kufikia saa 4.00 asubuhi jana, wanafunzi wote 3,500 walikuwa wameingiziwa fedha hizo, ambazo ni Sh. bilioni 1.3.
Alisema katika tukio hilo, wanafunzi nane walikamatwa na polisi, ambao walipelekwa katika kituo cha polisi Chang’ombe kabla ya kuachiwa kwa dhamana.
Miongoni mwa wanafunzi waliokamatwa, ni pamoja na Esau Meshack, anayesoma Kitivo cha Ualimu, ambaye alisema mgomo huo umeathiri ratiba nzima ya mtihani.
Alisema wakati mgomo huo unafanyika, alikuwa anaingia kwenye mtihani ndipo yeye na wenzake walipokamatwa na polisi.
Meshack alisema walifikishwa katika kituo hicho cha polisi, ambako walipekuliwa, huku wakipigwa virungu, makofi kwenye masikio na kudhalilishwa kwa kuvuliwa nguo.
Wakati hayo yakijiri, wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Mtakatifu Joseph jijini Dar es Salaam, Kitivo cha Ualimu wa mwaka wa kwanza wa masomo, wamepanga kufanya maandamano leo.  Tofauti na wenzao wa Duce, maandamano hayo yanalenga kushinikiza kufunguliwa kitivo hicho chenye wanafunzi zaidi ya 400 baada ya kufungwa kutokana na kudai fedha za kujikimu.
Mwanafunzi wa Sayansi ya Ualimu wa Hesabu katika chuo hicho, Mayagi Mustaph, alisema zaidi ya wanafunzi 400 wanashindwa kuingia darasani kutokana na chuo kufungwa.
Waziri wa Fedha wa Serikali ya Wanafunzi hao, Joseph Jingu, alipoulizwa kuhusiana na hilo, alisema wao kama serikali ya wanafunzi waliuomba uongozi wa chuo kukifungua kitivo ili kuruhusu wanafunzi kuendelea na masomo ifikapo Jumatatu ijayo.
Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Iringa (UoI) jana waliandamana kuishinikiza HESLB kuwapa fedha hizo, ambazo wanadai zimecheleweshwa muda mrefu na hivyo kuwafanya waishi katika mazingira magumu.
Wanafunzi hao wakitaka kuandamana chuoni hapo, huku wakitamka kuwa kama wasingeingiziwa fedha jana, lazima waandamane kuelekea kwenye ofisi ya mkuu wa mkoa.
Askari wa Jeshi la Polisi walionekana wakirandaranda maeneo ya chuo, kuanzia saa 2.00 asubuhi hadi saa 6.30 mchana wakiwa na silaha mbalimbali, yakiwamo maji ya kuwasha, mabomu ya machozi na risasi za moto.
Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Anjelina Mabula, aliwataka wanafunzi hao kutoandamana, kwani suala lao linafuatiliwa kwa karibu na HESLB.
Kuhusu wanafunzi 89 wa Chuo Kikuu cha Ruaha (Rucu) waliokamatwa na polisi juzi na kushikiliwa katika kituo cha polisi cha wilaya mkoani humo, Kamanda Mungi alisema wameachiwa kwa dhamana.
Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) wamegoma kushinikiza serikali kupatiwa fedha hizo pamoja na kulalamika kukatwa fedha nyingi kwa ajili ya Bima ya Afya.
 Mgomo huo ulianza juzi usiku na kuendelea hadi jana kwa wanafunzi wa Kitivo cha Elimu, Kozi Maalumu kwa ajili ya walimu wa masomo ya sayansi na hisabati pamoja na Kitivo cha Sanaa ya Lugha na Sayansi ya Jamii.
 HABARILEO
Katika hali isiyokuwa ya kawaida, mamia ya wanafunzi wa Kitanzania wanaosoma katika shule za msingi nchini Kenya, wameripotiwa kufukuzwa nchini humo.
Tayari 50 kati yao, wamerejeshwa nchini huku wengine kadhaa wakiwa bado wamekwama katika eneo la Narok Magharibi. Baadhi ya walioathirika ni wale ambao wako katika hatua za mwisho za kuhitimisha elimu yao ya msingi katika darasa la nane.
Vijana hao wanatarajiwa kufanya mitihani yao ya kumaliza shule Oktoba mwaka huu ; na kufukuzwa kwao kunawaweka katika wakati mgumu zaidi kimasomo.
Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Hashim Mgandilwa alikiri kuwepo na tatizo hilo na alilieleza gazeti hili jana kuwa: “Ni kweli wanafunzi wetu waliokuwa wanasoma Kenya wamefukuzwa nchini humo na 44 kati yao wamesharudi nchini, ila tuna wasiwasi kwamba mamia wengine watakuwa bado wamekwama huko na tuko mbioni kuwafuatilia zaidi.”
