Tuesday, July 26, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU YA 47

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI
 
MWANAMKE 47
 
ILIPOISHIA
 
Ilikuwa kweli nilihitaji kubadili nguo. Licha ya kuwa sikuwa na nguo za kubadili, zile nilizovaa zilikuwa zimechafuka na zilikuwa zinanitia aibu.
 
Nikachagua nguo. Nilichukua shati moja  na suruali moja pamoja na viatu na soksi.
 
“Ongeza” Abdi akaniambia.
 
Nikaongeza shati moja.
 
Abdi akanichagulia mashati mengine matatu.
 
“Ongeza suruali tatu” akaniambia.
 
Nikachagua suruali zingine tatu, nikawa na suruali nne.
 
Abdi akaniita upande uliokuwa na suti.
 
Nilipokwenda alinaiambia.
 
“Mimi napenda sana kuvaa suti na wewe chagua suti moja ya kuvaa”
 
Nikatabasamu. Ilikuwa ni mara ya kwanza kukunjua uso wangu tangu ile boti tuliyokuwa tukisafiria kutoka Pemba ilipozama.
 
Abdi alipoona natabasamu akacheka.
 
“Chagua suti moja au nikuchagulie mimi?” akaniuliza.
 
Kabla sijamjibu alishachomoa suti moja ya rangi ya kijivu.
 
“Chukua hii” akaniambia.
 
SASA ENDELEA
 
Nikaichukua ile suti.
 
“Nenda kajaribu hizo nguo kwenye kile chumba pale” akaniambia huku akinionesha mlango wa chumba hicho.
 
Nikaingia kwenye hicho chumba. Unapoingia katika chumba hicho unajiona mwenyewe kwani kilikuwa na vioo vitupu. Nilizijaribu nguo zote na kuona zilikuwa sawa.
 
Nilipotoka katika chumba hicho nilimwambia Abdi.
 
“Bado viatu na soksi”
 
“Kachague jozi mbili za viatu na soksi” akaniambia.
 
Nikaenda kuchukua jozi mbili za viatu na jozi mbili za soksi.
 
Abdi alinifuata na kuninong’oneza.
 
“Chukua na chupi kumi”
 
Aliponiambia hivyo sote tukacheka.
 
Baada ya kufanya manunuzi hayo ambayo Abdi aliyalipia kwa dola za Kimarekani tuliondoka kwa gari. Tulirudi kule hoteli ambako Abdi aliniacha.
 
“Nitakupitia baadaye” aliniambia wakati nikishuka kwenye gari. Alinyamaza kidogo kisha akaongeza.
 
“Najua utahitaji kujiweka vizuri kidogo na pia kupata chakula kizuri”
 
“Ndio. Nahitaji vyote hivyo”
 
“Kwa upande wa chakula nimeshaagiza utakula unachopenda”
 
“Sawa”
 
“Mimi naondoka kidogo, nitakupitia baadaye”
 
Abdi akatia gea gari lake  na kuondoka.
 
Niliingia hotelini nikiwa na begi langu lililokuwa na nguo. Mhudumu mmoja alioniona aliniekea lile begi akapanda ngazi na kwenda kunisubiri kwenye mlango wa chumba changu.
 
Nilipofika nilifungua mlango nikamwambia.
 
“Karibu ndani”
 
Alikuwa msichana mweupe wa kisomali mwenye mwili wa kutamanisha.
 
Msichana alitabasamu akaliingiza lile begi chumbani kwangu kisha akaniaga  na kutoka.
 
Sikujua kama wasomali walikuwa wanazungumza Kiswahili. Pale hotelini niligundua baadhi ya wasomali walikuwa wanajua kuzungumza Kiswahili tena Kiswahili cha kipwani kilichonyooka.
 
Nilipobaki mle chumbani nilivua nguo nikaenda kuoga. Niliotoka bafuni nilivaa ile suti mpya aliyoninunulia Abdi. Nikajitazama kwenye kioo na kuona nilipendeza. Angalau ilinisahaulisha madhila niliyokuwa nayo moyoni.
 
Baada ya kuvaa nilishuka chini nikaingia katika eneo la mkahawa. Yule mhudumu aliyeniokea begi alinifuata.
 
 
Akanisemea kwa kisomali.
 
“Sijui hiyo lugha labda mnifundishe” nikamwambia.
 
“Unajua Kiswahili peke yake?” akaniuliza.
 
“Na kizigua”
 
“Unatoka Handeni Tanzania?”
 
“Umejuaje”
 
“Kule ndio kuna wazigua”
 
“Nasikia na nyinyi pia mna asili ya huko”
 
“Babu zetu wametoka huko lakini mimi unaniona mweupe mama yangu ni mbarawa”
 
“Mmejifundisha  Kiswahili?”
 
“Mimi nilizaliwa Garisa nchini Kenya, kule watu wanazungumza Kiswahili. Wenzangu wengine wametoka Mombasa”
 
JE NINI KITATOKEA? Usikose hapo kesho hapahapa tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment