Monday, July 25, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU YA 56

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI 0655 340572

MWANAMKE 56

ILIPOISHIA

Abdi alifungua mlango wa nyuma wa gari hilo akaniambia nijipakie. Nikajipakia.

Yeye alifungua mlango wa mbele kando ya dereva akajipakia. Gari ikaondoka.

“Tunakwenda wapi?” Mtu aliyekuwa akiendesha alimuuliza Abdi tulipoingia kwenye mitaa.

“Nipeleke hotelini kwangu nikamuweke mgeni wangu halafu utaniachia gari”

Hapo ndipo nilipoliona na kulijua jiji la Mugadishu. Ilikuwa ni kabla  ya serikali ya Somalia ya Rais Siad Barre kupinduliwa na kuanza kwa vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyoendelea hadi leo hii na kuzua vikundi vya kigaidi.

Jiji lilikuwa zuri na la kisasa. Nililifananisha sana na jiji la Nairobi ambalo niliwahi kufika.

Baada ya kupita katika barabara kadhaa, gari hilo lilisimama mbele ya hoteli moja iliyokuwa na ghorofa tano.

“Zima gari unipe funguo” Abdi alimwambia dereva wa gari hilo ambaye alilizima gari na kuchomoa funguo akampa Abdi.

“Utatumia ile gari nyingine” Abdi alisema huku akifungua mlango wa gari na kushuka.

“Amour shuka twende nikakupatie chumba”

Abdi aliniambia huku akivuta hatua kuelekea kwenye mlango wa hoteli hiyo.

Nikafungua mlango wa gari hilo na kushuka, nikamfuata Abdi Msomali.

“Hii ni hoteli yangu” akaniambia na kuongeza.

“Inaitwa Handeni Hotel”

Alipotaja jina ‘handeni’ nilishituka kidogo kwa sababu Handeni ni moja ya walaya za mkoa wetu wa Tanga.

“Inaitwa Handeni au sikukusikia vizuri?” nikamuuliza.

“Inaitwa Handeni, pia ndio jina la eneo hili tuliopo”

“Handeni ni moja ya wilaya za mkoa ninaotoka mimi”

“Ninajua. Niliwahi kusikia kuwa Wasomali wanaoishi katika eneo hili wana asili ya kizigua. Ninajua kwamba Wazigua wako Handeni au nimekosa?”

“Ni kweli. Hata mimi ni mzigua”

“Basi hapa utakutana na ndugu zako”

“Lakini ndugu zangu hao ni Wasomali?”

“Ndio ni Wasomali kama mimi lakini babu zao walitokea Handeni miaka mingi iliyopita”

“Nimekuelewa”

SASA ENDELEA

“Kama usingefika hapa ungeijuaje historia?”

“Kwa kweli nisingeijua”

Tulikuwa tumeshaingia ndani ya jingo hilo la hoteli. Tulikwenda mapokezi ambapo niligundua msomali huyo alikuwa akiheshimiwa sana na wafanyakazi wa hapo.

“Nipatieni chumba kimoja” alimwambia mmoja wa wahudumu wa mapokezi huku akiegemea kaunta hiyo.

Mhudumu huyo ambaye alikuwa msichana wa kisomali aliyekuwa amevaa sare ya koti jeusi na sketi alichukua kitabu cha wageni na kukifungua.

“Niandike jina gain bosi?” akamuuliza Abdi kwa nidhamu huku akishika kalamu.

“Niandike mimi mwenyewe” akamwambia.

“Nitumie jina gani?”

“Una maana hujui ninaitwa nani?”

“Samahani bosi, ninalijua jina lako”

Msichana aliandika kwenye kitabu hicho kisha akainua uso wake na kumtazama Abdi.

“Niandike chumba cha daraja gani?”

Abdi akanitazama. Bila shaka alikuwa akinipima kama ninastahili chumba cha daraja gani.

“Mpatie chumba cha daraja la kwanza”

Mhudumu aliandika kisha akanitazama mimi.

“Ungependa ukae ghorofa ya ngapi?”

“Ghorofa ya kwanza au ya pili”

“Nitakupatia ghorofa ya kwanza”

Msichana alijaza kwenye kitabu kisha akamtazama Abdi.

“Mgeni atakaa kwa siku ngapi”

Abdi akanitazama tena kisha akamjibu.

“Hapo paache tu…”

Msichana akageuka na kuchukua funguo.

“Nimekupatia chumba namba 85 ghorofa ya pili” akaniambia.

Sikumjibu kitu kwa sababu hicho chumba sikukitaka mimi.

“Mpeleke” Abdi akamwambia.

“Twende nikakuoneshe chumba chako” Msichana akaniambia.

Alitoka nyuma ya kaunta akaelekea kwenye ngazi.

“Mfuate akakuoneshe chumba utakachokaa” Abdi akaniambia.

Nilimfuata yule msichna. Wakati anapanda ngazi nilikuwa nyuma yake. Niliuona mwili wake. Ulikuwa wa kuvutia. Alikuwa na umbo lililofinyangwa kisomali hasa..

Nilifuatana naye hadi ghorofa ya kwanza. Akanionesha chumba namba 84. Akakifungua na  kuingia ndani pamoja na mimi.

Baada ya kukiona chumba hicho msichana alitoka na kuniacha. Kwa vile sikuwa nimepata maelezo yoyote kutoka kwa Abdi na mimi nikatoka. Nilifunga mlango nikashuka ngazi.

Nilimkuta Abdi akinisubiri mapokezi.

“Umekiona chumba?” akaniuliza.

“Nimekiona”

Akamgeukia mhudumu wa mapokezi.

“Mtakuwa mnamuhudumia kwa kila kitu muda wote atakaokuwa hapa. Mtampatia chai ya asubuhi, chakula cha mchana na cha jioni, vinywaji na kila kitu atakachohitaji ikiwa ni pamoja na kufua nguo zake na kuzipiga pasi. Bili itakuwa juu yangu” akamwambia.

“Sawa bosi, tumekuelewa”

Abdi akanitazama.

“Twenzetu” akaniambia.

Sikujua aliniambia twenzetu wapi lakini kwa vile nilishakuwa kama mateka wake sikumuuliza kitu nikamfuata.

Tulitoka nje ya hoteli tukajipakia kwenye gari lake na kuondoka.

Tukiwa ndani ya gari nilitarajia angeweza kuniambia tunakwenda wapi lakini hakuniambia kitu. Nilimuona alikuwa katika  lindi la mawazo. Sikujua alichokuwa akiwaza.

Baadaya  kukata mitaa miwili mitatu alilisimamisha gari mbele ya jingo moja  la ghorofa lililokuwa na maduka makubwa. Akaniambia tushuke.

Tukashuka na kuingia katika duka mojawapo. Wakati tunaingia aliniambia.

“Hili pia ni duka langu”

“Ahaa…kumbe pia una maduka?” nikamuuliza.

Licha ya kwamba nilikuwa na fadhaa kwa kutojua hatima yangu, nilijaribu kujichangamsha na kuzungumza naye kwa vile alionesha kama ananijali.

“Sina maduka, nina duka moja tu” akaniambia.

Tulipoingia ndani ya duka hilo nililiona lilikuwa duka kubwa la nguo za wanaume. Kulikuwa na suti, mashati, fulana, suruali na aina kadha wa kadha ya nguo za kiume.

“Angalia nguo unazopenda, upate nguo za kubadili” akaniambia.

Ilikuwa kweli nilihitaji kubadili nguo. Licha ya kuwa sikuwa na nguo za kubadili, zile nilizovaa zilikuwa zimechafuka na zilikuwa zinanitia aibu.

Nikachagua nguo. Nilichukua shati moja  na suruali moja pamoja na viatu na soksi.

“Ongeza” Abdi akaniambia.

Nikaongeza shati moja.

Abdi akanichagulia mashati mengine matatu.

“Ongeza suruali tatu” akaniambia.

Nikachagua suruali zingine tatu, nikawa na suruali nne.

Abdi akaniita upande uliokuwa na suti.

Nilipokwenda alinaiambia.

“Mimi napenda sana kuvaa suti na wewe chagua suti moja ya kuvaa”

Nikatabasamu. Ilikuwa ni mara ya kwanza kukunjua uso wangu tangu ile boti tuliyokuwa tukisafiria kutoka Pemba ilipozama.

Abdi alipoona natabasamu akacheka.

“Chagua suti moja au nikuchagulie mimi?” akaniuliza.

Kabla sijamjibu alishachomoa suti moja ya rangi ya kijivu.

“Chukua hii” akaniambia.

MAMBO YANAZIDI KUSONGA. Hebu endelea kufuatilia ujue pana siri gani hapa. KWA LEO NASAINI OFF! MAMBO NI KESHO.

No comments:

Post a Comment