Meneja wa Baraza la Wafugaji katika Tarafa ya Ngorongoro, Peter Metele naye alikiri kuwepo kwa tatizo hilo na kuongeza kuwa yeye ndiye anayefanya kazi ya kwenda kuwachukua wanafunzi waliotimuliwa Kenya.
Imeelezwa kuwa chanzo cha kutimuliwa kwa watoto hao ni msuguano, ulioibuka baada ya kufanyika kwa operesheni maalumu ya kuwaondoa wahamiaji haramu kutoka nchi jirani ya Kenya, wanaodaiwa kuvamia maeneo ya Loliondo na Sale.
Hadi sasa watoto 27 wamehifadhiwa kwenye nyumba ya kulala wageni ya Cobra katika eneo la Wasso, Loliondo. Wengine takribani 10 wamepelekwa kwenye kata ya Arash na waliobakia wako majumbani mwao.
Tumewahifadhi kwenye nyumba za kulala wageni kwa sababu kuna wale wanaotoka vijiji vya mbali sana na tunataka tujitahidi kufanya mazungumzo na viongozi wa upande wa Kenya ili waruhusiwe kurejea mashuleni, iwapo tutafanikiwa basi iwe rahisi kuwarudisha Kenya,Metili.
Imedaiwa kuwa wanafunzi waliofanikiwa kurejeshwa ni wale wanaodhaminiwa na Baraza la Wafugaji na wale waliopelekwa na taasisi mbalimbali, ambao ilikuwa rahisi kutumiwa usafiri, ila kwa waliopelekwa na wazazi wao, bado wamekwama Kenya.
“Tulishafanya mazungumzo ya awali na viongozi wa upande wa Kenya siku ya tarehe 12 Mei mwaka huu, lakini ingawa tulikubaliana mengi, ikiwemo wafanyabiashara wetu kuruhusiwa kupeleka bidhaa Kenya inaonekana kuwa wananchi wa Narok wao wana maamuzi yao tofauti na serikali yao hivyo wanasisitiza kuendeleza mzozo, na sasa wameamua kuongeza tatizo kwa kuwatimua watoto,” alisema Mkuu huyo wa Wilaya.
HABARILEO
Madai ya wanawake wa wilaya ya Rombo, Kilimanjaro, kukodi wanaume kutoka nchini Kenya, baada ya kukosa huduma za ndoa kutoka kwa waume zao kwa muda mrefu, kutokana na ulevi wa gongo uliopindukia, zimemfadhaisha Mbunge wao, Joseph Selasini (Chadema).
Mbunge huyo amefikia hatua ya kusema kuwa familia yake na wananchi wa huko, wamefadhaika na kuingiwa na wasiwasi kuwa huenda wenzi wao katika ndoa zao ikiwemo ya mbunge, si waaminifu.
Selasini alisema hayo jana, alipokuwa akiuliza swali kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambapo alisema ingawa hali hiyo imewafadhaisha, lakini alitetea utengenezaji wa pombe za kienyeji, ikiwemo pombe haramu ya gongo.
Katika utetezi huo, Selasini alitaka Serikali iangalie namna ya kusaidia uboreshwaji wa pombe za kienyeji, kwa kuwa kipato chake kimekuwa kikisaidia ada za watoto, kujikimu na kuongeza kipato cha familia.
Akijibu swali hilo, Pinda alisema kwa namna Selasini anavyozungumza, huenda anatetea suala la kuhalalisha pombe haramu aina ya gongo, na kama ndio hiyo Serikali itaendelea kupiga vita utengenezaji na matumizi ya pombe hiyo kwa sababu viwango vyake havipimiki.
Mheshimiwa Selasini, kwa maelezo yako utakuwa unazungumzia gongo, sasa hii ni pombe haramu na Serikali inaendelea kuipiga vita kwa kuwa viwango vyake havipimiki.
“Lakini huenda kwa siku zijazo, jambo hili linaweza kuangaliwa na kiwanda cha Konyagi kuhusu namna ya kuiboresha kwa sababu hata Konyagi ni jamii ya gongo, lakini inapimika na haina madhara makubwa kwa watumiaji,” alisema Pinda.
Hata hivyo, katika swali la nyongeza la mbunge huyo, alimtaka Waziri Mkuu kukanusha tuhuma za Mkuu wa Wilaya ya Rombo, Lembrice Kipuyo alizotoa wiki iliyopita akidai kuwa wanawake wa wilaya hiyo, wanakodisha wanaume kutoka nchi jirani ya Kenya kwa ajili ya kuwahudumia mahitaji ya kimwili, kwa kuwa waume zao wameshindwa kutokana na ulevi uliopindukia.
“Mheshimiwa Waziri Mkuu, tunaomba kauli ya serikali kuhusu jambo hili, na mkanushe taarifa hizo kwani zimeleta mfadhaiko kwenye familia na hata familia yangu, wanandoa wana wasiwasi kwamba wenza wao wanatoka nje ya ndoa, lakini pia kauli hiyo ni ya kudhalilisha wananchi wa Rombo”,  Selasini.
Akijibu swali hilo, Pinda alisema hajasikia tuhuma hizo ;na kwamba kama zimetolewa na Mkuu huyo wa Wilaya ni vyema aliyetoa, azikanushe mwenyewe kwa kuwa ndiye anayejua alizitoa katika mazingira gani na wapi.
Aidha, alisema ni vyema apewe muda wa kulifahamu jambo hilo ;na kusema ataiagiza Ofisi ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), kuangalia jambo hilo kama Mkuu huyo wa Wilaya alichokisema, sio sahihi ili hatua nyingine zifuate.
MTANZANIA
Watu wenye ulemavu jana wamelazimika kufunga makutano ya barabara za Kawawa na Uhuru kwa kulala katikati ya taa za kuongoza magari kwa zaidi ya saa sita kama njia ya kupinga hatua ya Manispaa ya Ilala kuwavunjia meza zao za biashara katika Soko la Mchikichini.
Wafanyabiashara hao walikusanyika katika eneo hilo, hali iliyowafanya madereva wa magari wanaotumia barabara hizo kusota kwenye foleni kwa muda mrefu.
Mwenyekiti wa Umoja wa Wafanyabiashara Walemavu, Kidumke Mohamed, alisema juzi walipofika katika maeneo yao ya biashara walishangaa kukuta zaidi ya meza 200 wanazofanyika biashara zikiwa zimevunjwa na mizigo yao ikichukuliwa na mgambo wa Manispaa ya Ilala.
Alisema hawajui kuwa ni nani aliyeharibu vitu vyao, wakati Serikali iliwaruhusu kwa barua ya maandishi kufanya biashara katika soko hilo huku wakisubiri kutafutiwa eneo lingine.
“Tumeamua kufunga barabara hii ili tuweze kupata suluhu kwa viongozi wa Serikali. Hasara tumepata na haujui la kufanya mpaka sasa zaidi ya kuwa masikini,Mohamed.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Walemavu Wilaya ya Ilala, John Mleba, alisema Serikali imeamua kuvunja sheria ya makubaliano ya maandishi kwa kuwavunjia maeneo yao ya biashara.
“Tatuwezi kuondoka hapa wala kuruhusu barabara kupita hadi pale litakapopatiwa ufumbuzi wa suala letu hili la eneo la biashara na mali zetu ambazo zimeharibiwa.
“…hapa hatutoki hadi Mkuu wa Mkoa, Said Meck Sadiki atakapokuja ili kutatua suala hili, yeye ndiye aliyeturuhusu kufanya biashara katika soko hili kwa makubaliano ya maandishi, sasa tunashangaa wametufanyia hivi bila kutupa taarifa.
“Wangetupatia taarifa mapema sisi tungeondoa vitu vyetu, lakini wameviharibu na vingine wamevibeba wakati sisi tunapata fedha za kujikimu kimaisha kupitia biashara hizi,Mleba.
Kutokana na hali hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Raymond Mushi, alifika katika eneo hilo kwa lengo la kutafuta suluhu ikiwemo kuwataka wafanyabiashara hao kufungua barabara lakini alijikuta akifukuzwa.
Baada ya dakika chache, Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Ilala, naye alijikuta akifukuzwa na wafanyabiashara hao.
Wakati wa barabara hiyo ikiwa imefungwa, wafanyabiashara hao waliruhusu kupita magari ya jeshi pamoja na yale ya wagonjwa.
Ilipotimu sasa tisa alasiri uongozi wa Manispaa ulikwenda tena kuwahisi viongozi hao ili waende kukaa kikao cha pamoja ili kutafuta suluhu la mgogoro huo.
Katika kikao hicho, DC Raymond Mushi alikiri kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa lengo la kubomoa vibanda hivyo ni kupisha utanuzi wa barabara ya watembea kwa miguu katika eneo hilo.
Alisema kutokana na hali hiyo, waliafikiana kwa njia ya maandishi kwa mara ya pili kuwa wenye uwezo warudi na watengeneze meza zao na kuendelea kufanya biashara na wale wasiokuwa na uwezo wasubiri uchunguzi wa kutathmini athari zilizotokea ili walipwe fidia ya vitu vyao vilivyoharibika.
Kwa habari na matukio motomoto ni hapa hapa tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment